Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Friday, March 15, 2013

Kutotumia reli kunaua uchumi (sehemu ya pili kati ya mbili)


Katika makala hii yenye sehemu mbili, Dk. Amani Millanga anasisitiza umuhimu kwa Taifa wa kuendeleza mfumo wa reli.
*****************************************
KUTOTUMIA RELI KUNAUA UCHUMI (sehemu ya pili kati ya sehemu mbili)

Hapo utaona kwamba katika reli kuna ajira nyingi sana rasmi zenye mafao ya uzeeni kwa vijana wetu. Ajira hizi zitaongeza mapato kwa serikali kwani wafanyakazi watakuwa wanalipa kodi. Reli itatoa chachu ya kukua kwa viwanda vya kufua chuma, kutengeneza vipuri, n.k. na kuifanya Tanzania iingie tena katika mapinduzi ya viwanda na hasa viwanda vizito. Hili litasaidia kukuza ubunifu, uzoefu, utafiti na teknolojia nchini katika nyanja zote za viwanda vinavyogusa reli. Juu ya hayo reli ni usafiri wa uhakika wenye uwezo wa kusafirisha abira wengi zaidi ya mabasi na kwa usalama zaidi na kupunguza idadi ya vifo vitokanavyo na ajali za mabasi ambavyo vimewaacha watoto wakiwa yatima na wanawake wakiwa ni wajane. 

Nini kifanyike? Mosi, serikali imiliki shirika la reli. Pili, serikali iunde upya shirika la reli na liwe na muundo wa kujiendesha kwa faida kwa mujibu wa kanuni za biashara na menejimenti kwa ufanisi, uaminifu, kiushindani na kutoa huduma bora za kisasa. Tatu, serikali ijenge njia ya pili kwa reli zetu zilizopo hivi sasa ili iwe rahisi kusafirisha bidhaa na abiria kwa usalama zaidi. Ujenzi huu utanguliwe na ujenzi wa ki/viwanda cha/vya kufua chuma ili kuzalisha chuma cha pua ambacho hutumika katika ujenzi wa reli, kutoa ajira kwa vijana na kupunguza gharama za kuagiza vipuri na vifaa vingine nje ya nchi. Pesa ya kujenga njia ya pili ya reli kutoka Dar es Salaam kwenda Kigoma inatosha kabisa kujenga kiwanda cha kufua vyuma na kubakiza mtaji wa kukiendesha kiwanda hicho.
Nchi zilizoendelea zimewekeza kwenye mifumo ya reli na kufanikisha kupunguza gharama za usafirishaji. Picha ya Daniel Steger inatumiwa kwa utaratibu wa Creative Commons, CC:Attribution-ShareAlike.
Hakuna nchi duniani imeendelea bila kuwa na ki/viwanda vya kufua chuma. Hata historia ya mwanadamu inaonyesha mababu zetu waliweza kupiga hatua haraka za kimaendeleo pale tu walipogundua namna ya kufua chuma (nitaliongelea zaidi katika maoni yangu kuhusu viwanda vyetu).

Mkaa wa mawe na chuma huko Mchuchuma vingetusaidia sana katika hili. Nne, serikali kupitia shirika la reli inunue treni ziendazo kwa kasi. Tano, shirika la reli liweke utaratibu mpya wa kusafirisha abiria. Mfano, kwa treni iendayo kwa kasi kutoka Mwanza hadi Dar es Salaam isimame katika vituo vikubwa tu navyo visiwe zaidi ya kumi (mfano: Morogoro, Dodoma, Singida, Tabora, Shinyanga na vituo vingine vitano muhimu hapo katikati) na itumie masaa yasiyozidi 24 kusafiri kati ya Dar es Salaam na Mwanza. Pia baina ya vituo vikubwa ziwepo treni za kuhudumia vituo vidogo vidogo. Kwa mfano treni iendayo kwa kasi ikitoka Mwanza isimame Shinyanga lakini hapo katikati iwepo treni ya kuhudumia vituo vidogo vidogo kati ya Mwanza na Shinyanga. 

Tano, mfumo wa mawasiliano katika treni uboreshwe ili kuepusha ajali na hasa wakati njia moja tu inatumika kabla ya kujenga njia ya pili. Sita, serikali ijenge reli katika maeneo mengine ya nchi. Saba, shirika la reli liwe na ufanisi katika kupakia na kupakua mizigo. Idara hii ihakikishe mizigo haipotei na inafika katika muda uliopangwa.

Nane, tuna nchi sita jirani zinategemea bandari zetu. Reli ingeweza kuzihudumia nchi hizi kwa faida kubwa. Hivyo basi bandari za nchi kavu kama Isaka zingekuwa vituo kikubwa vya ajira na biashara. 

Je, tunashindwa kuyafanya haya? Naamini kwa nia safi na uzalendo tunaweza. Kinyume chake ipo siku tutakuta mwekezaji ameing’oa  reli  na kuiuza kwa vyuma chakavu.

No comments: