Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Friday, December 21, 2012

Dk. Antipas Massawe anasema Muungano umepitwa na wakati (sehemu ya kwanza kati ya sehemu mbili)


Katika makala hii ambayo nitaitoa hapa kwa awamu mbili, Dk. Antipas Massawe anatoa hoja kuwa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar umepitwa na wakati. Ni mawazo yake, si yangu.
*************************************
Muungano wa Tanzania umepitwa na wakati demokrasia ya vyama vingi ilipozaliwa (Sehemu ya Kwanza kati ya sehemu mbili).

Na Dk. Antipas Massawe

Muungano wa kisiasa kati ya Tanganyika na Zanzibar ulizaliwa tarehe 26 April, 1964. Sababu kubwa iliyopelekea kuzaliwa kwake ni moyo waliokuwa nao waasisi wake (Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Sheikh Abeid Amani Karume) wa kuunda muungano wa kisiasa baina ya nchi huru za Bara la Afrika wakianzia na shirikisho la Afrika ya Mashariki. Lengo lilikuwa kulinda na kudumisha mapinduzi ya Zanzibar ya tarehe 12 Januari, 1964 dhidi ya utawala wa wachache wa kisultani ulioondolewa madarakani na kuanzisha ujenzi wa shirikisho la Afrika ya Mashariki na muungano wa Bara la Afrika kisiasa.

Kuzaliwa kwa muungano wa Tanganyika na Zanzibar kulitokana na matakwa binafsi ya waasisi wake na wananchi wa kawaida kutoka pande mbili husika hawakushirikishwa kikamilifu katika zoezi zima la kufanya maamuzi kuhusu kuundwa kwake na haionekani mahali popote upembuzi yakinifu ulifanyika kubaini faida na athari za muungano wenyewe kwa wahusika (ukijumuisha mifumo ya serikali zake zote mbadala: moja (ya Muungano), mbili (ya Zanzibar na ya Muungano), tatu (ya Tanganyika na ya Muungano), nne (ya Zanzibar, ya Tanganyika na ya Muungano) na tano (ya Zanzibar na ya Tanganyika bila ya Muunngano). Kwa kifupi muungano wa Zanzibar na Tanganyika ulizaliwa wakati wa kipindi cha udikteta wa chama kimoja tawala ndani ya pande zote mbili husika kwenye Muungano.

Muungano wa Zanzibar na Tanganyika ni wa pekee na haujawahi kuigwa na wengine mahali popote duniani na umedumu chini ya utwala wa mfumo wa udikteta wa chama kimoja na sasa uko chini ya utawala wa demokrasia ya mfumo wa vyama vingi.

Athari  kubwa kutokana na Muungano hazikuweza kuonekana kwenye kipindi chake cha  awamu ya kwanza chini ya mfumo wa udikteta wa chama kimoja kwani kwenye kipindi hiki chama tawala ndicho kimekuwa kikiamua yote kuhusu maswala ya Muungano kitaifa na jukumu la wengine wote kutoka bara na visiwani lilikuwa ni kubariki maamuzi hayo ya chama kimoja tawala. Kwa mfano, chama kimoja tawala kikishaamua huyu ndiye atakaeyekuwa rais wa Muungano, basi jukumu la wengine wote kutoka pande mbili za Muungano limekuwa ni kupiga kura moja ya ndio kuashiria kubariki kwao chaguo la chama hicho kimoja tawala.

Kwa hiyo kutokuwepo upinzani kutoka vyama vingine vya siasa dhidi ya udikteta wa chama kimoja tawala kuhusu maswala ya Muungano na rais mteule wa chama tawala kutokuwa na ushindani wa wagombea kutoka vyama vya upinzani imekuwa ndiyo sababu ya athari kubwa tarajiwa kushindwa kujitokeza kutokana na utekelezaji wa Muungano huu baina ya Wazanzibari (ambao karibu wote ni Waisilamu) na Wabara (ambao karibu wote ni mchanganyiko wa Waisilamu na Wakristu) na fursa iliyopewa Zanzibar ya kuendelea kuwa na serkali yake ya Zanzibar wakati Tanganyika ikinyimwa fursa kama hiyo ya kuendelea kuwa na serikali yake ya Tanganyika bila sababu zozote za msingi.

Athari ya kwanza kubwa kutokana na huu Muungano wa kisiasa baina ya Wazanzibari na Wabara inatarajiwa kujitokeza kwa nguvu kwenye kipindi chake cha awamu ya pili chini ya mfumo wa demokrasia ya vyama vingi. Kwa mfano itakapojitokeza kwamba miongoni mwa wagombea wa kiti cha urais mmoja ni Mkristu na mwingine ni Mwisilamu basi itarajiwe kwamba karibu Wazanzibari wote ambao ni Waisilamu watajitokeza na kumpigia mgombea Muislamu kura ya ndio bila kuzingatia vigezo vingine vya ubora. Athari ni kwamba Muungano huu utakuwa unatujengea ubinafsi unaoambatana na agenda zenye lengo la kutujengea na kutuimarishia udini ndani ya demokrasia ya vyama vingi na matokeo yake ni Muungano kunyimwa utawala bora pale matakwa ya udini yatakapotawala chaguzi kuu za uongozi ndani ya Muungano na chuki za kidini na migogoro yake na athari zake kuanza kujitokeza  kama ilivyoshuhudiwa huko Zanzibar hivi karibuni.

Athari ya pili kubwa kutokana na huu Muungano uliowapa Wanzanzibari fursa ya kuendelea kuwa na serikali yao ya Zanzibar wakati Wabara wakinyimwa fursa kama hiyo ya kuendelea kuwa na serikali yao ya Tanganyika itarajiwe pia kujitokeza kwenye awamu yake ya pili chini ya mfumo wa demokrasia ya vyama vingi kwani sio haki Wazanzibari kufaidi kushiriki ndani ya serikali ya Tanganyika na bunge lake kupitia serikali ya Muungano na bunge lake wakati Wabara hawana fursa kama hiyo kutokana na kutoshirikishwa ndani ya serikali ya Zanzibar na bunge lake na uwezekano mkubwa wa mgongano wa maamuzi na utekelezaji wa sera za serikali ile ya Zanzibar na za ile ya Muungano.

(itaendelea...)

No comments: