Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Wednesday, January 9, 2013

Amani Millanga ahoji ukodishwaji wa maeneo makubwa ya ardhi kwa wawekezaji (sehemu ya kwanza kati ya sehemu tatu)


Katika makala yake hii ambayo nitaitoa katika sehemu tatu, Amani Millanga anahoji ukodishaji wa maeneo makubwa ya ardhi kwa wawekezaji na, kwa maoni yake, utaratibu huu unaturejesha kwenye ukoloni.
 ******************************************

Mali ya Taifa (sehemu ya kwanza)
Na Amani Millanga

Kwa mujibu wa takwimu za serikali, Tanzania inazo hekta 44 milioni za ardhi nzuri ya kilimo. Kwa sasa ni asilimia 23 tu ya ardhi hiyo inatumika kwa kilimo, ambayo ni sawa na hekta 10,120,000.  Hii ina maana kwamba tuna ziada ya hekta 33,880,000 (yaani hekta 44,000,000 kutoa hekta 10,120,000). Ziada hii ya ardhi ambayo haitumiki kwa lolote inaonekana ni kubwa sana. Hoja iliyoko mezani ni kuikodisha ardhi kwa wakulima wakubwa wa kigeni kwa ajili kilimo cha mashamba makubwa ili serikali na wananchi wanufaike na ardhi hii ambayo “haizalishi”.

Zinatolewa hoja kwamba wakulima wa kigeni wataleta teknolojia ya kisasa na mitaji mikubwa itakayohuisha kilimo na kutoa ajira kwa Watanzania. Kwamba “kupitia ukodishaji wa ardhi kwa wageni Tanzania itafanya mapinduzi makubwa ya kijani na hatimaye kupunguza umaskini”.

Ni hoja tamu, na zimeongeza kasi zaidi katika ukodishaji ardhi ili “tunufaike na kilimo cha kibiashara” ambacho kimsingi kipo tokea tupate uhuru. Zinatolewa hoja kwamba “Watanzania wasiwe na wasiwasi kwani ardhi ni mali ya taifa kwa mujibu wa Katiba na sheria.” Kwamba “mwekezaji atakodishwa ardhi kwa muda wa miaka 33, 66 au 99 na baada ya hapo ardhi itarejeshwa serikalini.” Hivyo basi “tuwapokee wakodishaji ardhi kwa mikono miwili kwani wanaleta neema.”

Hoja hizi hazina mashiko kwani zinahalalisha  kurejeshwa kwa ukoloni kwa mgongo laini wa ukodishaji ardhi jambo ambalo ni hatari sana kwa Tanzania ya leo na kesho na nitaeleza kwa nini.

Ukoloni unazo sura nyingi sana na mbinu kila aina za kuliteka taifa. Ukodishaji ardhi ni njia mojawapo ya kuukaribisha ukoloni mpya wa kutawaliwa na makampuni ya kibeberu. Ukisema hili wanajibu kwamba “hizo ni fikira za kale -Tanzania ni nchi huru.”

Lakini ukweli unabaki pale pale kwamba taifa-nchi (nation-state) ni ardhi. Hivi taifa-nchi linakaa wapi? Unapoikodisha ardhi kwa miaka 99 ina maana umeifanya ardhi hiyo kuwa ni koloni kwa miaka 99. Wajerumani na Waingereza walitutawala jumla ya miaka 77. Katika miaka 99 na nguvu ya pesa, mlowezi atafanya atakavyo. Na kwa kufanya hivi atakavyo Watanzania watageuzwa watumwa ndani ya nchi yao. Watanyanyaswa na kupigwa viboko. Tunayashuhudia haya yakifayika katika migodi ya dhahabu hadi Watanzania kuuwawa. Na katika Tanzania inayokumbatia rushwa na ufisadi mwekezaji anakingiwa kifua.

Je Mtanzania kibarua katika shamba la mlowezi atapata haki yake? Zipo taarifa nyingi kwamba kwa kutumia rushwa wageni wanapewa ardhi bwerere. Na kwa mchakato uliopo wa uraia wa nchi mbili (kama utapitishwa) katika siku si nyingi walowezi watapewa uraia na Tanzania ya kesho itageuka kuwa Zimbabwe ya sasa. Watanzania wataidai ardhi yao na walowezi wataiweka Tanzania katika msukosuko mkubwa. 

Taarifa zinazohusiana na hizi:
http://muhunda.blogspot.com/2010/07/kaburi-la-mbaguzi-nambari-wani-cecil.html

No comments: