Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Monday, November 12, 2012

Sijiuzulu ng'o! Hata mkija na winchi ya bandari

Jenerali David Petraeus wa Marekani amejiuzulu hivi karibuni kwa sababu ya mahusiano na mwanadada ambaye jina lake haliko kwenye cheti cha ndoa cha Jenerali huyo. Kwa Kiswahili anaitwa nyumba ndogo; kwa Kizanaki anajulikana kama kitungo.

Haya yangetokea Tanzania hamna mtu yoyote angeachia ngazi, na suala hili linaibua mitazamo tofauti kati ya utumishi wa umma hapa Tanzania na utumishi wa umma katika nchi nyingine.

Ukweli ni kuwa hata katika mijadala niliyoisikia kwenye vyombo vya habari vya nje kuna wale ambao wanaona kuwa Jenerali Petraeus hakustahili kung'atuka kwa sababu haya ni mambo ambayo yanatokea kwa watumishi wa ngazi za juu kwenye nchi mbalimbali duniani. Mtakumbuka kuwa Rais mstaafu Bill Clinton naye alikutwa na masuala yanayofanana na haya, na aliwekwa kiti moto kwa muda mrefu lakini hakujitoa kwenye uongozi. Tuhuma kubwa dhidi yake ilikuwa kusema uongo baada ya kula kiapo.

Kwa mantiki hiyo, inaelekea wadhifa wa Jenerali Petraeus kama Mkurugenzi wa shirika la ujasusi la Marekani, Central Intelligence Agency, ni nyeti zaidi katika nafasi ya uongozi wa nchini Marekani kuliko hata ule wa Rais wa Marekani, na inasemekana kuwa mkuu wa kazi wa Jenerali Petraeus ndiye aliyemshauri kuachia ngazi na yeye akafuata ushauri huo.

Nimetafakari suala hili iwapo aliyehusishwa na mahusiano haya angekuwa Mkuu wa Usalama wa nchi tofauti na Marekani na iwapo mkuu huyo angekuwa ni Mzanaki.

Soma mahojiano haya ya kubuni:

Mwandishi: Ndugu Madaraka, ninayo taarifa kuwa unahusishwa na tuhuma kuwa una uhusiano wa nje ya ndoa na [jina limehifadhiwa na gazeti] na...

Madaraka: Ndugu? Nani ndugu yako? Bwana mdogo, mimi ni mheshimiwa, tena mheshimiwa sana na ukitaka nijibu maswali yako nataka unipe heshima yangu. Na inaandikwa "m-h-e-" kabla ya jina...

Mwandishi: Samahani, mheshimiwa, nilikuwa nauliza....

Mhe. Madaraka: Swali nimelisikia. Bwana mdogo, nyie wasomi wa siku hizi mnafahamu sana mila na tamaduni za Ulaya na Marekani, lakini cha ajabu mnashindwa kudumisha na kuheshimu mila na tamaduni zenu wenyewe. Na ndiyo maana siku zote mtaendelea kutawaliwa kimawazo. Na ukishatawaliwa kimawazo utapangiwa mpaka maneno ya kuongea na mkeo nyumbani.

Sasa ngoja nikupe somo la bure kuhusu mila na tamaduni za kabila langu. Huyo mama ambaye wewe unashindwa kutaja jina lake, jina lake halisi ni [jina tumelihifadhi] na wala siyo siri kuwa ni mke wangu...

Mwandishi: Atakuwaje mke wako wakati tunafahamu mke wako ni......

Mhe. Madaraka: Mura! Enye ndakuburra ni mkane, bhono ni wazo? [Kijana! Mimi nakwambia ni mke wangu, sasa ni wako?] Bwana mdogo, ukitaka nikujibu usiniingilie ninapokujibu. Ukitaka kunipangia idadi ya kina mama zangu kwa sababu ulisomea Marekani, nashauri umuulize haya maswali Petraeus. Hapa siyo Marekani. Wao wana mila zao na mimi najaribu kukueleza mila zangu, kama utanisikiliza. Hutaki, kafanye kazi Marekani kwa sababu mimi hapa hatutaelewana.

Huyo nyie mnayemwita nyumba ndogo kijijini kwangu ana heshima yake, na wala hafichwi. Tunamuita kitungo, kama umeshawahi kusikia. Na kama ulifikiri utanitoa upepo kwa kunipa hofu kuwa umekalia siri ambayo utaifichua na kuniaibisha utakuwa unapoteza muda. Kwa taarifa yako ndugu zangu wote wanamfahamu, pamoja na mke wangu. Na hii ni pamoja na mamlaka iliyoniteua.

Haya, una lingine?

Mwandishi: Sawa mheshimiwa. Sasa pamoja na kwamba hizo ndiyo mila za Kizanaki, lakini wewe ni mtumishi wa Serikali na unashika wadhifa unaohusiana na usalama na maslahi ya Taifa. Utakuwa unafahamu kuwa nchi hii haiendeshwi kwa taratibu za kabila la Kizanaki. Inafuata kanuni, taratibu, na sheria. Huoni kama kwa kuwa na mahusiano haya yasiyo rasmi unaweza kuwa unahatarisha kuvujisha siri za nchi na kuwa unastahili kujiuzulu.

Mhe. Madaraka: Hivi wewe una akili timamu? Huyo aliyeniteuwa hana akili? Mimi mwenyewe sina akili? Kwamba nitaleweshwa na mahusiano yangu binafsi halafu nianze kuzianika siri za Serikali? Mbona hamkuwa na wasiwasi kuwa nitatoa siri kwa mke wangu, iweje leo nizitoe kwa huyu bi mdogo? Kama tatizo ni mahusiano na kina mama basi hizi kazi wawe wanafanya mapadri, watu ambao hawafungi ndoa. Lakini ni jambo ambalo pia mtalipinga, mtasema hatuwezi kuchanganya dini na Serikali maana hamksoi cha kusema nyie.

Unafahamu ile winchi ya badnari inayobeba kontena la futi 40? Nakwambia hata mkiileta ile kujaribu kuniondoa hapa, sitang'oka

No comments: