Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Friday, March 16, 2012

Amani Millanga azungumzia maandamano ya Songea (sehemu ya kwanza kati ya sehemu tatu)

Vijana na Maandamano, Polisi na Mauwaji: Tunaelekea Wapi? (Sehemu ya kwanza kati ya sehemu tatu)

Na Amani Millanga

Naomba nitwae fursa hii kuwapa pole wale waliofiwa na ndugu zao waliouwawa na Polisi huko Songea. Poleni sana.

Tunaelekea wapi?
Amani ya Tanzania sasa inatikiswa na hali si shwari nchini. Hali hii inatia hofu na mashaka makubwa kwa Mtanzania mzalendo kwani matukio ya mauwaji yanayotokana na wananchi kuandamana na kuuwawa na polisi yanazidi kuongezeka. Polisi wamewaua raia wasiokuwa na hatia katika sehemu mbalimbali nchini zikiwemo Arusha, Mbeya, na sasa Songea.

Mauwaji haya ni kinyume na maadili na wajibu wa Polisi kwani kazi zao siku zote ni kulinda usalama wa raia na mali zao. Iweje leo Polisi wanawaua raia na kuharibu mali zao? Chuki inayopandikizwa na ukiukwaji huu wa haki za binadamu ni kubwa dhidi ya Serikali na pia kwa Chama cha Mapinduzi. Chuki hii ni kubwa sana miongoni mwa vijana na hata watu wazima, na jambo la hatari zaidi ni kwamba inasambaa kwa kasi zaidi kile pembe ya nchi - mijini na vijijini. Katika makala haya nitawaongelea vijana kwani hawa ndio wamekuwa wakipambana na Polisi.

Wasifu wa Vijana
Vijana ninaowaongelea hapa wana umri kati ya miaka 16 na 40 (ingawa ujana unaanzia miaka 18) na ndiyo walio wengi katika nchi yetu. Pili, ndiyo nguvu kazi ya taifa. Tatu, wengi wao hawana hata elimu ya msingi, na wale waliobahatika kupata elimu ya sekondari wengi wao wamesomea katika sekondari za kata ambazo zimewakata. Nne, wengi wao hawana ajira rasmi yenye pensheni na mafao mengine. Tano, wamekulia katika mazingira ya ulimwengu wa utandawazi (Profesa Shivji anauita UTANDAWIZI) na Tanzania inayokumbatia sana siasa za uliberali mamboleo zilizojaa unyonyaji, dhuluma na uonevu. Sita, ni wahanga wa soko huria ambalo limewaacha wanalia. Saba, wengi wao hawaijui kwa dhati historia ya nchi yetu na siasa yake ya kuthamini UTU na HAKI ilivyokuwa. Nane, wengi wao si waoga pale wanapokuwa wanadai haki zao. Tisa, wengi wao wamekulia katika familia zenye hali ngumu ya maisha inayozungukwa na umaskini uliokithiri na magonjwa katika mitaa ya miji yetu na vijiji vyetu. Kumi, wengi wao wana afya zilizodhoofika kutokana na kutokupata lishe ya kutosha na matibabu ya uhakika lakini wanafanya kazi ngumu sana tena kwa muda mrefu na kulipwa ujira mdogo.

Mtu anaweza kuwadharau vijana hawa kwamba kwa kuwa wengi wao si wasomi na wana dhiki, basi ni rahisi kuwadanganya au kuwatisha wakanyamaza kwa dhana kwamba: hawazijui haki zao za msingi; hawajui mfumo wa uchumi wa dunia unavyofanya kazi na unavyowaathiri; hawajui athari za kupanda kwa bei ya mafuta; hawajui athari za mfumuko wa bei; na hawajui maana halisi ya demokrasia kwani zipo tuhuma kwamba wengi wao hawapigi kura au wanauza shahada zao. Na kwamba wanachojua ni kupata mlo wao na siku inapita. Lakini si hivyo hata kidogo.

Itaendelea

No comments: