Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Monday, July 4, 2011

Lugha Yetu Kiswahili: Kwa matumizi haya, Kiswahili kitaangamia


Suala moja ambalo linajidhihirisha mara kwa mara katika miaka ya hivi karibuni ni matumizi mabaya ya lugha ambayo yamejikita katika mazungumzo na hata maandishi ya kila siku ya lugha ya Kiswahili.

Mimi naamini mtu yoyote anayefahamu lugha yake, au anayetaka kulinda matumizi sahihi ya lugha yake hawezi kupuuza matumizi sahihi ya lugha, lakini kwa mwenendo wa matumizi ya lugha ya Kiswahili ulivyo siku hizi, hasa kwa vijana, Kiswahili kina wakati mgumu na uwepo wake uko hatarini.

Mimi nakubaliana na wanaosema kuwa kuna ulazima wa lugha kubadilika na msamiati kuongezeka kila muda unavyozidi kupita. Lakini siyo kwa mtindo huu wa sasa ambapo maneno sahihi yanageuzwa kuwa maneno yasiyo sahihi, na misemo isiyofaa kutumika hata kwenye vyombo vya habari. Nitoe mifano michache:

Vijimambo: Hili neno nimewahi kusikia watu wazima wakilizungumza. Ni afadhali ingekuwa vijana peke yao kwa kuwa wao wanajulikana kwa kutunga maneno mapya. Kwa uelewa wangu mimi lina maana ya mambo kadha wa kadha ambayo msemaji hawezi kuyaweka bayana na hutumia neno hilo kufunika hayo asiyoweza au asiyotaka kuyasema kwa wakati ule. Ushauri wangu ni kuwa kama huwezi kulisema inawezekana halistahili kusemwa.

Ndivyo sivyo: Huu msemo nimeusikia ukitumika na baadhi ya wanahabari na nashindwa kabisa kuelewa mwanahabari anawezaje kuacha kutumia lugha ambayo inaweka wazi maana anayokusudia badala ya msemo unaomlazimu msikilizaji kukisia maana inayokusudiwa.

Kudadeki: Kwa kadiri ninavyofahamu mimi chimbuko la hili neno ni tusi la nguoni na limeingia katika matumizi ili kuepuka mtumiaji kusema lile tusi lenyewe. Cha ajabu ni kuwa nimeshasikia tangazo kwenye redio la kampuni moja ya simu wakitumia neno hilo. Kama linatumika kwenye tangazo muda si mrefu litakuwa kwenye matumizi ya kawaida ya lugha. Ukiuliza maana yake sidhani kama wengi wa wanalolitumia wanafahamu kwa uhakika, lakini mimi naamini kuwa hili neno linatokana na tusi zito tu.

Kwa mtindo huu, Kiswahili kitapona?

No comments: