Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Tuesday, November 25, 2014

Mabondia na unga (sehemu ya kwanza ya awamu tatu)

Promota wa ndondi za kulipwa, Ibrahim Kamwe, anaeleza kwa nini baadhi ya mabondia wanajiingiza kwenye biashara ya madawa ya kulevya.
Ibrahim Kamwe
Asili ya mabondia wengi  duniani wanatoka katika familia duni. Kwa mfano hapa kwetu ni nadra kumkuta bondia ametoka Upanga, Oysterbay, au Masaki ushuwani, nikiwa na maana  mabondia wengi wanatoka uswahilini. Ni watu wa hali duni. Wengi wetu hatujakalia madawati ya shule na wengine tuliojitahidi tumefika darasa la tano au sita. Kama wazazi walikomaa ndiyo tunamaliza la saba.

Baadhi yetu tukiwa na umri wa kuanzia miaka sita nyumbani huwa tunaanza kupewa uzowefu wa kuuza visheti, maandazi, vitumbua, karanga n.k. na vikibaki nyumbani hauli chakula mpaka viishe. Shuleni mwalimu mkali, darasani hafundishi mpaka usome tuisheni ndiyo unapata kufundishwa kidogo, na ukishindwa maswali yake unapata viboko vya ghadhabu. Hapo ndipo tunapoamua kuachana na shule na kutinga mitaani. Michezo yetu ni katika madampo na vichochoroni na tukifikia umri wa kuanzia miaka 12 na kuendelea tunajua jinsi ya kutafuta pesa kwa kuuza njiwa, kucheza kamari, malani, kuiba kuku na bata, na kwa wale walio watukutu zaidi kuuza na kuvuta bangi ni sehemu ya maisha ya kawaida tu huku mitaani kwetu.

Mara nyingi mlo kwetu ni mmoja tu kiubishoo au kuwa wageni ndiyo tunakula milo miwili. Katika maisha yetu muda mwingi tupo huru na michezo kuliko kusoma, hasa kolokolo, ngoma, mpira, na ngumi. Mpira tunacheza mabarabarani, vichochoroni, na kwenye madampo, wakati ngumi tunajifundisha katika makamali, vichochoroni, au uwani kwa kina masta. Begi au tairi linafungwa juu ya mti, tizi linaendelea bila vifanyio vya mazoezi vilivyo rasmi. Mwendo mdundo tunasonga na tunashinda au kufanya vizuri katika mashindano yetu tunayoshiriki na hali yetu duni hii hii ya kimaisha, na majina yetu kutangazwa sana katika vyombo vya habari na kupata umaarufu mkubwa nchini, nchi jirani na hata nchi za Ulaya.

Lakini ukibahatika kututembelea na kuangalia tunapoishi na familia zetu na umaarufu tuliyonao, utakuta maisha yetu mabovu na yanasikitisha.

(itaendelea na sehemu ya pili)

sehemu ya pili ya makala hii

Friday, November 21, 2014

Wazanaki na dini

Simulizi hii nimepewa na Mwalimu Jack Nyamwaga, kiongozi mstaafu wa kijiji cha Butiama ambaye pia anafahamu vyema baadhi ya matukio ya historia ya kabila la Wazanaki wa eneo la Butiama. Ni simulizi inayotoa picha kuhusu baadhi ya mila na desturi za Wazanaki.
Mwalimu Jack Nyamwaga, kulia, akiongea na Dk. Thomas Molony, mtafiti na mhadhiri kutoka Chuo Kikuu cha Edinburgh.
"Wamisionari wa kwanza waliofika hapa Butiama walikuwa Waprotestanti. Wakati huo Roman Catholic walikuwa wameshafika Nyegina [karibu na Musoma]. Hata hivyo Waprotestanti hawakuingia ndani sana kueneza dini miongoni mwa Wazanaki.

Halafu wakaja Seventh Day Adventist (SDA) na wakasema kuwa masharti ya madhehebu yao ni pamoja na wanaume kuoa mwanamke mmoja tu na waumini wao kukatazwa kunywa pombe. Hayo masharti hayakuwa rahisi kukubaliwa na Wazanaki ambao siyo tu walikuwa na desturi ya kuoa mke zaidi ya mmoja, lakini walikuwa na asili ya kunywa pombe na hata kuitumia katika mitambiko. Mwaka 1938 SDA wakahamia Busegwe [kijiji cha jirani] ambako kulikuwa na mchanganyiko wa makabila mengine zaidi ya Wazanaki. 
Halafu wakaja Mennonite na wao pia walikuwa na marufuku ya kunywa pombe. Hawa wakashauriwa kwenda Bumangi [kijiji cha jirani]. Mtemi Nyerere Burito alipoambiwa kuwa anapaswa kuwa na mke mmoja akauliza: "Hawa wake zangu 13 nitawapeleka wapi?"

Walipofika wamisionari wa madhehebu ya Roman Catholic Wazanaki wa Butiama wakapendekeza kanisa lao lijengwe Magorombe, kijiji kilicho mbali na Butiama kwenye ardhi inayotitia ikitarajiwa kuwa kanisa likijengwa hapo lintaanguka. Mmisionari aliyekwenda huko alipanda mikaratusi iliyofyonza maji na akajenga kanisa imara.

Waislamu walipokuja nao walikuwa na marufuku ya kunywa pombe. Wao wakashauriwa waende Nyamuswa kwa Mtemi Makongoro Matutu, ambaye alikuwa rafiki wa Mtemi Edward Wanzagi. Yeye aliwapokea na akasilimu. 
Kizingiti kikubwa cha kuwahi kuenea kwa dini miongoni mwa Wazanaki wa Butiama ilikuwa suala la marufuku ya kuoa mke zaidi ya mmoja na marufuku ya kunywa pombe."