Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Tuesday, February 26, 2013

Lugha yetu Kiswahili

Hivi majuzi katika sherehe mojawapo niliandaa mtiririko wa nyimbo mbalimbali za muziki wa dansi za kusikiliza kwenye sherehe hiyo kwa kutumia kompyuta yangu ambayo inahifadhi mkusanyiko wa nyimbo nyingi ambazo nimezikusanya kwa miaka mingi. Baada ya hapo kompyuta inaunganishwa na vipaza sauti na nyimbo zilizochaguliwa zinaanza kusikika moja baada ya nyingine kwa muda mrefu tu.

Nyingi ya nyimbo hizo ni za wanamuziki wa zamani, wengi ambao hawako hai kwa sasa. Baadhi ya hizo Watanzania tunaziita "zilipendwa" au nyimbo za zamani ambazo vijana wengi wa siku hizi hawasikilizi.

Mmoja wa waliohudhuria sherehe hiyo alizipenda nyimbo zile sana na hakutulia sana kwenye kiti chake, akiinuka mara kwa mara kwenda kucheza muziki mmoja baada ya mwingine.

Nilivyotambua jinsi nilivyomsumbua huyo mtu nikajisifia kwa kumuuliza: Umenikubali? Na hapo nikazua mjadala na mtu mwingine aliyehudhuria sherehe hiyo akihoji iwapo ilikuwa sahihi kwangu kutumia neno hilo. Alisisitiza kuwa hawezi kunikubali mimi bali anaweza kukubali nyimbo ambazo nilizichagua kusikilizwa kwenye sherehe hiyo.

Mimi nilisisitiza kuwa "kunikubali" ulikuwa ni msemo tu lakini ukimaanisha alikubali uwezo wangu wa kuchagua nyimbo nzuri na siyo kunikubali mimi binafsi. Hoja yangu ilikuwa hata asingefahamu ni nani aliyechagua zile nyimbo angeweza kusema: "namkubali aliyepanga hizo nyimbo."

Ni kweli kuwa msemo wa "kumkubali" mtu umeibuka kwenye matumizi yasiyo rasmi ya lugha ya Kiswahili, hasa kwa vijana wa Tanzania, ukimaanisha kutoa sifa isiyo ya kawaida kwa mtu kwa uwezo wake wa kufanya jambo fulani.

Lakini siyo kweli pia kuwa tunaweza kuzungumzia kuwa wapiga kura "wamemkubali" mgombea mmoja na kumchagua kuwa kiongozi wao na kwa maana hiyo matumizi hayo yakaleta maana rasmi?

Wewe unasemaje?

No comments: