Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Friday, March 15, 2013

Tathmini ya muziki wa Tanzania mwaka 2012 (sehemu ya kwanza kati ya nne)

Katika makala hii nitakayoitoa katika sehemu nne, mwanamuziki mashuhuri John Kitime, anafanya tathmini ya hali ya muziki Tanzania mwaka 2012.
******************************************
Tathmini ya muziki wa Tanzania mwaka 2012

makala ya John Kitime

(Sehemu ya kwanza kati ya sehemu nne)

Mwaka 2012 ndiyo huo umetokomea Ni vizuri kuangalia yaliyopita ili kujitayarisha na yajayo. Muziki wa nchi yetu ulitawaliwa na muziki wa Bongoflava, Taarab, muziki wa bendi, matarumbeta, muziki wa injili, na muziki wa kiasili.

Si siri kuwa muziki wa Bongoflava ndiyo uliokuwa ukitawala katika vyombo vya habari na sehemu nyingi za maonyesho ukifuatiliwa na muziki wa Taarabu na muziki wa injili. 

Katika muziki wote huu jambo lililokuwa wazi ni kuwa waimbaji ndiyo waliokuwa wakipewa kipaumbele katika tasnia hii.  Waimbaji katika aina zote za muziki uliotajwa hapo juu ndiyo waliotajwa na kupewa sifa kwa ubora wa muziki. Kumekuweko na mashindano kadhaa ambayo yote yamejikita katika kutafuta vipawa vya waimbaji japo mara nyingi yamejitambulisha kama mashindano ya kusaka vipaji mbalimbali.

Hakuna ubishi muziki wa dansi na muziki wa asili ndiyo muziki uliopewa muda mchache sana katika vyombo vya habari. Na hata katika muziki huo, bendi ambazo zimejikita kufuata mipigo ya Kikongo zilipewa nafasi zaidi ya bendi ambazo zimejichagulia njia nyingine za muziki wao.

Kuna sababu kadhaa ambazo zimefanya muziki wa Bongoflava kuchukua nafasi zaidi katika vyombo vya habari. La kwanza ni uwingi wa kazi za Bongoflava zinazorekodiwa. Karibu kila mji una studio ya aina moja au nyingine, na katika studio hizo kazi nyingi zaidi zinazorekodiwa ni aina hiyo ya muziki, hivyo kutokana na uwingi wa kazi hizo ni wazi kabisa ndizo ambazo zitaendelea kutawala anga ya vyombo vya habari, na pia ni kutokana na mfumo wa vyombo vyetu vyote kujikita katika mfumo wa aina fulani tu za muziki.

Kwa mtazamo wangu heka heka za muziki wa injili zilipungua 2012. Yale matamasha makubwa ya muziki huo yalipungua sana, na hata nyimbo za kushtua jamii hazikuwa nyingi  kama ilivyokuwa miaka ya nyuma.

Muziki wa Taarabu haujaleta mabadiliko kimuziki. Mengi yaliyofanywa katika 2012 ni marudio tu ya ubunifu uliofanyika nyuma. Kama vile uanzishwaji wa kucheza show katika taarabu, upigaji wa gitaa na kuliachia peke yake kama ilivyokuwa kwa bendi kuachia gitaa la rhythm miaka kabla ya tisini na zile video za kucheza mbele ya viwanja vya hoteli. Kumekuweko tu ubunifu wa misemo na mipasho, jambo tena ambalo limesababisha kuenziwa zaidi kwa waimbaji tu katika fani hiyo pia.

Bendi ziko katika wakati mgumu. Wakati wanamuziki wengi wa bendi wakilalamika kuwa muziki wa bendi haupigwi, kumekuweko na jitihada ndogo za bendi kurekodi nyimbo mpya, maelezo mengi yamekuwa ni kuhadithia enzi ambapo muziki wa bendi ulitawala na kuona kama hiyo ni sababu tosha ya muziki huo kurushwa hewani. Bendi chache zilizorekodi hazijaja na  nyimbo zilizoweza kuteka umma wa Watanzania na hivyo kusababisha muziki huu kukosekana katika anga za muziki. Matangazo mengi ya muziki wa dansi yamekuwa ni kutangaza rap mpya au kupatikana kwa msanii mpya, lakini kiujumla hakujakuwa na kitu kipya katika muziki wa bendi.

(itaendelea)

Taarifa zinazohisiana na hii:
sehemu ya pili ya makala hii
sehemu ya tatu ya makala hii

No comments: