Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Tuesday, January 3, 2012

Maoni ya Amani Millanga kuhusu mafuriko ya Dar: sehemu ya tatu kati ya nne 

Kuhama si suluhisho pekee la kukabiliana na maafa. Suluhisho ni kujenga miundombinu inayoweza kuhimili maafa hayo ingawa naamini nguvu ya Mungu ndiyo kinga kuu. Zipo nchi kama Japan na New Zealand ziko kwenye ukanda wa tetemeko la ardhi. Indonesia takriban kila mwaka inakumbwa na tetemeko la ardhi, milipuko ya volkano na mafuriko. Uturuki, Pakistani na hata Marekani huwa zinakumbwa na athari za mitetemeko ya ardhi na mafuriko.

Ujumbe katika nchi hizi si kuhamisha watu bali ni kujenga miundombinu imara inayoweza kukabiliana na nguvu hizi za asili na walau kupunguza makali yake. Kwa Dar es Salaam sijasikia hoja ya kujenga kingo katika mto uliofurika ili kupunguza makali ya mafuriko siku zijazo. Kwa nini hatuoni hili la miundombinu na tunakimbilia kuwahamisha waathirika?


Ni ukweli uliowazi kwamba maeneo yalikotokea mafuriko ni maeneo mazuri kwa biashara na ujenzi wa majumba makubwa ya kisasa. Je, wakishahama hawa waathirika maeneo haya yatabaki kuwa wazi tu au yatagawiwa kwa matajiri na "wawekezaji" kujenga vitega uchumi vyao? Kama serikali au jiji litayagawa haya maeneo kwa wawekezaji kwa nini tunataka kuwahamisha watu hawa bila kuwapa fidia inayolingana na thamani ya maeneo yao?

Najua fika kuwa wakati huo waja, ambao serikali au jiji litasema 'maeneo haya ni mazuri kwa biashara na kwamba wawekezaji watajenga nyumba imara za kuhimili mafuriko na kujenga kingo kwenye mto na miundo mbinu ya kuzuia mafuriko'. Tutaipokea hoja hiyo kwa mikono miwili na kusahau kwamba ilifanyika dhuluma ya kuwahamisha waathirika bila kuwapa malipo. Naungana na waathirika kuidai fidia kabla ya kuhamishwa kwa haki katika maeneo yao. Natoa wito kwa serikali kuwalipa fidia waathirika. Pili natoa wito kwa Watanzania kuhakikisha kuwa waathirika wanapata haki yao. Natoa wito kwa jumuiya za kimataifa kuliangalia suala hili kwa kina na mapana yake.


Itaendelea.

No comments: