Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Saturday, November 24, 2012

Jimmy ChangChuu, msanii toka Bagamoyo atembelea Butiama

Jimmy ChangChuu, ni msanii anayeishi na kufanya kazi Bagamoyo. Baadhi ya kazi anazofanya ni pamoja na kuchonga vinyago, kufinyanga, kuandaa michoro ya grafiti (michoro ya ukutani) na ni mwanamitindo.

Aidha hushiriki kwenye matangazo ya televisheni na anafahamisha kuwa ameshiriki kwenye kipindi televisheni cha cha Dume Challenge. Hivi karibuni alitembelea Butiama na yafuatayo ni maoni yake kuhusu Butiama.
***************************************************

"Naishi hizi sehemu mbili, Dar es Salaam na Bagamoyo, kwa sababu Bagamoyo ni sehemu yangu ambayo napata msukumo, ni sehemu iliyotulia. Mizunguko ya Dar es Salaam kidogo inakuwa inanishinda lakini ninapohitajika Dar es Salaam nakuwepo na familia.

Hii ni mara yangu ya kwanza kufika Butiama. Mara ya kwanza nilipokuja tu ile mandhari ilinifanya nijisikie kama niko na amani, nilipata amani kwenye moyo. Mazingira yametulia, yaani hakuna kitu ambacho kinaweza kikajiingiza wakati unafikiria kufanya kitu fulani au wakati uanataka kufanya kitu. Kwa hiyo ni sehemu ambayo imetulia ambayo inaweza kukupa msukumo.

Ni ngumu sana kupata msukumo kwenye sehemu ambapo kuna vitu vinapita ambavyo vinakuvuruga lakini hapa unaona hali asili ya mazingira, unaona ndege, yaani vitu ambavyo vinakufanya unaona kuwa kuna Muumba ambaye ametengeneza hivi vitu. Ni vitu ambavyo vinavutia kweli.

Kitu ambacho kinaweza kufanya niwaambie watu waje Butiama ni mazingira na hali ya utulivu halafu nikiangalia chimbuko la kabila la Wazanaki kuna vitu ambavyo nilikuwa nikiviangalia ambavyo vina nguvu kubwa ambavyo ukiviangalia kwa juu juu huwezi kuviona, lakini kuna vitu ambavyo vipo ambavyo vimemfanya Mwalimu Nyerere akawa ana nguvu kwenye maamuzi yake, vitu ambavyo vinaendana na tamaduni yetu ya Kitanzania na ambavyo Mwalimu aliviweka kwenye siasa yake na kwenye mila na hakutoka nje ya mila yake kusikiliza mila za kigeni. Alisimama yeye pale aliposimama kutoka kwenye chimbuko la tamaduni yake.

Kwa hiyo unakuta sasa hata katika utawala wake hakutoka nje sana kwa sababu hata nikiangalia nilivyokwenda makumbusho [Makumbusho ya Mwalimu J.K. Nyerere] kule kuna vitu ambavyo nimesoma na Nyerere mwenyewe alikuwa anakwambia elimu ya wakoloni ilikuwa inawaandaa wao kuwatumikia wakoloni siyo kuwaandaa kuweza kujiendeleza wao wenyewe.

Kitu kizuri kama watu wanataka kuwa kwenye siasa na kuwa viongozi wazuri wanapaswa kujifunza kutoka kwa Nyerere na aliyoyafanya. Tangu akiwa shuleni alianza kuwa kiongozi na alichaguliwa na watu. Watu waliona Mwalimu alikuwa na kitu fulani wakamchagua. Siyo kwamba yeye alipendekeza 'mimi nataka kuwa kwenye nafasi hii.' Watu walimuona kuwa ana kitu ambacho anaweza kuchangia kwa wengine na pia alikuwa na uwezo wa kushawishi wengine."

No comments: