Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Wednesday, November 20, 2013

John Kitime aelezea historia yake

Zamani, kwenye miaka ya tisini, niliwahi kumiliki gazeti lliloitwa Sanaa na Michezo ambalo lilichapisha makala kuhusu maisha ya mwanamuziki John Kitime, ambaye sasa hivi yuko na Kilimanjaro Band, Wananjenje.

Wakati huo aliwasilisha maelezo yake ambayo yalitumika kuandika makala fupi iliyochapishwa kwenye gazeti hilo.

Huyu hapa tena, John Kitime, akielezea maisha yake ndani ya muziki.
"Nilianza kwanza kupiga gitaa mwaka 1968 nikiwa kwenye mwaka wangu wa kwanza wa shule ya sekondari. Tangu napata kumbukukumbu tulikuwa na gitaa nyumbani wakati wote. Baba yangu alipiga gitaa tangu alivyokuwa mdogo. Yeye ni mtaalamu wa nyimbo za asili na ana mamia ya tunzi ambazo kwa bahati mbaya hazijarekodiwa.

Mwaka 1968 nilianza masomo yangu ya sekondari na baba yangu aliniruhusu kupiga gitaa. Alikuwa ni mtu aliyesisitiza masomo kwanza.

Mwaka 1975 niliunda bendi ndogo kwetu Iringa na baadhi ya wanachama wa bendi hiyo waliendelea kimuziki na kupata umashuhuri mkubwa. Wawili kati yao, Ally Makunguru na Nicholas Mlapone, wako nje ya nchi. Makunguru yuko Mombasa, Kenya na Mlapone yuko Ujerumani.Kundi hili hili ndiyo lilikuwa chimbuko  ya bendi kubwa, Tancut Almasi Orchestra.

Mwaka 1980 niliondoka Iringa na kuelekea Dar es Salaam na nilianza kufanya kazi kama msomaji wa prufu wa gazeti la Daily News. Wakati wa ziada nilikuwa mwanamuziki wa bendi ya Osheka, bendi ambayo ilivunjika mwaka 1981. Lakini ilikuwa bendi ambayo ilikuwa na wanamuziki wazuri sana kama Martin Ubwe ambaye sasa hivi ni kiongozi wa bendi ya Mionzi ambayo iko Mbeya, na Sammy Mhina ambayo ni mpiga ngoma wa Heart Strings Band.

Mwaka 1983 nilipata fursa ya kuigiza kwenye sehemu ndogo ya filamu inayoitwa Wimbo wa Mianzi iliyotolewa kwa ushirikiano kati ya Kampuni ya Filamu Tanzania na One World Production (OUP), kampuni ya Uholanzi. Nilipewa pia mkataba wa kutunga nyimbo kwa ajili ya filamu hiyo.

Ilikuwa wakati natafuta wanamuziki wa kurekodi muziki wa filamu hiyo ndipo nilikutana na Tchimanga Assosa, mwanamuziki mashuhuri wa Congo ambaye aliwahi kupiga muziki na bendi ya Lipua Lipua na Orchestra Kamale, ambaye alikuwa anakusudia kuunda bendi na tukaunda bendi iliyoitwa Orchestra Mambo Bado. Nillikuwa na bendi hiyo kwa miaka miwili.

Baada ya hapo nikajiunga na Orchestra Makassy iliyomilikiwa na Mzee Makassy. Bendi hii wakati huo ilikuwa na mwanamuziki Fan Fan Mosesengo (aliyekuwa na Marehemu Lwambo Luanzo Makiadi} na pia Remmy Ongala, ambaye sasa amejijengea jina kubwa akiwa na Orchestra Super Matimila. Sasa hivi Fan Fan yuko London (Uingereza) akiongoza bendi yake mwenyewe, Somo Somo. Pia mwanamuziki mwingine aliyeunda Orchestra Makassy alikuwa Kinguti ambaye sasa yuko na Bicco Stars.

Baada ya hapo nikaunda bendi yangu mwenyewe, TX Seleleka. Nilipata vyombo kutoka kwa rafiki yangu Mholanzi Kick Van den Hevel ambaye baadaye tena alichukua vyombo hivyo hivyo na kuanzisha bendi ya Tatunane. TX Seleleka ilipiga muziki hoteli ya New Africa kama bendi ya hoteli kwa mwaka mmoja halafu ikavunjika baada ya Kick kuchukua vyombo vyake.

Mwaka 1986 nilirudi Iringa nikawa mwanamuziki mwanzilishi wa Tancut Almasi Orchestra bendi ambayo ilikuwa inaundwa na wanamuziki miongoni wa waliyo bora kuliko wote nchini: Kasaloo Kyanga na Kyanga Songa, mapacha wa Ki-Congo waimbaji; wapiga gitaa wawili Shaban Yohana, ambaye sasa hivi ni kiongozi wa Vijana Orchestra, na Kawelee Mutimwana, kiongozi msaidizi wa MK Group; Mafumu Bilali, mpiga saksafoni mahiri ambaye sasa yuko Japani na Zanzibar Sound;kinanda wakati huo kilipigwa na Abdul Salvador, kiongozi wa Washirika Stars, na wanamuziki wengine wengi ambao wameendelea kuwa na sifa kila walipoenda.

Mwaka 1990 nyimbo zangu mbili nilizotunga nikiwa na Tancut, Lungulye na Afrika Nakulilia, zilishinda mashindano ya Top Ten Show zikichukua nafasi ya kwanza na na pili. Nilishinda zawadi ya redio kaseti ya National ambayo nasikitika nililazimika kuiuza ili kupata pesa za kurekodi hii kaseti yangu ya sasa.

Nyimbo nane kwenye hizi ninazorekodi sasa ni uzoefu wangu kutoka kwenye hii miaka yote, bila kusahau ushawishi wa baba yangu. Hii nyimbo Ifipwepo ni utunzi wa baba yangu, nikiwa nimeupangilia kwenye muziki.

Ningekuwa na nafasi nzuri ningeweza kurekodi vizuri zaidi, na kutoa aina nyingi zaidi za muziki. Nakiri kuwa kaseti hii nimeirekodi kwa madhumuni ya kuiza kwa hadhira ya Watanzania ili niweze kurudisha pesa na kununua redio kaseti nyingine."
Taarifa nyingine zinazohusiana na hii:

No comments: