Friday, July 28, 2017
Afrika tunaibiwa sana, tena sana
Friday, July 21, 2017
Mamlaka ya Mapato Tanzania yawageukia wauza spea
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Mamlaka inachunguza bidhaa hizo zilizopo madukani ili kupata uthibitisho wa wenye maduka kuwa wamepata hizo bidhaa kwa njia za halali.
Kwa muda mrefu inaaminika kuwa baadhi ya wenye maduka yanayouza spea za magari wananunua spea hizo kutoka kwa wezi wa magari, au wezi wanaoiba spea kutoka kwenye magari.
Hizi hatua zikiendelea kwa muda mrefu zinaweza kupunguza wizi wa spea za magari, na hata wizi wa magari.
Miaka mingi iliyopita nilipoishi Dar es Salaam niliwahi kuibiwa kioo cha mbele cha gari. Nilipotoa taarifa kituo cha polisi niliambiwa na polisi kuwa wana hakika kuwa kioo changu kitapatikana Gerezani, eneo la Dar es Salaam ambalo huuza bidhaa mbalimbali zilizotumika, nyingi ya hizo zikiwa bidhaa za wizi.
![]() |
Wezi watapungua |
Cha ajabu ni kuwa wale polisi walinishauri ninunue kioo changu. Bila hivyo walisema sitakipata. Huo ndiyo ulikuwa utaratibu wa kupata mali ya wizi wakati huo.
Bila shaka hizi jitihada mpya za Mamlaka ya Mapato zitapunguza kasi ya wizi, na zitaleta mabadiliko chanya kwa wamiliki wa magari.
Taarifa nyingine kama hii:
https://muhunda.blogspot.com/2016/07/mada-yangu-ya-leo-mwizi-ni-mwizi-tu.html
https://muhunda.blogspot.com/2011/07/maana-sahihi-ya-neno-fisadi.html
Friday, July 14, 2017
Simulizi za Jaffar Idi Amin
Anasema kuna siku alikuwa kwenye matembezi kwenye jiji la Kampala akakuta gari aina ya Volkswagen imeegeshwa na akasimama kwa muda mrefu akiiangalia kwa sababu aliitambua kuwa ilikuwa gari ya zamani ya baba yake.
Akiwa anaiangalia akatokea mtu na kumsalimia na kumuuliza sababu za kukaa muda pale akiangalia ile gari. Mazungumzo yakawa hivi:
"Mbona unaishangaa sana hiyo gari?"
"Ilikuwa gari ya baba yangu."
"Baba yako nani?"
"Idi Amin."
Anasema alivyotamka jina la baba yake yule aliyekuwa anamhoji akashangaa sana na kusema: "Baba yako ndiyo alimuondoa baba yangu nchini!"
Aliyekuwa anaongea naye alikuwa mmoja wa watoto wa Milton Obote, Eddy Engena-Maitum. Serikali ya Rais Obote ilipinduliwa na Idi Amin, wakati huo akiwa kamanda wa jeshi la Uganda, tarehe 25 Januari 1971 wakati Obote akiwa nchini Singapore kuhudhuria mkutano wa Jumuiya ya Madola.
Idi Amin alishika madaraka mpaka mwaka 1979 baada ya Rais Nyerere kutangaza vita dhidi ya Uganda kufuatia uvamizi wa eneo la Kagera na majeshi ya Idi Amin. Baada ya kukomboa eneo lililovamiwa vita iliendelea ndani ya ardhi ya Uganda na kuhitimishwa kwa kuangushwa kwa serikali ya Amin.
Jaffar akamwambia Eddy: "Mimi nitakutambulisha kwa mtu ambaye baba yake alimuondoa baba yangu hapa Uganda." Alimaanisha mimi.
![]() |
Mwalimu Nyerere akiwa na mwenyeji wake, Rais Milton Obote, wakati wa moja ya ziara zake nchini Uganda. Wa pili kutoka kulia ni Idi Amin, na kulia ni Philemon Mgaya, aliyekuwa mpambe wa Rais Nyerere. |
Idi Amin na familia yake walikimbilia nchini Libya, na baadaye kuhamia Saudia Arabia. Milton Obote na familia yake walihamia Tanzania na wakawa majirani zetu Msasani kwa muda mrefu.
Saturday, July 1, 2017
Watoto wa mjini nimewakubali
Nimejifunza siku chache zilizopita kuwa mtoto anayeishi mjini ni tofauti sana na yule anayeishi kijijini. Wa mjini wajanja.
Nilikuwa kwenye mitaa ya Kariakoo hivi karibuni nikaamkiwa na binti mdogo aliyevaa baibui niliyemkadiria kuwa na umri usiozidi miaka saba. Aliniomba msaada wa pesa kwa ajili ya mama mlemavu aliyekuwa kwenye kiti cha walemavu upande wa pili wa barabara.
Nilitoa shilingi 5,000 nikamkabidhi na kumuuliza kama nimsaidie kuvuka barabara ya Livingstone ambayo wakati huo ilikuwa na msululu wa magari. Alinihakikishia atamudu kuvuka mwenyewe. Nikaendelea na kununua miwani kwa machinga na yeye akaondoka.
Dakika 20 baadaye nikamkuta yule mama mlemavu kwenye mtaa wa jirani nikamuuliza kama alipokea zile pesa nilizotoa.
"Pesa gani?"
"Zile elfu tano nilizompa yule binti akuletee?
"Hata sijazipata. Ngoja tumsubiri."
Wakati huo binti alikuwa kwenye duka moja akiendelea kuomba msaada kwa watu mbalimbali.
Binti alivyoniona akatabasamu kwa aibu na kukabidhi zile pesa kwa yule mama, ambaye alinijulisha kuwa ni mjukuu wake.
Nilitafakari kuwa inawezekana wanapozunguka kuomba pesa mjukuu anabaki na pesa nyingi kuliko anazokabidhi kwa bibi yake.