Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Wednesday, April 24, 2013

Mada yangu ya leo: Ukiritimba wa Tanzania ni kikwazo kwa maendeleo

Mojawapo wa vikwazo vikubwa kwa utendaji kazi Tanzania ni ukiritimba. Ni janga la Taifa, nadiriki kusema. Nimeshuhudia katika siku chache zilizopita tatizo hili kwenye taasisi kadhaa, ikiwa ni pamoja na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).

Nilimsindikiza mwekezaji mmoja kwenye ofisi ya kanda ya Kituo cha Uwekezaji Tanzania kuwasilisha maombi ya kusamehewa malipo ya kodi ya nyongeza ya thamani kwa mujibu wa sheria ya uwekezaji. Taratibu zinataka muombaji afuate hatua hizi:

1.       Achukue ankara kwa muuzaji wa bidhaa ambazo zinaombewa msamaha
2.       Ajaze fomu maalumu ya maombi ya kusamehewa kodi ya nyongeza ya thamani
3.       Awasilishe katika ofisi ya Mamlaya ya Mapato Tanzania fomu (kwenye mkoa ambako mradi unaendelezwa) ili idhini ya kusamehewa kodi itolewe; na
4.       Arudi kwa muuzaji na kulipia bidhaa bila kodi na kuchukuwa hivyo vifaa

Tatizo liko katika ngazi nyingi. Kwanza, taratibu zote za kuomba misamaha ya kodi au zinafanyika Dar es Salaam au kwenye makao makuu ya Kituo cha Uwekezaji na Mamlaka ya Mapato Tanzania, au kwenye ofisi za kanda za kituo cha uwekezaji. Ofisi hizi za kanda siyo nyingi kwa hiyo, kwa mwekezaji ambaye hayuko Dar es salaam au jirani na ofisi za kanda,  inamlazimu aingie gharama kubwa ya kusafiri mara kwa mara kati ya eneo la mradi kwenda kwenye maeneo hayo ambapo maamuzi ya kusamehewa kodi yanachukuliwa.

Si hivyo tu, lakini kwa mwekezaji ambaye hayuko Dar es salaam au jirani na mji mkubwa hulazimika mara kwa mara kupata mahitaji ya vifaa vya ujenzi kutoka sehemu mbali mbali za Tanzania. Mathalani, kwa mwekezaji aliyeko Butiama, anahitaji kusafiri mara kwa mara kwenda nje ya mkoa wa Mara kununua vifaa mbalimbali, ikiwa ni pamoja na Mwanza na Dar es Salaam.

Tatizo la ukiritimba, ambalo wapanga taratibu wa Dar es Salaam (na watunga sheria wa Dodoma) huwa hawalioni, ni hili na linaonekana vizuri kwa mfano halisi wa namna ambavyo mwekezaji wa Butiama anapaswa kupata msamaha wake wa VAT:

1.       Anasafiri kwenda Mwanza au Dar es Salaam kupata ankara ya vifaa ambavyo anataka kununua. Nasisitiza kuwa analazimika kusafiri kwa kuwa tunafahamu kuwa, tofauti na nchi zilizoendelea, kwetu ni muhimu kuona vifaa kabla ya kuvinunua.
2.       Anajaza fomu ya kuomba msamaha wa kodi na kuiwasilisha kwenye ofisi ya Mamlaka ya Mapato Tanzania ya Mkoa wa Mara, na kupewa idhini. Ofisi ya mkoa pia ina jukumu la kukagua mradi na kuhakikisha kuwa unaendelezwa.
3.       Anarudi Dar es Salaam au Mwanza kulipia vifaa bila malipo ya kodi, na kuchukuwa vifaa.

Jambo ambalo nimejifunza ni kuwa hali ya kutoaminiana kati ya ofisi za Mamlaka ya Mapato Tanzania katika ngazi mbalimbali (makao makuu na mikoani) ndiyo inayosababisha hizi taratibu za ajabu za kufanya muombaji alazimike kwenda Dar es Salaam au Mwanza mara mbili ili kukamlisha mzunguko wa manunuzi na kupata msamaha wa kodi.

Nilimuuliza Meneja wa Mkoa wa TRA Mwanza: “Hivi usingeweza kumpigia simu meneja mwenzako Musoma na kupata uthibitisho kuwa mradi huu ni halali na unaendelezwa Butiama?”

Alinijubu kuwa, kwanza, sheria na kanuni haziruhusu. Mwekezaji anatakiwa apate barua ya Mkuu wa Wilaya alipo (kutihibitisha uwepo wa mradi katika wilaya yake) ambayo inapaswa kuwasilishwa kwenye ofisi za Mamlaka ya Mapato ya Mkoa, na jalada la mwekezaji kufunguliwa likiwa na orodha ya vifaa vilivyoruhusiwa msamaha wa kodi. Halafu, kila mwekezaji anapofanya manunuzi ofisi ya TRA Mkoa itapunguza vile vilivyonunuliwa. Aidha, ofisi hiyo tu ndiyo yenye mamlaka ya kufanya ukaguzi wa mradi kuhakiki vifaa visitumike tofauti na ilivyoombwa na mwekezaji.

Meneja huyo wa Mwanza alinitolea mifano kadhaa ya wawekezaji wasiyo waaminifu ambao walipewa misamaha ya kodi lakini hawakuwa na miradi yoyote ya uwekezaji waliyoendeleza, na badala yake wakatumia vifaa vilivyosamehewa kodi kwa matumizi mengine. Alimalizia kwa kusema: “Unajua watu wamekuwa wadanganyigu sana siku hizi kwa hiyo lazima kuchukuwa tahadhari.”

Nilimuuliza iwapo taratibu zote zimekamilishwa, kwanini ofisi yoyote ya TRA katika mkoa wowote wa Tanzania isiweze kuwasiliana na ofisi ya TRA iliyopo kwenye mkoa wenye mradi ili kutihibitisha  uwepo wa mradi ili kumpunguzia mwekezaji ambaye ni mwaminifu safari ya nenda rudi ili kukamilisha mzunguko. Bado hakuona kuwa ni tatizo ambalo mamlaka inapaswa kusumbuliwa nalo na kwake yeye tatizo la msingi lilikuwa kudhibiti wasiyo waaminifu bila kujali athari kwa wale waliyo waaminifu.

Kwa maoni yangu tatizo la kudhibiti uhalifu linagubikwa pia na uvivu wa kufikiri mbinu za kudhibiti wahalifu. Kwa hiyo linapoonekana tatizo, uamuzi unakuwa kudhibiti utendaji badala ya kurahisisha utendaji. Sasa hivi Tanzania ina Mkongo wa Taifa ambao ungeweza kutumika vizuri kufanya mawasiliano kati ya ofisi za TRA za mikoa ili taarifa muhimu za wawekezaji ziweze kupatikana kwenye ofisi yoyote ya TRA nchini.

Si hivyo tu, kompyuta zimejaa kwenye maofisi ya Tanzania. Zinatumia kwa ajili ya nini? Nimeshuhudia kwenye maofisi kadhaa hutumika kisikilizia nyimbo za kwenye CD na kuangalia televisheni. Nina hakika pia hutumika kwa ajili ya Facebook, Twitter, na shughuli nyingine za mtandao ambazo kamwe haziwezi kumpunguzi bugdha mwekezaji anayejaribu kuomba msamaha wa kodi ya nyongeza ya thamani.

Nilimwambia yule meneja wa Mwanza kuwa iwapo polisi wa Tanzania wangekuwa wanafanya kazi kama TRA, basi hali ya uhalifu ingekuwa mbaya kuliko ambavyo ilivyo sasa. Kwa sababu Mtanzania angetenda uhalifu Butiama akahamia Kibondo akiwa na uhakika kuwa polisi wa Kigoma wakimwona watasema kuwa siyo kazi yao kumkamata kwa sababu kosa limefanyika kwenye Mkoa wa Mara. Kwangu mimi  TRA ni chombo cha kitaifa na huduma yao haiwezi kuishia ndani ya mipaka ya mikoa. Ama sivyo tuambiwe sasa kuwa Chama cha Mapinduzi kinaanza kutekeleza sera za CHADEMA kwa kupitia njia za panya.

Nilijaribu kueleza kwa meneja wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania kwenye ofisi yao ya kanda iliyopo Mwanza adha hii ya ukiritimba, na hasa kufanyika Dar es Salaam kwa maamuzi ya masuala mbali mbali. Kwa maoni yake (na baadhi ya sheria zinaelekeza hivyo) kuna maamuzi mengi ambayo yanaweza kuidhinishwa na maafisa mahususi tu ambao wako Dar es Salaam.

Nilimkumbusha kuwa kuna maelfu wa maafisa hapa nchini wanaotekeleza majukumu kwa niaba ya rais kwa hiyo labda umefika wakati kupitia upya sheria na kuangalia uwezekano wa kukaimishwa kwa baadhi ya maamuzi yanayokwamisha utendaji.

Kuacha Mamlaka ya Mapato, ipo mifano mingine mingi kwenye taasisi nyingine ambayo nayo inaathiri utendaji katika sehemu mbalimbali za nchi. Mfano mmojawapo ni huduma za kampuni za simu. Ni mara kadhaa nimepiga simu kwenye kitengo cha huduma kwa wateja katika mojawapo ya kampuni za simu kulalamikia huduma fulani nikaambiwa: “njoo ofisini.” Hawa waliyoniambia “njoo ofisini” hawakuwa na ofisi Musoma, kwa hiyo “njoo ofisi” kwangu inamaanisha “njoo/nenda Mwanza”, safari ya kilomita 190.

Tatizo la vitengo vya huduma kwa wateja kwenye kampuni hizi za simu ni kuwa wanapaswa kuwa na watu wenye uwezo wa kutoa maelekezo kutatua tatizo kwa njia ya simu, lakini labda kwa kutokuwa na watu ambao wamepewa mafunzo ya kutosha, wanaposhindwa kumaliza tatizo lako wanasema: “njoo ofisini.”

Tanzania ina watu wengi kuliko wanaoishi Dar es Salaam. Hili likizingatiwa, matatizo mengi ya ukiritimba yatapungua.

Taarifa nyingine zinazofanana na hii:

No comments: