Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Tuesday, January 29, 2013

Amani Millanga ahoji ukodishwaji wa maeneo makubwa ya ardhi kwa wawekezaji (sehemu ya pili kati ya sehemu tatu)


Katika sehemu ya pili ya makala yake hii ambayo nitaitoa katika sehemu tatu, Amani Millanga anahoji ukodishaji wa maeneo makubwa ya ardhi kwa wawekezaji na, kwa maoni yake, utaratibu huu unaturejesha kwenye ukoloni.
**********************************************************
Mali ya Taifa (sehemu ya pili)

Na Amani Millanga

Hoja ya pili kwamba “ardhi bado ipo” ni hoja ambayo inatolewa bila kuangalia kwa mapana na kina athari za ukodishaji ardhi kwa wageni. Mwaka 1961 idadi ya watu ilikuwa ni milioni kumi. Miaka 50 baadaye Tanzania ilikuwa na watu milioni 45. Hii ina maana kwamba idadi ya watu imeongezeka mara 4.5 toka milioni kumi hadi milioni 45 mwaka 2011.

Kwa msingi wa hesabu hii ina maana kwamba katika miaka 50 ijayo  (mwaka 2061) Tanzania itakuwa na watu milioni 45 x 4.5 = watu milioni 202.5. Je watu hawa wataishi wapi? Watajimudu vipi? Watapata wapi ardhi ilhali sehemu kubwa ya ardhi yetu itakuwa imekodishwa kwa wageni kwa miaka 99?

Hapo ina maana kwamba utakuwa na miaka 49 ya wawekezaji kumaliza muda wao. Katika hii miaka 49 (yaani mwaka 2110) idadi ya Watanzania itakuwa imeongezeka tena mara 4.5 (tukitumia msingi wa hesabu yetu wa ongezeko la watu wa mara 4.5) kwa maana kwamba watu milioni 202.5 x 4.5 = Tanzania itakuwa watu milioni 911.25 Hadi idadi ya watu inafikia kiwango hiki cha milioni 202.5 katika miaka 50 ijayo (mwaka 2061) au milioni 911.25 katika miaka 99 ijayo (mwaka 2110) tufahamu kwamba itakuwepo vita kali sana ya wananchi kuidai ardhi yao. Wengi watakufa bure kwa sababu ya maamuzi yasiyo ya kizalendo yanayotolewa hivi sasa ya kukodisha ardhi.

Mtu anaweza kusema ni jambo ambalo haliingii akilini kwamba Tanzania katika miaka 99 ijayo itakuwa na watu milioni 911.25. Lakini hili ni jambo ambalo linawezekana tukidurusu historia ya ongezeko la watu duniani. Ukiziangalia takwimu za ongezeko la idadi ya watu duniani katika miaka 2000 iliyopita utaona kwamba ongezeko kubwa la watu limekuwepo katika miaka 200 tu iliyopita. Mwaka 1800 dunia ilikadiriwa kuwa na idadi ya watu bilioni moja na mwaka 1900 idadi ya watu iliongezeka na kufikia bilioni moja na nusu. Tokea mwaka 1800 hadi mwaka 2000 idadi ya watu iliongezeka mara sita kufikia watu bilioni 6.1. 

Katika kipindi cha miaka 12 tu yaani mwaka 2000 hadi mwaka 2012, idadi ya watu duniani imeongezeka kwa kasi kubwa sana na imefikia watu zaidi ya bilioni 7.1 kwa mujibu wa tovuti http://www.worldometers.info/world-population/. Umoja wa Mataifa unakadiria idadi ya watu itakuwa bilioni 9 ifikapo mwaka 2050 na ongezeko kubwa la watu liko Afrika, kusini mwa Jangwa la Sahara, ambayo itakuwa na watu bilioni 2.756 mwaka 2050, likiwa ni ongezeko la watu bilioni 1.9 kutoka watu milioni 856 mwaka 2010 (ongezeko la watu zaidi ya mara mbili katika miaka 40) na 39% ya watu wenye umri kati ya miaka 15 hadi 24 duniani watakuwa Waafrika ifikapo mwaka 2100 kutoka 14% mwaka 2010.

Kwa hiyo upo ushahidi wa kutosha kwamba katika miaka 50 ijayo Tanzania itakuwa na watu milioni 202.5. Ardhi haiongezeki. Sasa katika hizo hekta milioni 44 tulizonazo ambazo kwa idadi ya watu ya milioni 45 ya mwaka 2011 ni sawa na hekta 0.977 kwa kila Mtanzania (kwa maana ya hekta milioni 44 gawa kwa watu milioni 45). Je hamuoni kwamba wastani huo wa ardhi kwa kila mtanzania utakuwa umeshuka sana katika miaka 50 ijayo?

Hesabu hii itatupa mwanga: hekta milioni 44 gawa kwa watu milioni 202.5 utapata hekta 0.217 kwa kila mtanzania. Je katika kasi hii ya kukodisha ardhi kwa wageni wastani huu wa hekta 0.217 utakuwepo kwa kila mtanzania? Ardhi itapatikana wapi? Bila shaka vijana watasimama kuidai ardhi tena kwa mabavu.

Ni ukweli usio na shaka kwamba idadi ya watu wanaohama vijijini kwenda mijini inaongezeka lakini hii haina maana kwamba katika miaka 50 ijayo 80% ya Watanzania itakuwa inaishi mijini na 20% itakuwa inaishi vijijini. Katika miaka 50 iliyopita yamekuwepo mabadiliko madogo sana ya watu kuhamia mijini ingawa kasi ya kuhamia mijini inaongezeka lakini bado 80% na huenda hata zaidi wanaishi vijijini hivi sasa. Kama hali itaendelea kuwa hivi, basi katika kujenga taswira ya hali ya mambo itavyokuwa tunaweza kukadiria kwamba 50% ya Watanzania watakuwa wanaishi mijini mwaka 2061. Hii ina maana kwamba watu milioni 202.5 gawa kwa mbili utapata idadi ya watu 101.25 watakuwa bado wanaishi vijijini wakitegemea kilimo kama ajira yao kuu.

Je tutakuwa na ardhi ya kukidhi mahitaji ya watu hawa kwa mnasaba wa kasi ya ukodishaji ardhi iliyopo? Hapa ndipo unahitajika umakini wa hali ya juu sana katika kuangalia hatima ya Tanzania na watu wake. Kwa mtizamo uliopo sasa Tanzania ya 2061 itakuwa na mgogoro mkubwa sana wa ardhi zaidi ya ule wa Zimbabwe. 

Taarifa zinazohusiana na hizi:
http://muhunda.blogspot.com/2010/07/kaburi-la-mbaguzi-nambari-wani-cecil.html

No comments: