Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Tuesday, December 17, 2013

Mandela! Mandela! Mandela! (sehemu ya pili ya awamu tatu)

Kwenye makala hii ambayo imegawanywa kwenye awamu tatu, Notburga Maskini anaandika kuhusu Mzee Nelson Mandela, aliyefariki tarehe 5 Desemba na kuzikwa leo, tarehe 15 Desemba 2013 kwenye kijiji cha Qunnu nchini Afrika ya Kusini.

Mandela! Mandela! Mandela! (Sehemu ya Pili)
Na Notburga Maskini*

Migongano ya Kitabaka
Matabaka ya mabwana na watwana yalijitokeza kutokana na unyonyaji, udhalilishaji, na ubaguzi uliofanywa na makundi dhalimu ambayo yalijitokeza na kuonekana katika mifumo ya kijamii kwa maana ya Ukomunisti na Ubepari ambapo mabwana au wenye nguvu, waliwadhalilisha wanyonge; ilitengeneza tabaka la watu wachache matajiri wa kupindukia ambao wameshikilia na kuwekeza asilimia 80 ya utajiri wa dunia katika mtaa wa tano (the 5th Avenue New York).  

Tabaka la pili ni la umma wa wakulima na wafanyakazi maskini na wanyonge katika nchi zetu na duniani ambao bidii na jasho lao haviwawezeshi kujikwamua kutokana na mirija ya dhuluma iliyopangwa na tabaka hili  la watu wachache lakini lenye nguvu kubwa kiuchumi na kiutawala. Tabaka la tatu ni tabaka la maskini wa kutupwa miongoni mwao wakiwemo wazee, wastaafu, vijana wasio na ardhi wala ajira, wanawake na watoto.

Hali hii  ya kuhuzunisha na tishio kwa amani ya nchi zetu na dunia ilionekana mapema machoni na kwenye mioyo ya viongozi hawa mashujaa Nelson Rolihlahla Mandela na Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. Waliichukia na kufanya bidii kubwa kuchukua hatua sawia kupambana ili kuona mfumo wa haki usawa na heshima kwa binadamu unasimikwa dhidi ya mifumo ya unyonyaji, ubaguzi na udhalilishaji.

Kazi iliyobaki ya kugawa rasilimali hizi za dunia ziweze kuwafikia watu wengi na kuondoa umaskini duniani ndio njia pekee ya kumuenzi Mzee Mandela bila unafiki. Tunahitaji mashujaa kama Mzee Nelson Mandela na Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ambao wataweka ushawishi na kupambana hasa wakati huu zinapoonekana dalili kuwa jambo hili linawezekana. Kifo cha shujaa huyu  tumeshuhudia viapo na dhamira zikiwekwa kanisani na hadharani kuashiria kuwa tayari hata kufa ili kutetea ustawi wa binadamu na amani duniani. 


State Funeral of former President Nelson Mandela, 15 Dec 2013
Picha: Maafisa wa jeshi la Afrika ya Kusini wakiwa wamebeba jeneza lenye mwili wa Marehemu Nelson Mandela kwenye mazishi ya taifa yaliyofanyika tarehe 15 Desemba 2013 kwenye kijiji cha Qunu, jimbo la Eastern Cape.

Kusaliti na kuvunja tabaka
Mzee Nelson Mandela na Mwalimu Julius Nyerere ni miongoni mwa watu waliojaaliwa na Mwenyezi Mungu kuumwa na kuchukizwa na hali mbaya ya binadamu wote. Waliona ubaya na adha inayotokana na binadamu kumdhalilisha binadamu mwingine na hatari yake kwa amani ya dunia hivyo hawakuivumilia hata kwa sekunde chache. Walipinga hali hii pamoja na uwezo waliokuwa nao kutokana elimu na nafasi zao za kuzaliwa wakiwa watoto wa machifu, ambapo wangaliweza kuungana na wadhalilishaji na kuwa wanufaikaji wa mifumo dhalimu iliyojaa uroho, uchoyo, dharau, na tamaa.

Mzee Mandela na Mwalimu Nyerere walizungumza kwa sauti kubwa na hivyo kuweka ushawishi mkubwa ndani ya jamii na nchi zao na kuanzisha vuguvugu la mapambano yaliyokusudia kuleta heshima kwa binadamu. Ni dhahiri kuwa walitumia maisha yao hapa duniani kujitoa mhanga kwa ujasiri wa kupindukia hata kuuwa matabaka yao (class suicide) kupigania usawa haki na heshima kwa binadamu. Ndiyo maana kuondoka kwao duniani Mzee Nelson Mandela aliyetanguliwa na rafiki yake mkubwa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere muongo mmoja na nusu uliopita kunaleta mshtuko na wasiwasi mkubwa kwa amani ya dunia, usawa, ubinadamu, demokrasia, na utawala bora.  Hii inatokana na ukweli kwamba binadamu wa aina hii hutokea kwa nadra sana.

Itaendelea na: Heshima katika historia ya nchi na dunia


*Notburga A Maskini ni Kaimu Rais wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA).

No comments: