Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Friday, December 12, 2014

Mabondia na unga (sehemu ya tatu ya awamu tatu)

Promota wa ndondi za kulipwa, Ibrahim Kamwe, anaeleza kwa nini baadhi ya mabondia wanajiingiza kwenye biashara ya madawa ya kulevya.
Ibrahim Kamwe
Ukiangalia umbumbumbu na maskini tulionao mabondia, hapo wajanja wenye pesa zao, wafanyabiashara, na baadhi ya viongozi wanatumia udhaifu tulionao mabondia kutuhadaa kwa kutupatia safari za nje za kimichezo au matembezi ya kwenda kufanya mazoezi ughaibuni na hatimaye kutubebesha mihadarati (madawa ya kulevya) bila kujua kwa kutuwekea katika mizigo tunayosafiri nayo. Wakati mwingine kuna baadhi ya wafanya biashara hao wenye pesa zao hukuweka wazi wakati unaenda pigana umbebee mzigo wake na atakulipa pesa nyingi. Hapo ndipo tunapobanwa ukiangalia nyumbani tunalalia telemka tukaze, tunashindia tembele mlo mmoja, msosi wa kengele tena kwa masimango, mfukoni huna kitu na wala huna kazi itakayokupatia pesa ya kula kwa wakati huo. Hapo sijaingiza mambo ya kodi, na demu wangu namlinda vipi.

Hii njaa na umaskini tulio nao mabondia ndiyo inawapa nguvu vigogo kututumia kwa kutubebesha madawa ya kulevya kusafirisha nje wakijua wazi hatuwezi kataa kutokana na dhiki tuliyo nayo. Tutakubali tu kwani hakuna apendae kulala njaa, kulala pachafu, au kuvaa midabwada.

“Siwezi acha dili la pesa kama hili wakati jina langu kubwa kila kona linatajwa mitaani na vyombo vya habari lakini mimi binafsi nauli ya daladala sina. Siku ya tatu leo nakula mlo mmoja kwa siku, watoto hawapo katika hali nzuri, mazoezi yenyewe sifanyi kwa raha nafikiria nitapata wapi mshiko. Leo unaniletea ishu ya pesa niikatae si nitakuwa kichaa?”


“Wadau wenzangu wa ngumi ,wapambe wao, na walio karibu na sisi mabondia wana nguo za bei kubwa wanapendeza, wana magari. Ukiangalia mimi bondia ndiye mtendaji wao mkuu nipo ovyo sina kitu mfukoni wala tumboni, madeni kibao yaani majanga matupu.”

Ushauri wangu kwa serikali au taasisi zinazohusika na wanaolichukia jambo hili kiukweli - maana wengine hujifanya kulichukia mdomoni pembeni ndiyo watendaji wakuu wa kuwatumia wanamichezo au wasanii kwa faida zao - mabondia au wanamichezo tuboreshewe maeneo yetu ya michezo ikiwemo katika vilabu vyetu na maeneo ya mazoezi, na vifaa viongezwe. Ikiwezekana kodi ya vifaa vya michezo ipunguzwe ili viwe vingi nchini mabondia wasibabaike na vya kuazima au kuangalia katika TV vifaa vya wenzetu.


Serikali iwajali mabondia, isaidie kudhamini semina za walimu wa ngumi ili wawaongoze vyema vijana wao. Magym ya makusudi yajengwe na maeneo ya wazi wasigawane wenye pesa na viongozi kwa faida zao. Wajenge sehemu za michezo ya ndani, na kama pia itatumika njia ya kutoa madarasa matupu katika mashule yetu kwa ajili ya kutuachia sehemu ya mazoezi ya jioni itasaidia sana kukuza mchezo na walimu wenye taaluma kufundisha vizuri kuliko mabondia kufundishana vichochoroni na kutokuwa na nidhamu ya mchezo wala maisha.

No comments: