Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Wednesday, May 1, 2013

Ukarimu wa Watanzania unatoweka

Enzi zilizopita utamaduni wa Mtanzania ulihusisha pia ukarimu. Leo hii utamaduni huo unatoweka.

Nianze kwa tukio lililonitokea yapata miaka 27 iliyopita. Nilikuwa nasafiri kutoka Arusha kuelekea Butiama nikiendesha gari nikiwa peke yangu. Nilitoka kwenye lango la Ikoma la Hifadhi ya Serengeti jioni na mvua kubwa ilikuwa inanyesha. Kwa sababu kiza kilikuwa kimeingia na kwa sababu barabara ilikuwa mbaya sana kutokana na mvua na ilikuwa dhahiri gari ingeweza kuzama kwenye matope na kusababisha nilale porini, nilipofika Fort Ikoma niliamua kuelekea Mugumu ili niweze kulala huko na kuendelea na safari kesho yake.

Kutokana na mvua kubwa iliyoendelea kunyesha, barabara kati ya Fort Ikoma na Mugumu nayo ilikuwa mbaya sana lakini Landrover 109 niliokuwa naendesha ilimudu kukabiliana na hali mbaya ya barabara ingawa mara kadhaa ilielekea kunasa kwenye matope. Katikati ya safari yangu kuelekea Mugumu, ikiwa imepita saa 3:00 usiku na nikiwa katikati ya pori, nilikutana na mtu mmoja akitembea kwa mguu ambaye aliashiria kunisimamisha na kuomba nimchukue. Nilisimamisha gari kumchukua. Alikuwa anaelekea Mugumu.
File:Land Rover Series III 109.JPG
Aina ya gari niliyoendesha siku hiyo. Picha: Buckers.
Nakumbuka tulifika Mugumu baada ya saa 5:00 usiku na sikufanikiwa kupata chumba kwenye hoteli za Mugumu. Zote zilikuwa zimejaa. Yule mtu niliyemchukua porini alinuchukua mpaka anakoishi akanipisha chumba chake nikalala mpaka asubuhi na kuendelea na safari yangu ya kuelekea Butiama. Bila yeye ningelala ndani ya gari.

Hiyo ndiyo Tanzania ya zamani. Ya watu wenye kuaminiana na wenye ukarimu ambao leo hii ni vigumu kuuona. 

Pamoja na kuwa miaka 27 iliyopita nilisimamisha gari katikati ya pori na kumpa msaada mtembea kwa miguu ambaye sikuwa namfahamu, nakiri kuwa leo hii nitasita kusimamisha gari mchana kumchukuwa mtu nisiyemfahamu katika eneo lolote la Tanzania. Na hata yule mtu aliyenipisha kitanda chake sidhani kama leo hii atathubutu kukaribisha mtu asiyemfahamu alale chumbani kwake bila kuwa na hofu kuwa mgeni wake atahama na baadhi ya mali zake.

Imani inatoweka na ukarimu unafifia kutokana na mabadiliko ndani ya jamii ambayo yameleta Watanzania wasiyothamini uhai wa binadamu wenzao na hivyo kusababisha kubadilika kwa mila na desturi ambazo tulizoea zamani.

No comments: