Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Thursday, March 14, 2013

Kutotumia reli kunaua uchumi (sehemu ya kwanza kati ya mbili)


Katika makala hii yenye sehemu mbili, Dk. Amani Millanga anasisitiza umuhimu kwa Taifa wa kuendeleza mfumo wa reli.
*****************************************
KUTOTUMIA RELI KUNAUA UCHUMI (sehemu ya kwanza kati ya sehemu mbili)
Dk. Amani Millanga
Kwa miaka zaidi ya kumi Tanzania imezungukwa na taswira iliyokomaa ya kudhoofika kwa njia kuu za usafirishaji za reli, meli na ndege kana kwamba hazina umuhimu wowote katika ujenzi na ukuwaji wa uchumi wa taifa letu na ustawi watu wake. Vituo vyote vya treni vimeota magugu. Reli imegeuka kichaka. Sababu kubwa za kudhoofika huku ni serikali  kushinikizwa na wakubwa kujitoa katika kumiliki njia kuu za usafirashaji. Mashirika yetu ya reli, bandari na ndege yamekufa. Huu ni msiba mkubwa kwa taifa. Athari zake zinatugusa sote na utaziona kwa macho kila pembe ya nchi. Mwaka 2010 niliandika kuhusu Athari za Kutokutumia Reli. Makala haya ni muhtasari yake.

Tanzania inatumia magari mengi sana ambayo yanatugharimu pesa nyingi za mafuta, vipuri na matairi. Matokeo yake ni mfumuko wa bei kwa sababu ya gharama kubwa za usafirishaji. Kwa mfano mwaka 2010 mfuko wa sementi ulikuwa unauzwa sh.9,000 katika maduka ya rejareja jijini Dar es Salaam lakini Mwanza ilikuwa sh 18,000. Gharama za kusafirisha tani moja ya sementi ilikuwa ni sh.150,000 ili hali kwa treni ilikuwa sh.103,663. Hapo utaona zingebaki sh.46,337 mfukoni mwa wananchi kwa kila tani ya sementi, mchele, mahindi, sukari, chumvi n.k. kama tungetumia treni au sh.2,316.85 kwa kila kilo 50.

Kama nchi nzima tungesafirisha kwa kiwango cha chini kabisa tani milioni tano tu kwa treni utapata hesabu hii: sh.46,337 zidisha kwa tani 5,000,000 utapata sh 231,685,000,000 (sh bilioni 231.685) ambazo zingebaki mfukoni mwa wananchi. Hali hii inagusa kila sehemu ya Tanzania. Huko Muleba bei ya sementi ilikuwa ni sh.23,000 mpaka 25,000. Kumbe behewa la sementi lingekuwa linafika Mwanza na kuwekwa kwenye meli ya mizigo hadi Kemondo bila shaka unafuu wa maisha ungekuwa mkubwa kwa mkazi wa Muleba ambaye kipato chake kwa mwaka ni kati ya sh.100,000 na sh.150,000 kwa mujibu wa takwimu za serikali.

Usafiri wa treni pia ni nafuu sana kwa abiria. Mfano nauli ya kutoka Dar es Salaam hadi Mwanza daraja la tatu ilikuwa ni sh.19,000 ili hali kwa nauli ya basi ilikuwa sh.50,000. Hii ina maana sh.21,000 zingebaki mfukoni kwake. Kama watu milioni moja wangetumia treni kwa mwaka 2010 ina maana sh.21,000,000,000 zingebaki mfukoni mwao.

Kampuni ya reli kwa sasa ilikuwa na wafanyakazi 3,220 mwaka 2010 baada ya kupunguzwa kutoka 6,500. Kama shirika la reli litasimamiwa vizuri na serikali litatoa ajira rasmi na zisizo rasmi kwa malaki ya Watanzania. Miongoni mwa ajira rasmi ni pamoja na wahandisi wa ujenzi na ukarabati wa treni na reli, madereva wa treni, mafundi katika karakana, wahudumu katika treni za abiria, wakata tiketi katika vituo, watunza takwimu za usafirshaji mizigo, wapakua mizigo kwenye mabehewa na hata wafanyabiashara kama kina mama lishe na baba lishe katika vituo vya treni.

Kwa mfano kutoka Dar es Salaam hadi Mwanza kuna vituo 68, na kutoka Dar es Salaam hadi Kigoma kuna vituo 85. Fikiria reli ya kwenda Mpanda na ile reli ya Tanga, Moshi na Arusha, ile ya Mtwara na Lindi, na TAZARA kuanzia Mbeya hadi Dar es Salaam. Fikiria ajira za wasomi wetu waliosomea usimamizi wa biashara, takwimu, uhasibu n.k. ambao wangepata ajira katika kila kituo cha treni. Fikiria ajira katika viwanda vitakavyokuwa vinafua chuma kwa ajili ya kutengenezea mataluma, kupasua kokoto, karakana, sementi, rangi, ufyatuaji matofali, vioo, upasuaji mbao n.k kwa ajili ya kujenga reli mpya na vituo vipya.

(itaendelea)

sehemu ya pili ya makala hii

No comments: