Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Tuesday, November 6, 2012

Mlima Kilimanjaro unapendeza zaidi tokea Tanzania au Kenya?

Kuna mdau hapa anauliza swali: Mlima unaonekana vizuri tokea Tanzania au Kenya? Huyu mdau anahisi kuna hujuma inafanywa na jirani zetu kuvutia wageni wengi zaidi waende Kenya na ndiyo maana hoja hii inaibuliwa.

Hili swali halipaswi hata kuulizwa. Mlima Kilimanjaro unavyoonekana kutokea Kenya ni tofauti kidogo na unavyoonekana upande wa Tanzania. Kama kuna mtu kapendezewa na taswira ya mlima tokea Kenya huwezi kumlazimisha afurahie taswira ya mlima huo kutoka upande wa Tanzania.

Lakini huu utaratibu wa kulalamikia jirani zetu wa Kenya kunufaika na Mlima Kilimanjaro wakati sisi wenyewe tumekaa na kuongea tu pia hauna manufaa yoyote kwa maendeleo yetu.

Ninavyoamini mimi, mgeni yoyote aliyetoka nje ambaye amekuja kukwea mlima huu maarufu hajali kama uko Kenya, Tanzania, au kwenye sayari ya Zuhura. Mgeni anavutiwa na mlima wenyewe na siyo mipaka ya nchi.

Mimi nimeshakwea Mlima Kilimanjaro mara kadhaa na ukweli ni kuwa ni Watanzania wachache sana wanakwenda huko kulinganisha na wageni wa nje. Kwa kweli kule mlimani Mtanzania ndiyo mgeni na wageni ndiyo wenyeji kwa sababu idadi yao ni kubwa sana. Hivi karibuni nimekutana na Wakenya kibao kwenye njia ya Marangu wakielekea kileleni.

Mimi ningefurahi sana kuona hawa wenye uchungu na mlima huu kusemwa uko Kenya basi wawe wanajitokeza mara moja moja nao kukwea huu mlima. Hiyo itawawezesha kuzungumzia mlima wao kwa kujiamini badala ya kuuliza maswali tu na kulalamika.
Mlima Kilimanjaro unavyoonekana kutoka upande wa Tanzania.
Kitu ambacho watajifunza ni kuwa mandhari nzuri kuliko zote za mlima huu ziko huko huko mlimani. Lakini haya ni maoni yangu tu.

No comments: