Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Friday, November 1, 2013

Mtwara sawa lakini Loliondo hapana?

Nimekuwa na msimamo unaofanana kidogo na sera ya serikali juu ya rasilimali za Tanzania; kwamba ni mali ya Watanzania wote, na siyo ya wale walio karibu na hiyo rasilimali. Sikubaliani na hoja kuwa wale wananchi walio karibu na rasilimali ndiyo wapewe upendeleo zaidi juu ya kufaidika na rasilimali hiyo.

Sababu yangu ya msingi ni kuwa kufanya upendeleo wa aina hiyo kutajenga ubaguzi dhidi ya Watanzania wengine. Watanzania wengine wataonekana kuwa "wanaingilia" rasilimali inayopaswa kutumika na wale wazawa wa eneo husika tu. Na ndiyo maana napata shida kuunga mkono hoja ya baadhi ya Watanzania, kama wale wananchi wa Mtwara, wanaodai rasilimali ya gesi ni yao kwanza.

Lakini hatuwezi kusema hatuelewi kwanini kuna madai kama yao. Unaweza kujenga hoja nzuri kuzungumzia kwanini wananchi wa Mtwara wanaamua kuwa gesi ya Mtwara ni yao. Ni ubovu wa sera za muda mrefu za serikali zilizopuuza umuhimu wa kuhakikisha kuwa Watanzania wanafaidika na rasilimali yao. Haya ni matokeo ya muendelezo ule wa sera zinaotoa vipengele vya upendeleo kwa wawekezaji na ulipaji wa mrahaba pekee. Mwekezaji aliweza kumiliki asilimia 100 ya mradi wa rasilimali muhimu na kuilipa serikali au kodi kidogo au kusamehewa kabisa na kiwango cha mrahaba ambacho, kimsingi, kilikuwa kidogo sana.

Wananchi waliofundishwa miaka nenda rudi kuwa yatosha kutoa misamaha ya kodi kwa wawekezaji na malipo ya mrahaba wa chini ya asilimia tano hawakuelewa hilo somo na hawataweza kulielewa hata kwa karne nzima. Matokeo yake ni kupoteza imani kabisa kwa serikali na maamuzi yoyote inayoyafanya kwenye eneo la uwekezaji. Tunachoshuhudia sasa ni wananchi "kuchukua chao mapema"; kwamba rasilimali ambazo ziko jirani nao ni lazima ziwape faida wao. Watanzania wengine wahangaike na mali zilizopo maeneo yao. 

Huu ni mwanzao wa kuparaganyika kwa nchi. Wale wasio na rasilimali watakula wapi? Watapata ajira wapi? CHADEMA wamejaribu kuelezea namna utaratibu wa kila mtu na chake (majimbo) na kidogo kilichopo kipelekwe kwenye serikali kuu lakini kwangu mimi sera hii ina walakini kuwa itaanza kupandikiza hisia kuwa Mlima Kilimanjaro una wenyewe. Hali kadhalika Serengeti, Selous, na mbuga nyingine ambazo zinaliingizia Taifa mabilioni ya shilingi kila mwaka. Vivyo hivyo kwa gesi na mafuta yanayosubiriwa kwa hamu.

Badala ya kuitaka serikali iwajibike zaidi katika kuwanufaisha wananchi wake, tunaanza kugawana kile kidogo kilicho jirani yetu. Ni sawasawa na wenyeji kugombania makombo baada ya chakula kutengewa wageni.

Kutegemea kuwa jambo litatokea (ubaguzi wa watu kutokana na maeneo yao ya asili) hakuthibitishi kuwa jambo hilo kweli litatokea. Lakini binadamu wote tunaishi kwa kufanya maamuzi kuhusu yaliyokwisha tokea zamani, ya sasa, na matarajio yetu ya yale yanayoweza kutokea. Ndiyo msingi wa mipango yote thabiti, kwa hiyo siyo rahisi kujenga hoja kupuuza hoja za aina hii.

Sasa basi tugeukie Loliondo. Wakati siungi mkono madai ya wananchi wa Mtwara naunga mkono madai ya wale wa Loliondo ambao wanapinga kusudio la serikali la kutenga kilomita za mraba 1,500 kwa wawekezaji kwa shughuli za utalii, pamoja na serikali kutaka watu hao wahame kupisha shughuli za uwekezaji. Wamasai wapatao 30,000 na ng'ombe zao wahamishwe ili kupisha shughuli za utalii.

Bado nina msimamo kuwa Tanzania ni ya wote lakini kwa wakazi wa tarafa ya Loliondo, ambao wengi wao ni wafugaji na wanaoishi maisha yanayotegemea sana ardhi wanayokalia kwa ustawi wao na wa mifugo yao, kugawa hayo maeneo kwa matumizi ya wawekezaji ni kuwanyima Watanzania hawa chanzo cha msingi kinachobeba mfumo wao wa maisha.

Hii ni sawa na kuhatarisha uhai wao. Hasara atayopata mkazi wa Loliondo atakayehamishwa haiwezi kamwe kufidiwa na kiasi chcochote cha pesa, hata kama pesa hizo zisingieishia serikalini na zikagawiwa kwa wakazi hao.

Mkazi wa Mtwara ana haki kuhoji serikali ionyeshe faida kwake (na kwa Watanzania wengine) ya sera ya muda mrefu ya uwekezaji, lakini hata kama madai ya kuweka Mtwara viwanda muhimu vya sekta ya gesi haitatimizwa, maisha ya mwana-Mtwara hayatabadilika kwa kiasi kikubwa kulinganishwa na athari na matatizo makubwa ambayo atayapata mkazi wa Loliondo ambaye maisha yake yataathrikia kutokana na kuhamishwa kwenye ardhi ambayo anaitegemea kila siku kwa maisha yake na kwa mifugo yake.

Katika mazingira haya, madai ya wananchi hawa wa Loliondo ni sahihi kabisa, kwa maoni yangu. Ya Mtwara bado yanahitaji kujengewa hoja zaidi.

Taarifa nyingine zinazohusiana na hii:
http://muhunda.blogspot.com/2010/09/john-mnyika-wa-chadema-anajibu-hoja.html
http://muhunda.blogspot.com/2010/10/amani-millanga-bado-anahoji-sera-ya.html

No comments: