Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Saturday, November 16, 2013

Hatua kumi za mauaji ya kimbari: 1 na 2

Nimetembelea Rwanda hivi karibuni na nikiwa huko nilipata fursa ya kutembelea mojawapo ya vituo vya kumbukumbu ya mauaji ya kimbari ya mwaka 1994.

Jambo moja la msingi ambalo Watanzania tunaweza kijufunza ni kuwa maafa yaliyotokea Rwanda yanaweza kutokea pia Tanzania. Kwa mujibu wa wachunguzi wa sababu zinozogeuza binadamu mmoja kuwa adui wa binadamu mwenzake na hata kufikia hatua ya kumaliza uhai wa mwenzake ziko duniani kote.

Sababu hizi zinaanza na mchakato wenye hatua nyingi ambao hufikia mauaji kama yale yaliyotokea Rwanda. Kinachozuwia maafa kama hayo kutokea ni hatua mahususi zinazopaswa kuchukulia na jamii za kukatisha uendelezwaji wa huo mchakato.

Kwa mujibu wa Dr. Gregory Stanton wa Genocide Watch, hatua za viashiria vya kuwepo kwa mchakato na za kuzuwia maafa kama ya Rwanda ziko kumi.

Hatua ya Kwanza: Uainishaji

Hapa inafanyika jitihada ya kuainisha makundi ndani ya jamii, "sisi na wao." Ubaguzi unaweza kuchukua njia mbalimbali kama vile dini, kabila, utaifa, na hata matabaka ya jamii.

Uainishaji unasaidia kuwagawa watu na kurahisisha kampeni za mapambano dhidi ya kundi mojawapo ndani ya jamii.

Mifano: Tanzania tumeshaanza kujipambanua kwa dini zetu kwa muda mrefu sasa, pamoja na kwa maeneo tunayotoka. Aidha, "wa bara na wa visiwani" umekuwa wimbo mashuhuri wa miaka ya hivi karibuni.

Hatua za kuepuka uainishaji: Kusisitiza utaifa zaidi kuliko makundi. Kuweka mkazo kwenye matumizi ya lugha moja inayounganisha wote, mfano Kiswahili. Kupinga kwa nguvu zote wanasiasa na vyama vya siasa vinavyoendeleza siasa za kibaguzi.

Hatua ya Pili: Uashiriaji

Hapa zinatumika alama au ishara zinazoweka mkazo wa kubainisha makundi yaliyoainishwa katika hatua ya kwanza.

Mifano: Wakristu dhidi ya Waislamu, Wazanzibari dhidi ya Watanzania bara; Itikadi nazo zinaweza kutumika kama nyenzo za kubaguana: walalahoi dhidi wa wala nchi, Wadanganyika dhidi ya Wadanganyaji, n.k.

Hata nguo zinaweza kutumika kubaguana: magwanda dhidi ya wale wa kijani na njano. Nimeshuhudia picha ya makada wa chama kimoja cha siasa wakimshambulia mwanachama wa chama tofauti kwa mawe na matofali.

Hatua za kuepuka uashiriaji: ni pamoja na kuondoa uainishaji wa kidini au kikabila kwenye vitambulisho vya aina zote. Mpaka leo hii Mtanzania yoyote anayetoa taarifa kwenye kituo cha polisi anapaswa kutaja dini na kabila lake.
Vitambulisho vya Rwanda vilitoa taarifa za kabila la mwenye kitambulisho na vilitumika kuwasaka wahanga wa mauaji ya kimbari ya mwaka 1994.
Aidha, kupinga matumizi ya maneno au majina yanayodhalilisha kundi lolote ndani ya jamii.

Itaendelea na:
  • Hatua ya Tatu: Ubaguzi
  • Hatua ya Nne: Udhalilishaji wa Binadamu
Taarifa nyingine inayohusiana na hii:

No comments: