Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Sunday, March 17, 2013

Tathmini ya muziki wa Tanzania mwaka 2012 (sehemu ya pili kati ya nne)

Katika makala hii nitakayoitoa katika sehemu nne, mwanamuziki mashuhuri John Kitime, anafanya tathmini ya hali ya muziki Tanzania mwaka 2012.
******************************************
Tathmini ya muziki wa Tanzania mwaka 2012

makala ya John Kitime

(Sehemu ya pili kati ya sehemu nne)

Muziki asili pia umekosekana kwenye vyombo vya habari kwa kuwa si vikundi vingi vya muziki huu vyenye uwezo wa kulipia gharama za studio ambao muziki huu unastahili kurekodiwa. Studio nyingi zimejengwa kwa ajili ya muziki wa aina ya Bongoflava tu. Zile studio za kuweza kuruhusu kundi la muziki wa asili kurekodi gharama yake huwa ni kubwa sana.

Kundi la Makirikiri lilitakiwa kuwa elimu tosha kwa wasanii wa muziki wa kiasili, kuwa na muziki huo ukifuata taratibu nzuri ya kurekodiwa unauza vizuri sana. Bahati mbaya kuna vikundi sasa vimeacha muziki na ngoma zao, vinaiga uchezaji wa Makirikiri.

Pengine watu watasema nimesahau muziki wa kwaya; sijausahau. Kwa kweli muziki huu umebaki  hasa kwenye muziki wa injili. Hapo zamani ulikuwa ukitumika sana kwenye siasa na kampeni , lakini kwa mwaka 2012 hali imekuwa mbaya kwa muziki huu.

Pamoja na kuwa wengine wangeweza kusema tunasonga mbele katika muziki, kwangu mimi naona tunarudi nyuma kitaaluma. Tasnia inaingiza pesa nyingi zaidi, na hata kuna wasanii walioingiza pesa nyingi sana, lakini  kwangu hilo si kipimo cha maendeleo katika tasnia hii.

Kama nilivyoanza kusema washika maikrofon wamekuwa ndiyo alama ya muziki wa Tanzania. Muziki ni zaidi ya kuimba. Katika kuimba sauti nzuri ya muimbaji ni muhimu, na ninashukuru kwa hilo tunao waimbaji wazuri wengi sana, lakini ule muziki unaomsindikiza muimbaji ni muhimu sana kwani ule hauna mipaka wala lugha, na ndio unaoweza kutufungulia mlango wa soko la kimataifa. Wengi tunapenda sana muziki wa kutoka Kongo, Nigeria, Afrika Kusini; pamoja na kuwa hatujui hata moja wanaloliongelea tunaupenda muziki huo kutokana na mpangilio wa vyombo vyao.

Kutokujali wapigaji katika mfumo wa nchi yetu ndiyo unatupelekea kuwa watu wa ‘copy and paste’ wa upigaji wa muziki wa nchi nyingine. Ukiorodhesha nyimbo zote zilizotikisa nchi hii kwa mwaka 2012 utagundua asilimia kubwa ya muziki uliotumika ulikuwa ni wa kunakili kutoka muziki wa nchi nyingine, Nigeria, Congo na Afrika Kusini ndiyo wamekuwa waalimu wetu wakuu.

Ushauri kwa ma-producer wa Bongoflava: kuangalia pia muziki wetu wa asili humu ndani ya nchi ili tuje tumalize 2013 na kitu chetu ambacho Wanaigeria, Wakongo nao pia waige toka kwetu. Inawezekana sana maana wimbo wa Weekend wa Afro70 uliwahi kuweko katika  kumi bora 1972, Nigeria.

Muziki wa injili pamoja na kuwa ndiyo unaotegemewa kutufundisha maadili, ulikuwa na kasoro moja kubwa nayo ni kukosa maadili kwa ku-copy na ku-paste. Nyimbo nyingi zilizokuwa maarufu na kuteka hisia za maelfu ya watu zilikuwa ni kuiga moja kwa moja kutoka Afrika ya kusini. Najiuliza je ndiyo kilichopunguza moto wa muziki huu 2012? Kulikuwa hakuna za kukopi? Wanamuziki wa injili kama ilivyo kwa ushauri kuhusu Bongoflava, ni muda wa kurudi nyuma na kutumia rasilimali ya utamaduni iliyoko kuleta mabadiliko na kukuza soko la muziki huo.

(itaendelea)

Taarifa zinazohusiana na hii:

No comments: