Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Monday, July 4, 2011

Lugha Yetu Kiswahili: Kwa matumizi haya, Kiswahili kitaangamia


Suala moja ambalo linajidhihirisha mara kwa mara katika miaka ya hivi karibuni ni matumizi mabaya ya lugha ambayo yamejikita katika mazungumzo na hata maandishi ya kila siku ya lugha ya Kiswahili.

Mimi naamini mtu yoyote anayefahamu lugha yake, au anayetaka kulinda matumizi sahihi ya lugha yake hawezi kupuuza matumizi sahihi ya lugha, lakini kwa mwenendo wa matumizi ya lugha ya Kiswahili ulivyo siku hizi, hasa kwa vijana, Kiswahili kina wakati mgumu na uwepo wake uko hatarini.

Mimi nakubaliana na wanaosema kuwa kuna ulazima wa lugha kubadilika na msamiati kuongezeka kila muda unavyozidi kupita. Lakini siyo kwa mtindo huu wa sasa ambapo maneno sahihi yanageuzwa kuwa maneno yasiyo sahihi, na misemo isiyofaa kutumika hata kwenye vyombo vya habari. Nitoe mifano michache:

Vijimambo: Hili neno nimewahi kusikia watu wazima wakilizungumza. Ni afadhali ingekuwa vijana peke yao kwa kuwa wao wanajulikana kwa kutunga maneno mapya. Kwa uelewa wangu mimi lina maana ya mambo kadha wa kadha ambayo msemaji hawezi kuyaweka bayana na hutumia neno hilo kufunika hayo asiyoweza au asiyotaka kuyasema kwa wakati ule. Ushauri wangu ni kuwa kama huwezi kulisema inawezekana halistahili kusemwa.

Ndivyo sivyo: Huu msemo nimeusikia ukitumika na baadhi ya wanahabari na nashindwa kabisa kuelewa mwanahabari anawezaje kuacha kutumia lugha ambayo inaweka wazi maana anayokusudia badala ya msemo unaomlazimu msikilizaji kukisia maana inayokusudiwa.

Kudadeki: Kwa kadiri ninavyofahamu mimi chimbuko la hili neno ni tusi la nguoni na limeingia katika matumizi ili kuepuka mtumiaji kusema lile tusi lenyewe. Cha ajabu ni kuwa nimeshasikia tangazo kwenye redio la kampuni moja ya simu wakitumia neno hilo. Kama linatumika kwenye tangazo muda si mrefu litakuwa kwenye matumizi ya kawaida ya lugha. Ukiuliza maana yake sidhani kama wengi wa wanalolitumia wanafahamu kwa uhakika, lakini mimi naamini kuwa hili neno linatokana na tusi zito tu.

Kwa mtindo huu, Kiswahili kitapona?

Monday, June 20, 2011

Mlima Meru, wa pili kwa urefu Tanzania, wa 72 ulimwenguni

Mlima Meru ni Mlima wa pili kwa urefu Tanzania baada ya Mlima Kilimajaro. Una urefu wa mita 4,565 juu ya usawa wa bahari na unaorodheshwa kushika nafasi ya 72 kwa milima mirefu kuliko yote duniani. Mlima Meru uko mkoa wa Arusha, ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Arusha.
Mlima Meru ukionekana kutoka Arusha.
Watu wengi wanaoparamia milima kama mimi huanza kupanda milima rahisi kwanza kabla ya kwenda kwenye ile yenye kutoa changamoto kubwa zaidi. Wengi hupanda Mlima Meru kabla ya Kilimanjaro, ingawa mimi nimeanza kupanda Mlima Kilimanjaro nikikusudia baadaye kuukabili Mlima Meru. Waliopanda milima yote miwili wanasema kuwa, pamoja na kuwa Meru siyo mrefu kuliko Kilimanjaro (Kilimanjaro una urefu wa mita 5,895 juu ya usawa wa bahari), untoa changamoto kali kwa sababu kupanda kwake ni mpando wa siku 2 mfululizo wakati Mlima Kilimanjaro unahusisha njia zinazovuka mabonde kadhaa na hiyo ina maana kuwa wanaoelekea kileleni hujikuta wakipanda na kushuka na hata wakati mwingine kupita sehemu zenye tambarare.

Tafiti zinathibitisha kuwa miaka bilioni kadhaa iliyopita Mlima Meru ulilipuka kutokana na msukumo wa gesi za volkano na kusababisha sehemu yake ya pembeni kumeguka na kutapakaa kwenye eneo la umbali unaofikia upande wa magharibi ya Mlima Kilimanjaro. Hizo tafiti zimethibitisha kuwepo tabaka ya udongo wa Mlima Meru juu ya sehemu hiyo ya Mlima Kilimanjaro.

Picha hii ya chini ambayo imepigwa na vyombo vinavyoruka juu vya shirika la Marekani NASA inaonyesha vizuri sehemu ya Mlima Meru iliyomeguka kutokana na mlipuko wa volkano. Tofauti ya rangi iliyopo kwenye picha inaakisi tofauti ya umbali kutoka usawa wa bahari wa eneo hilo la Mlima Meru.
Hii picha ya Mlima Meru inatumika kwa hisani ya NASA/JPL-Caltech. [Photo: Courtesy NASA/JPL-Caltech]

Saturday, June 18, 2011

Tarehe za kupanda Mlima Kilimanjaro mwaka huu ni Septemba 20 hadi 27

Kila mwaka tangu mwaka 2008 nimekuwa napanda Mlima Kilimanjaro kuchangisha pesa za hisani. Mwaka 2008 nilipanda Mlima huo na raia wa Vietnam, Le Hu Dyuong. Mwaka 2009 nilipanda Kilimanjaro na Notburga Maskini, ambaye tulisoma pamoja Shinyanga Commercial Institute (Shycom) miaka iliyopita. Yeye alikuwa pamoja na mtangazaji maarufu wa Clouds FM, Gerald Hando.
Le akiwa kwenye bwawa lenye mamba, baada ya msafara wa kupanda Mlima Kilmanjaro mwaka 2008.
Mwaka jana nilipanda mlima na Jaffar Amin, mtoto wa kiongozi wa zamani wa Uganda, Idi Amin.
Jaffar Amin, akiwa amekaa mbele ya mahema yetu kwenye kambi ya Karanga iliyopo mita 3,963 juu ya usawa wa bahari wakati wa msafar wa mwaka jana wa kupanda Mlima Kilimanjaro.
Mwaka huu natarajia kupanda Mlima Kilimanjaro kuanzia tarehe 20 hadi 27 Septemba. Natarajia kupanda mlima pamoja na wafuatao. Ambao wamesema watajiunga na mimi mwaka huu ni pamoja na mwanablogu mwashuhuri Muhidini Issa Michuzi, mdau wa Utalii Aysha Boma, raia wa Uswisi Andrea Wobmann, mtengeneza filamu wa Marekani Jim Becket (amewahi kuongoza picha ya Mark Dacascos) pamoja na mpigapicha wake, na raia wa Uganda Barbara Allimadi. Kuna wengine ambao bado hawajathibitisha.

Thursday, June 16, 2011

Tabia ya Tumbili

Kumradhi endapo nitakuwa nimemuudhi yoyote kwa kutumia hii picha hapa chini ya huyu jamaa akiwa kwenye mkao wa kula, pamoja na kwamba nilishwahi kuitumia hapa.
Miaka kadhaa iliyopita nilihudhuria mafunzo ya muda mfupi katika chuo kilichopo Tengeru karibu na Arusha, sehemu ambayo ilikuwa inatembelewa na tumbili mara kwa mara.

Jioni moja baada ya kutoka darasani nilishuhudia baadhi ya wanafunzi wenzangu, wakiwa wamevutiwa na hawa wanyama, na walijaribu kuwasogelea pole pole lakini kila walipowakaribia wale tumbili walisogea mbali.

Cha ajabu ni kuwa mmoja wa wakufunzi wetu alipopita kwenye njia ya mguu karibu kabisa na sehemu ambapo tumbili walikuwa wamekaa, wale tumbili hawakuondoka na walibaki pale pale. Raia wa Zambia ambaye alikuwa mmoja wa wale wanafunzi alitabiri mapema kuwa wale tumbili wasingemkimbia yule mkufunzi. Yule mkufunzi alikuwa mzungu. Na ndivyo ilivyotokea na akapita pale karibu yao kabisa bila kumkimbia.

Mimi ninao uzoefu wa kuishi karibu na tumbili. Huyo aliye kwenye picha ni mmoja kati wengi wa makundi makubwa ya tumbili yaliyopo hapa Butiama. Niliwaambia wenzangu kuwa inaelekea kuwa tumbili wanatambua sura za watu na hukumbuka na kuzigawanya sura hizo katika makundi mawili – wale ambao wanaweza kuwa hawatishii usalama wao na wale ambao wanatishia usalama wao. Nikiwa Butiama, wakati nafanya mazoezi ya kutembea kujiandaa kupanda Mlima Kilimanjaro hukutana na tumbili mara kwa mara na huwa hawanikimbii ingawa nimeshuhudia wanawakimbia baadhi ya watu wengine, hasa watoto.
Hawa tumbili wa Butiama wanayo sababu nzuri ya kukaa mbali na binadamu. Tumbili wana tabia ya kuiba mazao ya kilimo na wakazi wengi wa Butiama wanalazimika kuwafukuza tumbili wanaojaribu kuiba hayo mazao. Sijawahi kufukuza tumbili, kuacha mara chache wakati mlango uliachwa wazi na nikamkurupusha tumbili aliyekuwa ananyemelea maandazi yangu asubuhi.yemelea ,aribu kuw

Wednesday, June 15, 2011

Leo katika historia ya Kombe la Dunia 2006: Poland, Trinidad & Tobago, na Paraguay zaaga mashindano


Poland, Trinidad & Tobago, na Paraguay ziliaga mashindano ya Kombe la Dunia.

Poland ilipoteza michezo yake yote miwili ya Kundi A, kwanza kwa Ecudaor (0-2), halafu kwa Ujerumani (0-1). Ingawa ilishinda mechi yake dhidi ya Costa Rica (2-1), haikutosha kuivusha na kuingia raundi ya pili. Ni ushindi wa Ecuador wa 3-0 dhidi ya Costa Rica uliyoivusha Ecuador, na kuiondoa Poland kwenye mashindano.

Trinidad & Tobago, katika ilipangwa na England, Sweden, na Paraguay katika Kundi B. Yenyewe ilitoka sare mechi moja tu na Sweden (0-0), na kupoteza mechi mbili. Tarehe ya leo, mwaka 2006, Trinidad & Tobago ililazwa 2-0 na England na kuyaaga mashindano, ikiwa ya mwisho kweye kundi lake.

Paraguay, ilishika nafasi ya pili toka mwisho kwenye kundi lake baada ya kufungwa 1-0 na Sweden, tarehe 15 Machi 2006, na timu ikapanda ndege kurudi Ascuncion.

Kwenye Kundi A Ujerumani na Ecuador ziliingia randi ya pili, wakati ni England na Sweden zilizoingia raundi ya pili toka Kundi B.