Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Monday, November 25, 2013

Hatua kumi za mauaji ya kimbari: 3 na 4

Nimetembelea Rwanda hivi karibuni na nikiwa huko nilipata fursa ya kutembelea mojawapo ya vituo vya kumbukumbu ya mauaji ya kimbari ya mwaka 1994.

Jambo moja la msingi ambalo Watanzania tunaweza kijufunza ni kuwa maafa yaliyotokea Rwanda yanaweza kutokea pia Tanzania. Kwa mujibu wa wachunguzi wa sababu zinozogeuza binadamu mmoja kuwa adui wa binadamu mwenzake na hata kufikia hatua ya kumaliza uhai wa mwenzake ziko duniani kote.

Sababu hizi zinaanza na mchakato wenye hatua nyingi ambao hufikia mauaji kama yale yaliyotokea Rwanda. Kinachozuwia maafa kama hayo kutokea ni hatua mahususi zinazopaswa kuchukulia na jamii za kukatisha uendelezwaji wa huo mchakato.

Kwa mujibu wa Dr. Gregory Stanton wa Genocide Watch, hatua za viashiria vya kuwepo kwa mchakato na za kuzuwia maafa kama ya Rwanda ziko kumi.

Hatua ya Tatu: Ubaguzi

Hatua hii inaanza kutenga makundi kwa mujibu wa uainishaji wa hatua ya kwanza. Mfano mashuhuri wa ubaguzi huu ni sera za kibaguzi za Afrika ya Kusini, apartheid. Kwenye hatua hii pia ndoa kati ya mtu wa kundi moja na jingine inapigwa marufuku na wale wanaoendeleza dhana hii. Yawezekana pia hata watu wa kundi linalobaguliwa kuanza kufukuzwa kwenye kazi, kama ambavyo ilifanyika dhidi ya Wayahudi wakati wa utawala wa Hitler huko Ujerumani.

Wakati mwingine zinatolewa hoja za kutenga nafasi za kazi kwa makundi mahususi ndani ya jamii. 

Mifano: Katika kukoleza ubaguzi zinaweza kuchukuliwa hatua za kubagua watu wa kundi moja kutonunua bidhaa za watu wa kundi jingine.

Hatua za kuepuka ubaguzi: Kuweka sheria zinazozuwia ubaguzi kwa misingi ya rangi, dini, kabila, utaifa, jinsia, tabaka, au chama.

Kuwezesha watu binafsi, na siyo waendesha mashtaka wa serikali pekee, kufungua mashitaka dhidi ya watu wanaotuhumiwa kufanya ubaguzi.

Hatua ya Nne: Udhalilishaji wa Kibinadamu

Kwenye hatua hii kundi moja linajipambanua kuwa ni bora kuliko lingine na kufanya kundi linalonyanyaswa kuonekana kama siyo binadamu kamili. Udhalilishaji wa kibinadamau unaondoa kusita kwa binadamu mmoja kuchukua hatua ya kumuua binadamu mwenzake.

Mifano: Nchini Rwanda kabla ya mauaji ya kimbari, Watutsi waliitwa mende na majina mengine ya kudhalilisha.

Hatua za kuepuka udhalilishaji: Kupinga kwa nguvu zote matumizi ya maneno ya kudhalilisha binadamu mwingine, pamoja na kuzuwia watu wa aina hii visa za kusafiria kwenda nchi nyingine na kueneza chuki.

Kuchukua hatua za kisheria dhidi ya watu au makundi ya watu yanayochochea madhara dhidi ya makundi mengine.

Serikali ichukue hatua za kufungia vituo vya redio na televisheni ambavyo vinachochea uhasama baina ya makundi mbali mbali. Tanzania tumeshuhudia vituo kadhaa kufungiwa kwa muda tu na kuruhusiwa kuendelea na matangazo.

Zitolewe fursa za kuleta maridhiano kwa njia zifuatazo:
  • kuanzisha vipindi kwenye vyombo vya habari vya kitaifa vyenye maudhui yanayokusudia kupunguza au kuondoa uhasama
  • kushirikisha viongozi wa kisiasa na dini kuongea na kukemea ubaguzi na kuhubiri kustamihiliana
  • kuhimiza madhehebu na dini mbalimbali kufanya kazi pamoja dhidi ya makundi ya chuki
  • kujenga makundi yanayofanya kazi pamoja kuepusha mauaji ya kimbari  
Muongozaji wageni katika mojawapo ya vituo vya kumbukumbu ya mauaji ya kimbari ya Rwanda ya mwaka 1994 akitoa maelezo kwa wageni.
Itaendelea na:
  • Hatua ya Tano: Uratibu
  • Hatua ya Sita: Kingamizi

No comments: