Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Friday, November 21, 2014

Wazanaki na dini

Simulizi hii nimepewa na Mwalimu Jack Nyamwaga, kiongozi mstaafu wa kijiji cha Butiama ambaye pia anafahamu vyema baadhi ya matukio ya historia ya kabila la Wazanaki wa eneo la Butiama. Ni simulizi inayotoa picha kuhusu baadhi ya mila na desturi za Wazanaki.
Mwalimu Jack Nyamwaga, kulia, akiongea na Dk. Thomas Molony, mtafiti na mhadhiri kutoka Chuo Kikuu cha Edinburgh.
"Wamisionari wa kwanza waliofika hapa Butiama walikuwa Waprotestanti. Wakati huo Roman Catholic walikuwa wameshafika Nyegina [karibu na Musoma]. Hata hivyo Waprotestanti hawakuingia ndani sana kueneza dini miongoni mwa Wazanaki.

Halafu wakaja Seventh Day Adventist (SDA) na wakasema kuwa masharti ya madhehebu yao ni pamoja na wanaume kuoa mwanamke mmoja tu na waumini wao kukatazwa kunywa pombe. Hayo masharti hayakuwa rahisi kukubaliwa na Wazanaki ambao siyo tu walikuwa na desturi ya kuoa mke zaidi ya mmoja, lakini walikuwa na asili ya kunywa pombe na hata kuitumia katika mitambiko. Mwaka 1938 SDA wakahamia Busegwe [kijiji cha jirani] ambako kulikuwa na mchanganyiko wa makabila mengine zaidi ya Wazanaki. 
Halafu wakaja Mennonite na wao pia walikuwa na marufuku ya kunywa pombe. Hawa wakashauriwa kwenda Bumangi [kijiji cha jirani]. Mtemi Nyerere Burito alipoambiwa kuwa anapaswa kuwa na mke mmoja akauliza: "Hawa wake zangu 13 nitawapeleka wapi?"

Walipofika wamisionari wa madhehebu ya Roman Catholic Wazanaki wa Butiama wakapendekeza kanisa lao lijengwe Magorombe, kijiji kilicho mbali na Butiama kwenye ardhi inayotitia ikitarajiwa kuwa kanisa likijengwa hapo lintaanguka. Mmisionari aliyekwenda huko alipanda mikaratusi iliyofyonza maji na akajenga kanisa imara.

Waislamu walipokuja nao walikuwa na marufuku ya kunywa pombe. Wao wakashauriwa waende Nyamuswa kwa Mtemi Makongoro Matutu, ambaye alikuwa rafiki wa Mtemi Edward Wanzagi. Yeye aliwapokea na akasilimu. 
Kizingiti kikubwa cha kuwahi kuenea kwa dini miongoni mwa Wazanaki wa Butiama ilikuwa suala la marufuku ya kuoa mke zaidi ya mmoja na marufuku ya kunywa pombe."

No comments: