Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Friday, August 24, 2012

Mada yangu ya leo: Muungano una manufaa

Pamoja na kuwepo malalamiko mengi juu ya muungano uliounganisha Unguja na Tanganyika na kutoa Tanzania, tushukuru kuwepo kwa muungano huu kwa kutuepusha na majanga mengi.

Na wanaopaswa kushukuru zaidi ni Watanzania wa upande ulioitwa Tanganyika kabla ya tarehe 26 Aprili 1964, siku ulipozaliwa Muungano.

Bila Muungano kusingekuwepo Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ). Bila shaka ingekuwepo JWTZ lakini labda ingekuwa ni Jeshi la Wananchi wa Tanganyika.

Leo hii, makamanda wa Jeshi la Wananchi wa Tanganyika wangekuwa wakikuna vichwa kutafakari namna ya kupambana na nchi mbili: Malawi na Zanzibar. Yote hii kutokana na kutokuafikiana kwa pande mbili za Muungano kuhusu mgawanyo wa mapato yatakayotokana na mafuta yanayokisiwa kuwepo ndani ya mipaka ya Tanzania kwenye eneo la Bahari ya Hindi, na pia kutokana na madai ya Malawi kuwa eneo lote la Ziwa Nyasa ni mali ya Malawi, ikiwa ni suala linaloibuliwa na kuwepo kwa uwezekano kuwa kuna shehena kubwa ya mafuta chini ya Ziwa Nyasa. Tanzania haitambui madai hayo ya Malawi na kubainisha kuwa mpaka kati yao upo katikati ya Ziwa Nyasa.

Kwa bahati nzuri Amiri Jeshi Mkuu wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania, Rais Jakaya Kikwete, ametamka hivi karibuni kuwa mgogoro kati ya Malawi na Tanzania juu ya mpaka wa Ziwa Nyasa hautahusisha vita na kuwa utamalizwa kwa njia za kidiplomasia.

Lakini hapa tusisahau kuwa hata majeshi ya Idi Amin yalipovamia maeneo ya Tanzania mwaka 1978 Serikali ya Tanzania ilifanya jitihada kubwa za kutatua ule mgogoro kwa njia za kidiplomasia. Zile jitihada hazikufaulu kumaliza mgogoro na matokeo yake Tanzania na Uganda zikaingia kwenye vita ambayo ilileta madhara makubwa kwa pande zote mbili.

Hasara ya Uganda: gari la kijeshi lililoteketezwa na majeshi ya Tanzania ndani ya eneo la Tanzania kwenye mji mdogo wa Mutukula.
Na kwa uhakika kwa sababu ya Muungano, mgogoro kati ya Tanzania Visiwani na Tanzania Bara hautahusisha vita. Bila hivyo zingepigwa mpaka mmoja aelewe hoja ya mwenzake. Anaesema Muungano hauna faida yoyote atafakari tena.

No comments: