Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Friday, November 29, 2013

Maajabu ya mapishi [imefanyiwa masahihisho]

Hii ni tafsiri ya makala ya lugha ya Kiingereza niliyoandika na ikachapishwa kwenye gazeti la Daily News kwenye safu yangu iliyoitwa Letter from Butiama, makala nilizoandika kati ya mwaka 2005 na 2011. Makala hiyo ilichapishwa tarehe 26 Juni 2005.
*****************************************************
Inasemekana kuwa biashara zote zinazohusu nyama ndani ya mkoa wa Mara zinadhibitiwa na Wazanaki. Utawakuta kwenye kila ngazi ya biashara hiyo kama wamiliki, kama wafanyabiashara wa kununua na kuuza ng'ombe, na muhimu zaidi, kama wamiliki wa bucha. Aidha wamepata mafanikio wakubwa kwenye biashara hiyo kwenye jiji la Mwanza.

Somo kubwa linalojitokeza katika kuchunguza masuala yanayobainisha kampuni zenye mafanikio makubwa na zile zenye mafanikio duni ni ukweli kuwa mameneja wa kampuni zenye mafanikio wamejikita kwenye shughuli za bidhaa na huduma ambazo wanazielewa vyema. Inaelekea kuwa mmoja wa wafanyabiashara wa ng'ombe niliyeonana naye anaelewa vyema ukweli huu. Alinipa somo kuhusu hali mbali mbali za nyama kutoka sehemu tofauti za mwili wa ng'ombe na kuhitimisha kuwa nyama ya ng'ombe yenye ladha bora kuliko zote ni inayopatikana sehemu ya ndani ya paja la ng'ombe. Uelewa usiyo wa kawaida kama huu pengine ndiyo chanzo cha Wazanaki kutawala biashara ya ng'ombe na nyama ndani ya mkoa wa Mara. Napata picha ya matajiri wa Kizanaki wakimiliki biashara ya nyama ya bara la Afrika kama ambavyo Wajapani wamedhibiti biashara ya magari.

Pamoja na hii hamasa ya Wazanaki juu ya ng'ombe na nyama, ukweli unabaki kuwa hisia kali ya mtu mmoja inaweza kuwa mwiko kwa mtu mwingine. Migongano mikubwa ya kitamaduni inaweza kupatikana kwenye chaguzi ambazo watu toka tamaduni mbalimbali wanafanya kuhusu chakula wanachokula na kile wasichokula. Kwa baadhi ya dini kula nyama ni mwiko. Mboga na nafaka ndiyo hutumika kama vyakula vya msingi kwa jamii hizi.

Suala la chakula lilizua taharuki kwenye ziara mojawapo ya Rais Nyerere katika miaka ya sabini kwenye nchi mojawapo ya Ulaya. Kama ilivyo desturi kwenye misafara ya viongozi wa nchi, kiongozi mwenyeji wa nchi ile aliandaa dhifa ya taifa kwa mgeni wake, na baada ya juma moja Rais Nyerere akaandaa dhifa kwa mwenyeji wake. Wakati wa dhifa ya pili, mmoja wa Watanzania waliokuwa kwenye msafara ule alimdanganya Mtanzania mwenzake kuwa miongoni mwa vyakula vilivyoandaliwa kwenye dhifa ya kwanza ilikuwa ni pamoja na vyura na kuwa yule mwenzake alikula hao vyura bila kufahamu.

Aliyetoa taarifa hiyo alikusudia yawe mazungumzo kati yao tu, lakini aliyepewa taarifa ya kula miguu ya vyura alianza kujisikia vibaya hapo hapo na akaanza kutapika wakati dhifa ikiendelea.

Nilipokuwa mwanafunzi nchini Italia mimi na rafiki yangu George kutoka Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo tulialikwa chakula cha jioni na mwenyeji wetu Mtaliani. Baada ya kutuagizia chakula alisema kuwa alikuwa ametuchagulia chakula mahususi kwa ajili yetu ambacho huandaliwa marafiki wa karibu kabisa au wageni mashuhuri. Ukweli ni kuwa alikuwa ametuagizia miguu ya vyura. Ilikuwa mara yangu ya kwanza kula miguu ya vyura na nakumbuka ladha ilikuwa kama ya samaki. Mara tulipowekewa sahani zetu mezani na mhudumu, George alishituka na alitaka kuhama kabisa ile meza tuliyokaa. Mimi na mwenyeji wetu tulipoanza kushambulia ile miguu nakumbuka George alipata shida kubwa kubaki kwenye meza moja na sisi na kuangalia kitendo ambacho ni dhahiri kilimfadhaisha sana.

Mwenyeji wetu, ambaye aliwahi kutembelea nchi kadhaa za Afrika, alishangaa sana George. Alimuuliza anawezaje kuona kinyaa kula miguu ya vyura wakati yeye ameshuhudia Waafrika wakila wale wadudu ambao hutokeza baada ya mvua kunyesha. Alikuwa anazungumzia senene. George naye alishindwa kumuelewa Giuseppe. Mtu anawezaje kulinganisha kula senene na miguu ya vyura? Alisema Giuseppe alikuwa analinganisha vitu ambavyo havipaswi kulinganishwa kabisa.

Kuacha mimi, hamna kati yao ambaye alikuwa ameshakula miguu ya vyura pamoja na senene. Kimya kimya niliwashangaa hao wawili ambao walikuwa wanabishana ubishi ambao hawakuwa na mamlaka hata kidogo ya kuuendeleza. Jambo ambalo sikuweza kulibainisha wakati ule ni chakula kipi, kati ya chura na senene, kilikuwa na ladha nzuri zaidi.

Ukweli ni kuwa yawezekana kufikia usemi kuwa ladha ya chakula ni uamuzi ambao uko kichwani mwa mtu mmoja mmoja. Nimewahi kujitwika ujasiri usiyo na mfano na nikala chakula ambacho machoni kilikuwa kinatisha kuangalia lakini nikajikuta nimeweka mdomoni chakula chenye ladha nzuri kuliko maelezo. Tofauti na mwananchi mwenzangu ambaye alikuwa kwenye ziara ya Rais Nyerere, mimi nilifahamu chakula nilichokula siku ile kwenye ule mgahawa nchini Italia, kwa hiyo jambo la kushangaza ambalo naweza kulizungumzia ni ladha nzuri tu ya miguu ya vyura.

No comments: