Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Friday, March 22, 2013

Tathmini ya muziki wa Tanzania mwaka 2012 (sehemu ya tatu kati ya nne)

Katika makala hii nitakayoitoa katika sehemu nne, mwanamuziki mashuhuri John Kitime, anafanya tathmini ya hali ya muziki Tanzania mwaka 2012.
******************************************
Tathmini ya muziki wa Tanzania mwaka 2012

makala ya John Kitime

(Sehemu ya tatu kati ya sehemu nne)


Tasnia ya muziki wa Tanzania katika tafiti mojawapo umeitwa ‘the radio-driven contemporary music industry’. Kwa maneno rahisi, tasnia ambayo imekuwa inaendeshwa na redio. Redio zimekuwa na uwezo wa kumpandisha na kumshusha mwanamuziki, kumtafutia soko, kumzibia soko na kadhalika. Hali hii ikisindikizwa na rushwa ambayo imetapakaa katika jamii yetu, unapata picha kuwa kungeweza kukawa na sura bora au tofauti ya muziki hali isingekuwa ilivyo.

Kuna ripoti za watu kutoa hongo nyimbo za wenzao zisipigwe, hongo ili nyimbo zipigwe, visasi vya kuzuia nyimbo zisipigwe na kadhalika. Na katika jamii ambayo imekuwa na kawaida ya kutegemea vyombo vya habari kujua muziki gani mpya na mzuri, uwanja huu si uwanja ulio tambarare hata kidogo. Bahati mbaya inaonekana wenye vyombo hivi wako mbali na ukweli unaoendelea katika vyombo vyao au kwa kutokujua au kupuuza.

Janga hili limevikumba hata vyombo ambavyo vinaendeshwa na taasisi za dini. Wanamuziki wa muziki wa injili nao pia wanalia kudaiwa rushwa na watangazaji wa radio za injili!.  Nakumbuka siku niliyopata nafasi kuongea na kiongozi mmoja wa dini ambaye kanisa lake linaendesha kituo cha redio, nilipata mshangao baada ya mkuu huyo, kuanza kutetea watangazaji wake badala ya kuamua kufanya uchunguzi wa tuhuma.

Umefika muda wa redio kuanza kujigawa kimuziki. Ni kichekesho mji kuwa na vituo vya redio 30 halafu vyote vinapiga aina hiyohiyo ya muziki, wakati kuna aina mbalimbali za watu. Ajabu ni kuwa wenye redio wanajua kuwa katika nchi nyingine unaweza kukuta redio iliyoamua kupiga aina fulani tu ya muziki, Jazz Radio, Country music Radio, Classic Music Radio, lakini hilo limekuwa gumu kwao kutekeleza hapa. Kuwe na utofauti, wasikilizaji tuko wa aina tofauti.

Vyombo vya habari vijitahidi kupata wataalamu husika wa aina tofauti za muziki, muziki unaviingizia vyombo hivyo mabilioni ya fedha, vyombo vya habari viupe heshima yake. Bila muziki hakuna redio.

Magazeti yamekuwa mstari wa mbele katika kutangaza aina mbalimbali za wasanii na sanaa. Pamoja na hongera kwa kazi nzuri lakini bado kuna nafasi kubwa ipo tupu, hakuna wataalamu wa uandishi wa habari za muziki. Hivyo habari nyingi za muziki zinaandikwa na waandishi kama wapenzi wa muziki na si wataalam wa uandishi wa muziki, jambo ambalo liko tofauti na uandishi wa michezo, kwa mfano soka. Unaweza ukasoma habari ya soka ambapo mwandish atakueleza nafasi za wachezaji, kama ni faulo, ni nini kilisababisha, na kama ni goli lilikuwa ni la kichwa au kona au penalty. Hili haliko katika muziki. Utaambiwa tu bendi ilipagawisha, au msanii fulani ateka nyoyo za wapenzi, na maelezo ya juu juu kama yale.

Kunahitajika kuanzishwa mafunzo ya elimu ya uandishi wa kazi za sanaa. Hili litapunguza hata vurugu kama zilizotawala mwaka huu za wapiga picha kufikia hata kulala chini ili tu wapate picha ya nguo za ndani za msanii na hayo ndio kuwa maelezo makuu ya onyesho zima la muziki.

(itaendelea)

Taarifa zinazohusiana na hii:

No comments: