Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Saturday, March 27, 2010

Mada yangu ya leo: biashara ya fedha za kigeni

Jambo moja ambalo napata shida sana kulielewa ni taratibu za kuendesha biashara ya fedha za kigeni nchini Tanzania.

Unapokwenda kubadliisha fedha za kigeni kwenye mabenki au maduka ya fedha za kigeni baadhi ya sehemu hizo hazipokei fedha za Marekani zenye tarehe kabla ya mwaka fulani (nadhani ni 2003). Hivi karibuni niliposindikiza wageni kubadilisha fedha zao na nilipouliza ni kwanini kuna utaratibu kama huu, niliambiwa na mfanyakazi mmoja wa tawi la benki moja iliyopo Musoma kuwa Benki Kuu ya Tanzana inaelekeza kuwa pesa hizo zisibadilishwe na badala yake zichukuliwa pesa zenye miaka ya hivi karibuni, yaani kuanzia 2004 na kuendelea.

Hili ni jambo la ajabu sana, kwa sababu Tanzania ndiyo inaweza kuwa moja ya nchi chache duniani ambayo inakataa fedha ambazo wenyewe waliyozitengeneza hawana tatizo nazo. Nadhani Wamarekani wanaofika Tanzania na dola zao wakiambiwa kuwa hapa hazina thamani, hubaki kushangaa tu. Hapa Tanzania mteja anapunjwa kwa kupewa thamani ndogo ya fedha anazobadilisha wakati wanaobadilisha wanapata thamani ile ile ya fedha ya kigeni huko nje.

Jambo lingine ambalo linaruhusiwa na taratibu za Benki Kuu ni kuweka viwango taofauti kwa noti zenye thamani kubwa (mfano za mia, na za hamsini), na viwango vya chini kwa noti zenye thamani ya chini (mfano za ishirini, na kwenda chini).

Kwa kuweka viwango viwili tofauti, ni kama vile vile mteja anafanyiwa hisani kubadilishiwa zile noti za thamani ndogo. Aidha ni kama vile huko nje noti hamsini zenye thamani ya dola moja moja zina thamani ndogo zaidi kuliko noti moja ya dola hamsini. Wanaobadilisha noti zenye thamani ndogo kwa kiwango cha chini wanapata thamani ile ile ya pesa ya kigeni wanapoipeleka nje, lakini mteja anapunjwa.

Hivi karibuni nilimsindikiza rafiki yangu Mtanzania anayesoma Uingereza kubadilisha fedha kwenye benki mojawapo ya Musoma na alipopewa viwango tofauti, hakuelewa somo. Aling'ang'ania kiwango cha juu mpaka benki wakakubali yaishe na kumbadilishia paundi zake za Uingereza kwa kiwango kile cha juu.

Kuna wakati nilipolalamika kwa mfanyakazi wa kampuni ya simu na kutaka kufahamu sababu ya kuruhusu mawakala wao kuuza vocha kwa bei inayozidi thamani iliyochapishwa juu ya vocha yenyewe (mfano, kuuza vocha ya sh.1,000/- kwa sh.1,100/-), niliambiwa kuwa hawawezi kuingilia kwa kuwa tuko kwenye mfumo wa biashara huria. Sikuelewa. Naamini pia jibu kama hilo linaweza kutumika kutetea huu utaratibu wa viwango tofauti vya kubadilisha fedha za kigeni.

Maoni yangu: hii siyo biashara huria; ni ujambazi tu uliyoidhinishwa na sheria na taratibu.

1 comment:

Mija Shija Sayi said...

Si katika biashara ya fedha za kigeni tu, ukiangalia katika mambo mengi bado ni wapuuziaji tu. Watanzania bado tuna safari ndefu.