Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Wednesday, September 29, 2010

Kisa cha kuacha kuvuta sigara: safari yangu ya kupanda Mlima Kilimanjaro (makala ya saba kati ya kumi)


Jumamosi 23 Agosti 2008
Tuliamka kukiwa na hali nzuri ya jua na tukaanza mpando mmoja mkali kuelekea Kambi ya Barafu. Nagundua mabadiliko kidogo; najihisi kama nina nishati ya ziada kidogo. Hii itakuwa ni Red Bull. Nilijadiliana kwa kirefu na Yahoo uwezekano wa kuleta watu wengine kupanda Mlima Kilimanjaro mwakani iwapo nitafanikiwa kufika kileleni. Hii itakuwa Red Bull iliyonipa ujasiri wa kufikiri kuwa upo uwezekano kwangu wa kufika kileleni.

Tulifika Kambi ya Barafu (iliyopo mita 4,600 juu ya usawa wa bahari) ikikaribia wakati wa mlo wa mchana na tukala saa 8 mchana. Najihisi kama, kadiri siku zinavyopita, mwili wangu unaanza kuzowea hali ya kuwa kwenye nyanda za juu. Yahoo, pamoja na kuwa kila wakati anazungumzia mikakati ya kujitoa iwapo nitashnidwa kuukabili Mlima, amesema kuwa naonekana mwenye hali nafuu leo.

Kwenye kambi ya wahifadhi kuna mtu alikuwa anauza makopo ya bia ya Kilimanjaro kwa Sh.3,000 kila moja, na bei hiyo hiyo kwa Coca Cola. Ukilinganisha ni jinsi gani tulivyo juu kutoka usawa wa bahari, unaweza kusema kuwa bei hizo ja juu ni muafaka kabisa.

Tulikutana tena na kundi la wale vijana wa Kijerumani, waliyotupita karibu na Lava Tower jana, wakiteremka kutoka kileleni. Niliambiwa kuwa walipitiliza Kambi ya Karanga [kambi ambayo sisi tulilala] na yawezekana kuwa walilala kwa saa chache tu kwenye Kambi ya Barafu kabla ya kuanza kuelekea kileleni.

Leo hii nina uzoefu wa kutosha wa kupanda milima kiasi cha kuweza kutoa ushauri kwa wanafunzi wasiyo wazoefu. Siwezi kupendekeza kupanda Mlima huu kwa mtu ambaye:
  • hafanyi mazoezi mara kwa mara
  • hawezi kustahimili hali ya baridi
  • hukaa ofisini kuanzia Jumatatu hadi Ijumaa na kuhamia kwenye kaunta ya baa kati ya Ijumaa na Jumapili
  • saa chache baada ya kuanza kutembea atafikiri, "Hivi huku nimefuata nini? Naweza kuwa kwenye chumba chenye joto, napata laga yangu moja baridi, na nikiangalia kwenye luninga ligi ambayo hupendelea sana kuangalia."

Ukikusudia kupanda huu mlima lazima uwe unasukumwa na jambo moja zito sana. Mimi nimechagua kuchangisha pesa kwa ajili ya elimu. Nimekuwa najaribu kufikiria kwa nini mtu yoyote awe tayari kulipa pesa na ajiingize kwenye fatiki kubwa kiasi hiki na bado nakosa jawabu. Naweza kuandika orodha ndefu ya marafiki zangu, wanafamilia, na washirika wangu ambao hawatakuwa tayari hata kulipwa pesa kuja kupanda mlima huu.

Kesho, nitafahamu iwapo ninazo sifa za kuweza kufika kwenye kilele kirefu kuliko vyote vya bara la Afrika. Leo, tunauona mlima vizuri kabisa na naanza kuhisi kuwa kesho nitapambana na kasheshe isiyo ya kawaida. 
Naanza kutafakari msemo niliyousikia kuwa "kupanda Mlima Kilimanjaro ni mtihani wa kisaikolojia zaidi kuliko wa maguvu." Ninavyautazama mpando mkali wa kesho, naanza kuelewa uzito wa usemi huo:
Nimesimama mbele ya Mlima Kilimanjaro katika safari ya kuelekea Kambi ya Barafu

 inawezekana vipi kwa mtu yoyote ambaye anapanda mlima huu kwa mara ya kwanza kushindwa kuelewa uzito huo.

Wakati najiandaa kulala joini namwambia Le kuwa mpaka sasa sehemu ngumu kabisa ya kupanda mlima huu inanikumba ninapokwenda chooni. Nikiwa nyumbani ninayo fursa, ambaye nadra kuitumia, ya kufungua gazeti na kulisoma nikiwa maliwatoni; hapa Kilimanjaro nalazimika kuchuchumaa. Mimi napata shida kubwa kuchuchumaa sehemu yoyote, wacha mlimani. Kwa hiyo kuchuchumaa mita 4,600 juu ya usawa wa bahari ni mtihani mkubwa sana kwangu.

Kwenye nyanda za juu hata kufunga kamba za viatu inahitaji kuhenyeka kwa hali ya juu. Asubuhi nafunga kamba ya kiatu kimoja halafu inabidi nipumzike na kuvuta pumzi kwa kama dakika tano hivi kabla ya kufunga kamba ya kiatu cha pili. Kwenda chooni inahitaji mara mbili ya nguvu inayotumika kufunga kamba za viatu.

Leo nilishuhudia wakweaji watatu wakiwasili Kambi ya Barafu na nikaona nyusa zao zilizogubikwa uchovu mkubwa na nikawaza: kama hivi ndivyo na mimi huonekana kila ninapofika kambini baada ya kutembea kwa siku nzima, basi kupanda huu mlima siyo mchezo hata kidogo.

Nimeshaamua kuwa huu mlima ni wa kupendezesha macho tu na wa kusifiwa kwa mbali, na pengine wa kusifiwa na kutazamwa kwenye picha lakini, kwa hakika, siyo mlima wa kukwea hata kidogo.

Makala ijayo: Kilele cha Uhuru na Kambi ya Crater


Makala zinazohusiana na hii:

No comments: