Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Tuesday, March 30, 2010

Wageni: Mke wa Rais, Mama Salma Kikwete azuru Butiama

Picha: Mama Salma Kikwete (kulia) akihutubia kijijini Butiama leo asubuhi. Kushoto ni Mkuu wa Mkoa wa Mara, Kanali Mstaafu Enos Mafuru

Mke wa Rais Jakaya Kikwete, Mama Salma Kikwete, leo asubuhi alifanya ziara fupi kijijini Butiama ambapo alitembelea kituo cha afya cha Butiama, pamoja na kutoa msaada wa vifaa vya hospitali.

Akiwa pia Mwenyekiti wa Taasisi ya Wanawake na Maendeleo (WAMA), alichukuwa fursa katika hotuba yake kuelezea madhumuni ya WAMA kuwa ni pamoja na kuhamasisha uboreshaji wa afya ya wanawake na watoto, kuhimiza maendeleo ya elimu, hasa kwa wasichana, pamoja na kutahadharisha juu ya janga la UKIMWI.

Aliwaasa wanafunzi wa kike waliyohudhuria mkutano wake kutokubali vishawishi vya wavulana, vishawishi ambavyo alisema vikikubaliwa vitaleta athari kwa msichana na maendeleo yake ya elimu.

Wakati wa ziara yake alipewa zawadi ya ng'ombe na Halmashauri ya Wilaya ya Musoma ambae alinunuliwa kutoka kwa mfugaji mashuhuri wa ng'ombe wa maziwa wa Butiama, Nashon Jirabi.

Nashon siyo mfugaji mzuri tu wa ng'ombe, bali amenijulisha kuwa ana kuku 200 wa mayai na anavuna zaidi ya trei 4 kila siku. Kwa bei ya Sh.5,000/- kwa trei moja, siyo pesa mbaya ukizingatia kuwa atavuna hayo mayai kwa kipindi cha miaka miwili. Inashinda biashara ya gari kwa mbali na hakuna visingizio vya kukamatwa na askari wa usalama barabarani.

Nashon pia amewahi kufanya kazi kama operata wa magari makubwa katika machimbo ya dhahabu ya Buhemba, pamoja na machimbo yaliyopo karibu na Lubumbashi, katika Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo.

Picha: Mama Kikwete (katikati ya picha) akitoa shukurani baada ya kukabidhiwa zawadi ya ng'ombe wa maziwa.

Picha: Kushoto ni mwanakiji mwenzangu, Nashon Jirabi akiwa na Mbunge wa Musoma Vijijini Mh. Nimrod Mkono (katikati), pamoja na Mwenyekiti wa Kijiji cha Butiama, Zacharia Mang'ararya Wambura ambaye anajulikana zaidi kama "Debe Tupu" kabla ya kukabidhi zawadi ya ng'ombe kwa Mama Kikwete.
Picha: Nashon Jirabi (kushoto), Mbunge Nimrod Mkono (katikati), na Mwenyekiti wa Kijiji cha Butiama, "Debe Tupu."

Picha: Nashon akizungumza na Mbunge wa Musoma Vijijini Mh. Nimrod Mkono wakati wakisubiri kuwasili kwa Mama Salma Kikwete

No comments: