Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Saturday, July 26, 2014

Mada yangu ya leo: siyo kila aliye chumbani amelala usingizi

Siyo kweli kuwa kila aliye chumbani amelala usingizi. Nitafafanua.

Ninapokuwa kijijini Butiama sehemu kubwa ya kazi yangu inahusu kutangaza kijiji hiki kama kivutio cha utalii wa kihistoria na kiutamaduni. Nafanya kazi hiyo kwa taarifa ninazoweka mtandaoni na kwa mawasiliano ya moja kwa moja (kwa simu na barua pepe) na wale wanaopanga safari za kutembelea Butiama.Vitendea kazi vyangu ni kompyuta ambayo ninayo chumbani kwangu, na simu. Chumba changu ni ofisi yangu. Mimi nikisema naenda ofisini inanichukua chini ya dakika moja kufika kazini, kwa sababu ni safari ya kutoka kitandani kwangu mpaka kwenye meza yenye kompyuta.

Nafahamu wataalamu wanasema zipo athari za kuweka ofisi nyumbani lakini hiyo siyo mada yangu ya leo. Ninachosisitiza sasa ni kuwa mabadiliko ya teknolojia yamerahisisha kuhama na ofisi sehemu yoyote tunayotaka. Kompyuta na simu zimepunguza ulazima wa aina fulani za wafanyakazi kuwepo ndani ya jengo mahususi ili kutekeleza majukumu yao.
Ofisini kwangu.
Kwa bahati mbaya mabadiliko haya ya teknolojia hayako wazi kwa kila mtu. Kwa wengi kazi halisi ni inayofanyika katika sehemu mahususi, mathalani shambani, kiwandani, au ofisini, na kwa kijijini inaonekana kuwa ni kazi iwapo tu inamtoa mtu jasho.

Ukijifungia chumbani (kwangu ni ofisini) kuanzia asubuhi mpaka jioni unadhaniwa kuwa umelala usingizi. Kuna siku nilisikia mgeni anaambiwa kuwa nimelala na nikalazimika kutoka ndani kumkaribisha chumbani aliyetamka maneno hayo na kumuonyesha kuwa chumbani kwangu ni ofisini kwangu.

Kama nilvyosema siyo kila aliyekuwa chumbani amelala usingizi.

No comments: