Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Tuesday, July 29, 2014

Mwisho wa Tanzania siyo Kibaha

Kuna watumishi wengi katika sekta ya umma na ya binafsi ambao kwao Tanzania ni Dar es Salaam. Sisi tunaoishi bara hatuna tofauti na kuwa wakazi wa Kandahar nchini Afghanistan.

Nitatoa mifano. Jana nilitaka kukamilisha usajili wangu wa shahada mojawapo ya chuo kikuu kimojawapo cha Tanzania. Waliopitia zoezi hili wanafahamu kuwa maombi yote yanafanyika kwenye mtandao. Ukikwama wakati wa kujaza maombi zimetolewa namba za simu ambazo unaweza kupiga kupewa maelekezo. Nilikwama mapema kwa sababu nina stashahada ya nje ya nchi ambayo mchakato wa maombi hauitambui. Nilipiga simu hizo kwa muda mrefu lakini au hazipokelewi au haziko hewani.

Bahati nzuri nilipata namba nyingine ya Kamisheni ya Vyuo Vikuu (TCU) ambayo nilipiga na kuunganishwa na mama mmoja. Nilimueleza tatizo langu. Akaniambia kuwa TCU bado haijakamilisha tathmini ya shahada za nje na kwa hiyo nilipaswa kupeleka shahada yangu “ofisini” ili ihakikiwe.

Nilimwambia kuwa mimi niko Musoma. Akanijibu: “Sasa mimi nifanyeje?” Ilikuwa ni kama vile ananieleza: “Nani kakutuma kuishi bara?”

Sifahamu kama watu wanaopanga taratibu mbovu kama hizi wanatambua kuwa safari kutoka baadhi ya sehemu za Tanzania ni zaidi ya kilomita 1,000 hadi Dar es Salaam na inagharimu pesa. Hawa wanatoa majibu kama vile Watanzania wote milioni 45 wanaishi Dar. Naamini kuna makumi ya maelfu ya waombaji wa kusoma kwenye vyuo vikuu ambao hawako Dar. Kwanini inashindikana kuwepo mwakilishi wa Kanda ili mimi niliye Butiama nisilazimike, mathalani, kusafiri hadi Dar kuhakiki cheti changfu? Ingetosha kusafiri hadi Mwanza tu, ingawa wakati mwingine hata Mwanza pia naona ni mbali ambako ingewezekana kupanga muda maalumu wa kuonana na huyu mhakiki na gharama yake kujunuishwa kwenye gharama ya maombi. Ongezeko la gharama hii haitazidi gharama za kusafiri kwenda Dar.

Ukweli ni jukumu la serikali kuhakikisha kuwa raia wake wote wanapata huduma kwa haki na usawa ule ule. Ningekuwa na muda (na pesa) ningefungua kesi mahakamani kudai kukiukwa kwa haki zangu za msingi kama raia ambaye anastahili kupata huduma ile ile ya umma kama raia anayeishi Dar es Salaam.

Mfano mwingine, na hapa nasisitiza kwa nini nimesema kuwa hata Mwanza ni mbali, unahusu kampuni za simu. Kuna aina nyingi za matatizo ambayo yanaweza kumalizwa kwenye simu, lakini baadhi ya watoa huduma za kampuni za simu watakwambia unapaswa kwenda kwenye ofisi zao ili kutatua shida fulani.

Nagombana mara kadhaa na watoa huduma wa kampuni ya simu ya Voda. Watoa huduma wa Voda wanayo sentensi wanayopenda sana kutumia kumaliza tatizo: “Nenda Voda Shop.” Mimi kwenda Voda shop iliyo karibu ni kilomita 80 (kwenda na kurudi). Mimi nilifikiri maana ya kuwa na simu ni kupunguza ulazima wa kufunga safari zisizo za lazima, na kuongeza ufanisi katika kazi. Ukiniambia niende Voda Shop napoteza siku nzima ya kazi bila sababu ya msingi.

Halafu siku ukitoa takwimu kuwa una wateja milioni 10 na mimi pia utanihesbau katika usawa ule ule na mteja wa Dar es Salaam wakati mimi nalazimika kulipia gharama za ziada ili kutumia huduma yako?

Nasema haya siyo kwa kukosoa tu bila sababu ila kwa kutoa hoja kuwa kuna baadhi ya taratibu zinapaswa kupitiwa upya ili kutoa huduma sawa kwa mteja wa Butiama kama ambavyo anafaidika mteja wa Dar. Kuna ukweli kuwa foleni za Dar zinaweza kusababisha hata mkazi wa Dar kuona kuwa safari ya kwenda Voda Shop badi ni kero kwake. Kama hii ni kweli, basi hata yeye ana haki ya kulalamika.

Teknolojia ina manufaa ni na ingerahisisha sana shughuli za utawala na biashara nchini lakini bado ziko hitilafu nyingi za kurekebisha. La msingi ni kuwa Tanzania ni nchi kubwa na inahitaji mtazamo huo mpana kupanga mipango ya kuhudumia raia na wateja.

No comments: