Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Sunday, December 15, 2013

Mandela! Mandela! Mandela! (sehemu ya kwanza ya awamu tatu)

Kwenye makala hii ambayo imegawanywa kwenye awamu tatu, Notburga Maskini anaandika kuhusu Mzee Nelson Mandela, aliyefariki tarehe 5 Desemba na kuzikwa leo, tarehe 15 Desemba 2013 kwenye kijiji cha Qunnu nchini Afrika ya Kusini.

Mandela! Mandela! Mandela! (Sehemu ya Kwanza)

Na Notburga Maskini*

Hiki kimekuwa ni kilio cha dunia nzima kumwomboleza shujaa mpigania uhuru, amani, haki, utu na utawala bora duniani, mwana wa bara la Afrika mwenye asili ya Afrika ya Kusini Nelson Rolihlahla Mandela mwanaharakati, kiongozi wa chama cha ANC na Rais Mstaafu wa Afrika ya Kusini; aliyeaga dunia tarehe 5 Desemba 2013.  Mimi binafsi na kwa niaba ya wafanyakazi wa Tanzania naungana na Watanzania wenzangu, wafanyakazi wa Afrika ya Kusini na Dunia kuomboleza msiba huu mkubwa ambao ni pigo kubwa kwa tabaka la wafanyakazi duniani na vilevile ni pigo dhidi ya utawala bora, haki, amani na utu. 

South Africans mourn the
death of the late former President Nelson Mandela, 8 Dec 2013
Picha: Wanachama wa Umkhonto We Sizwe, lililokuwa jeshi la chama cha African National Congress lilioendesha mapambano ya kivita dhidi ya utawala wa kibaguzi wa Afrika ya Kusini, wakiwasili kwenye makazi ya jijini Johannesburg ya marehemu Nelson Mandela tarehe 8 Desemba 2013. (Picha ya GCIS).

Niandikapo makala hii nakumbuka mwaka 2003 nilipokuwa jijini Johannesburg kuhudhuria mkutano wa dunia kuhusu uwekezaji wa mitaji Afrika, Kusini mwa Sahara kwenye ukumbi mmojawapo katika jengo maarufu la Sandton. Wakati wa kutoka ukumbini tulikutana nae ana kwa ana mlangoni akiwa na watu wengine, nafikiri kiongozi huyu alitokea kwenye ukumbi mwingine wa mkutano katika jengo hilo. Binafsi nilifurahi sana kumuona Mzee Mandela aliyekuwa katika hali ya kawaida kabisa. Hata hivyo mimi na hata wenzangu hatukuweza kufanya chochote angalau kuweza kumsalimia kutokana na kutofahamu taratibu na mipaka ya kiitifaki.  Alikuwa ni kivutio kikubwa kwetu sote tuliokuwepo siku hiyo.

Afrika Kusini na Tanzania
Ndugu zetu wa Afrika ya Kusini kama ilivyokuwa kwetu Watanzania tarehe 14 Oktoba 1999 alipotuaga Mwasisi wa Taifa hili, mwanamapinduzi aliyeheshimika duniani, na kipenzi cha Watanzania, Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, nao wanapitia hali ngumu iliyojaa majonzi, vilio, na mashaka lakini pia wakimshukuru Mungu kwa zawadi kubwa aliyoupatia umma wa Afrika Kusini, Bara la Afrika na Dunia.

Katika kitabu chake cha dondoo Nelson Mandela By Himself, 2013 Mzee Mandela anatufariji kwa maneno yake mwenyewe kuwa: 

“kifo hakikwepeki. Wakati binadamu ameshatimiza yale aliyofikiri kuwa ni wajibu wake kwa watu wake na nchi yake, anaweza kupumzika kwa amani.  Naamini kuwa nimefanya bidii kutimiza wajibu huo na ndio maana nitalala katika umilele”  

Ni dhahiri kuwa Mzee Mandela ameondoka akiwa anaridhishwa na bidii kubwa aliyoweka katika kazi kubwa aliyoifanya ya kuondoa ubaguzi wa rangi na udhalilishwaji wa mtu mweusi katika nchi yake ya Afrika ya Kusini. Pengine Watanzania na waombolezaji tuliobaki yafaa kutafakari sasa kuhusu wajibu wetu kwa watu wetu na nchi zetu na iwapo tutaweza kuwa jasiri na kusema maneno hayo siku yetu itakapofika. 

Imani na mapenzi ya Umma dhidi ya chuki za maadui
Mzee Nelson Mandela kama alivyokuwa Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere wameteka mioyo ya walimwengu na wananchi wao kwa imani yao katika utu badala ya vitu, na kusimamia kwa vitendo bila ya kutetereka. Wanamapinduzi hawa wa Afrika waliweka mbele maslahi ya taifa na utu wa watu wao.  Walijitoa muhanga maisha yao yote kwa ajili ya nchi zao na watu wao jambo ambalo ni nadra kwa viongozi wengi tuliowashuhudia katika karne ya ishirini.

Wakati Mwalimu Julius Nyerere akiongoza mapambano ya ukombozi wa Bara la Afrika na dhidi ya udhalimu dhidi ya ubinadamu ikiwemo Afrika Kusini yenyewe, alitengeneza maadui waliotokana na kundi la wakandamizaji waliojijengea uhalali na kuamini kuwa wao ni bora kuliko binadamu wengine. Hata hivyo maadui hao kama tunavyoshuhudia leo wamejirudi na kujifunza thamani ya utu na utaifa katika kutumikia umma. 

Isingewezekana wakati ule wa mapambano ya ukombozi kuwa Afrika ya Kusini ingebadilika na kuwa kama ilivyo sasa. Kinachodhihirika hapa ni nguvu ya upendo, msamaha, na uzalendo kwa nchi na watu wake vinavyoweza kuleta mabadiliko chanya.  Hili ni somo kubwa kwa Afrika na Dunia.

Itaendelea na: Migongano ya Kitabaka

*Notburga A Maskini ni Kaimu Rais wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA).


No comments: