Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Sunday, September 5, 2010

Amani Millanga atoa maoni yake kuhusu uchaguzi

Sera za Serikali za Majimbo ni Hatari kwa Utaifa Wetu
Na Amani Millanga
-------------------------------------------------------------------------
Amani Millanga ni mhadhiri wa Chuo Kikuu cha St. Augustine ambaye yuko masomoni kwenye Chuo Kikuu cha Leicester, nchini Uingereza, akisomea shahada ya uzamivu katika mawasiliano ya umma. Tasnifu ya shahada yake ni  Broadcasting for Sustainable People Centred Development in Tanzania: A Case Study of TBC as a Tool for Eradicating Extreme Poverty. Tafsiri isiyo rasmi ya tasnifu ni: Upashaji Habari kwa ajili ya Maendeleo Endelevu ya watu nchini Tanzania: Uchunguzi Kifani wa TBC kama chombo cha Kufuta Umaskini Uliyokithiri.

Nimetuma ombi kwa CHADEMA wajibu hoja za Amani Millanga na mara nitakapopata majibu hayo, nitayaweka hapa. 

--------------------------------------------------------------------------------------------
Amani Millanga, kushoto, akiongea na David Saragana, Afisa Kilimo wa Kijiji cha Butiama kama sehemu ya utafiti anaofanya kwa ajili ya masomo yake ya uzamili.

Hatuzihitaji na Hatuziamini
Tukielekea katika uchaguzi mkuu tutayasikia mengi na ahadi lukuki kutoka kwa wagombea wa urais, ubunge na udiwani kwamba wakichaguliwa Tanzania itajaa neema na kila mmoja wetu atayaona mabadiliko makubwa yakienda sambamba na ukuwaji wa uchumi. 


Wagombea wanawajengea watu matumaini na hamu ya kuiona Tanzania hiyo ya ahadi. Pasina shaka ahadi wanazozitoa wagombea zinatokana na sera za vyama vyao.

Sera ndizo dira na mwelekeo mgombea na chama chake katika kuijenga Tanzania yetu. Hivyo basi sera za kiutawala za chama chochote kinachotuomba ridhaa ya kutuongoza ni lazima ziwe zinalenga kujenga nchi na taifa lenye umoja, udugu, amani na mshikamano.

Ndugu zangu, vipo vyama vinawania kuliongoza taifa letu vyenye sera za kimajimbo. Chama chenye sera kama zino hatukihitaji na wala hatukiamini kukipa dhamana ya kutuongoza kwani kitatupeleka pabaya hata kama zake sera nyingine ni nzuri kiasi gani.

Siku zote ustawi wa taifa na watu wake huanzia kwenye umoja na amani katika taifa husika. Matokeo ya sera za serikali za majimbo ni kuondoa umoja, udugu na hatimaye utaifa mambo ambayo ni muhimu katika kuijenga na kuilinda amani ya nchi, uchumi na ustawi wa watu wake.

Ukaburu
Ukiongelea serikali za majimbo katika Tanzania bila shaka unaongelea umkoa na ukabila. Mambo haya mawili hayasigani na ni hatari kwa umoja wetu, amani yetu, udugu wetu na utaifa wetu kama watanzania. Sera hizi za majimbo ni sera za kupandikiza mbegu chafu ya ukabila itakayoigawa Tanzania. Baadhi yetu
wanaweza kuwa wanazishabikia lakini ukweli unabaki pale pale kuwa zitatumaliza.

Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere alituusia kuwa tuwaogope kama ukoma wale wenye sera za ukabila, umkoa, udini au rangi za ngozi za watu kwani ni wabaguzi na hawana tofauti na makaburu. Bila shaka sera za serikali za majimbo ni za kibaguzi na hazitufai katika nchi yetu.

Tanzania Jimbo Letu
Wapo wanaosema mbona Nigeria au Marekani hata India kuna serikali za majimbo, kwa nini isiwe hapa kwetu Tanzania? Tena watakupa mifano ya mafanikio ya serikali za majimbo katika nchi hizo. Lakini wanasahau kwamba Tanzania kama taifa na nchi inayo historia yake ambayo imejengeka katika misingi imara ya kujiona kuwa sisi sote ni watanzania na kabila letu wote ni watanzania na jimbo letu ni Tanzania.

Utamaduni wetu wa kuulizana kabila au mkoa atokao mtu ni kutaka ujue kama ni mtani wako na mtaniane na si vinginevyo. Lakini tukileta serikali za majimbo tutaanza kuulizana tunatoka mikoa gani ili tubaguane na tuwapendelee wale tunaotoka nao mkoa mmoja na kabila moja. Haya yapo India, Nigeria na hata Marekani. Serikali za majimbo kimsingi zitawaongezea wananchi mzigo wa gharama za kuiendesha serikali kuu na serikali za majimbo zenye mabunge na msululu wa viongozi. Nigeria ni mfano hai.

Tanzania Kuparaganyika
Kwa kuwa sisi ni taifa changa, sera hizi za kimajimbo zitaturudisha kule tulikotoka kabla ya uhuru – Nchi bila Utaifa. Na bila shaka huo ndio mwanzo wa Tanzania kumegeuka na kupasuka vipande vipande. Hakika huo ndio mwanzo wa watu wa jimbo fulani kujiona wao ni bora kuwazidi watu wa jimbo jirani. Huo ndio mwanzo wa jimbo fulani kutangaza kwamba raslimali zote zilizoko kwenye jimbo hilo ni zake na wala zisitumike kwa manufaa ya majimbo mengine. Huo ndio mwanzo wa kusikia siku moja Kagera inatangaza kujitenga na kuwa nchi. Hapo Tanzania kama nchi na taifa haitakuwepo tena. Kama Mwalimu Nyerere angekuwa na fikra hizi za
kimajimbo basi Rukwa, Kigoma, Dodoma au Singida kusingekuwa na kitu au maendeleo yeyote.

Hitimisho
Ndugu zangu, tukielekea kwenye masanduku ya kupigia kura tukumbuke kuwa sera ya serikali za majimbo ni kitanzi cha kuunyonga utaifa wetu, umoja wetu na amani yetu. Tuzikatae sera hizi kwa kuwanyima kura zetu. Kinga ni bora kuliko tiba.

No comments: