Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Thursday, September 13, 2012

Mada yangu ya leo: kufahamu Kiingereza siyo kuwa msomi

Mada yangu leo si ndefu sana, lakini naamini ni muhimu.

Nianze na tukio moja la zamani. Niliwahi kufahamiana na raia mmoja wa Uingereza ambaye aliishi na kufanya kazi Dar es Salaam kwenye miaka ya tisini, akiwa mwajiriwa wa kampuni moja ya ulinzi. Huyu alikuwa mtu mmoja mcheshi, na mchangamfu kwa wengi aliyefahamiana nao ingawa kwa aliyewaongoza kazini alikuwa mkali sana.

Kuna Mtanzania mwenzangu ambaye naye alikuwa akifahamiana naye na alimheshimu sana, siyo tu kama binadamu mwenzake lakini naamini kwa wadhifa wake muhimu wa kuongoza kampuni yenye wafanyakazi wengi wenye jukumu la kulinda mali na makazi ya wateja wa hiyo kampuni.

Miaka kadhaa ilipita na yule Mtanzania mwenzangu siku moja aliniambia: "Unafahamu? Kumbe yule jamaa amesoma mpaka darasa la nne tu!"

Mtanzania mwenzangu, ambaye alikuwa na shahada ya chuo kikuu, hakuamini kuwa mtu aliyemdhania ni msomi mwenzake kumbe alikuwa amesoma mapaka darasa le nne tu, pamoja na kupewa jukumu la kuongoza kampuni moja mashuhuri ya Tanzania.

Tatizo nililoliona mimi lilikuwa la lugha. Kwa kipimo cha Mtanzania mwenzangu yule Mwingereza alikuwa anazungumza Kiingereza safi kabisa kuliko ambacho yeye alikuwa anamudu kuongea na kwa mantiki aliyofikia ingekuwa ni dhahiri kuwa yule jamaa alikuwa ni msomi. Kwa sababu tu anaongea Kiingereza kizuri kuliko cha kwake.

Nilimuuliza: "Sasa utamdharau kwa sababu ya ya elimu yake, wakati wote huo ukimwona ni mtu wa maana sana?"

Haya yalitokea zaidi ya miaka 20 iliyopita lakini tatizo la kumpa mtu uzito mkubwa zaidi kwa sababu anaongea Kiingereza vizuri bado lipo mpaka leo.

No comments: