Saturday, December 13, 2014
Mwisho wa kampeni Butiama za uchaguzi wa serikali za mitaa
Friday, December 12, 2014
Mabondia na unga (sehemu ya tatu ya awamu tatu)
![]() |
Ibrahim Kamwe |
“Siwezi acha dili la pesa kama hili wakati jina langu kubwa kila kona linatajwa mitaani na vyombo vya habari lakini mimi binafsi nauli ya daladala sina. Siku ya tatu leo nakula mlo mmoja kwa siku, watoto hawapo katika hali nzuri, mazoezi yenyewe sifanyi kwa raha nafikiria nitapata wapi mshiko. Leo unaniletea ishu ya pesa niikatae si nitakuwa kichaa?”
“Wadau wenzangu wa ngumi ,wapambe wao, na walio karibu na sisi mabondia wana nguo za bei kubwa wanapendeza, wana magari. Ukiangalia mimi bondia ndiye mtendaji wao mkuu nipo ovyo sina kitu mfukoni wala tumboni, madeni kibao yaani majanga matupu.”
Sunday, December 7, 2014
Mabondia na unga (sehemu ya pili ya awamu tatu)
%2B(640x480).jpg)
Tuesday, November 25, 2014
Mabondia na unga (sehemu ya kwanza ya awamu tatu)
![]() |
Ibrahim Kamwe |
Friday, November 21, 2014
Wazanaki na dini
Mwalimu Jack Nyamwaga, kulia, akiongea na Dk. Thomas Molony, mtafiti na mhadhiri kutoka Chuo Kikuu cha Edinburgh. |
"Wamisionari wa kwanza waliofika hapa Butiama walikuwa Waprotestanti. Wakati huo Roman Catholic walikuwa wameshafika Nyegina [karibu na Musoma]. Hata hivyo Waprotestanti hawakuingia ndani sana kueneza dini miongoni mwa Wazanaki.
Halafu wakaja Seventh Day Adventist (SDA) na wakasema kuwa masharti ya madhehebu yao ni pamoja na wanaume kuoa mwanamke mmoja tu na waumini wao kukatazwa kunywa pombe. Hayo masharti hayakuwa rahisi kukubaliwa na Wazanaki ambao siyo tu walikuwa na desturi ya kuoa mke zaidi ya mmoja, lakini walikuwa na asili ya kunywa pombe na hata kuitumia katika mitambiko. Mwaka 1938 SDA wakahamia Busegwe [kijiji cha jirani] ambako kulikuwa na mchanganyiko wa makabila mengine zaidi ya Wazanaki.
Halafu wakaja Mennonite na wao pia walikuwa na marufuku ya kunywa pombe. Hawa wakashauriwa kwenda Bumangi [kijiji cha jirani]. Mtemi Nyerere Burito alipoambiwa kuwa anapaswa kuwa na mke mmoja akauliza: "Hawa wake zangu 13 nitawapeleka wapi?"
Walipofika wamisionari wa madhehebu ya Roman Catholic Wazanaki wa Butiama wakapendekeza kanisa lao lijengwe Magorombe, kijiji kilicho mbali na Butiama kwenye ardhi inayotitia ikitarajiwa kuwa kanisa likijengwa hapo lintaanguka. Mmisionari aliyekwenda huko alipanda mikaratusi iliyofyonza maji na akajenga kanisa imara.
Waislamu walipokuja nao walikuwa na marufuku ya kunywa pombe. Wao wakashauriwa waende Nyamuswa kwa Mtemi Makongoro Matutu, ambaye alikuwa rafiki wa Mtemi Edward Wanzagi. Yeye aliwapokea na akasilimu.
Kizingiti kikubwa cha kuwahi kuenea kwa dini miongoni mwa Wazanaki wa Butiama ilikuwa suala la marufuku ya kuoa mke zaidi ya mmoja na marufuku ya kunywa pombe."
Tuesday, October 14, 2014
Huduma kwa mteja mkoani Mara
Baada ya muda kondakta alimsogelea abiria aliyekaa karibu yangu na mazungumzo yakawa hivi:
Konda: Nipe hizo hela!
Abiria: Ngapi?
Konda: Kwani hujui?!?!?!
Baada ya muda abiria akatoa nauli kamili halafu wakaendelea:
Abiria: Nifahamishe nauli sahihi kwa ustaarabu.
Konda: Kwani wewe nani? Usiniletee mambo yenu ya Kikurya!
Sehemu nyingine Tanzania watu wangekunjiana ngumi. Mkoa wa Mara ni mazungumzo ya kawaida tu kati ya mtoa huduma na mteja wake.
Saturday, October 11, 2014
Uongo wa waandishi wa habari: sikuikataa noti ya Mwalimu Nyerere
Mgeni rasmi alikuwa Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Juma Reli. Katika kumalizia neno la shukurani niliomba uongozi wa Benki Kuu kuangalia uwezekano wa kubadilisha picha ya Mwalimu Julius Nyerere waliyotumia kwenye noti ya shilingi elfu moja. Kwa maoni yangu ile picha haifanani kwa karibu sana na sura ya Mwalimu Nyerere. Sikuamuru wala sikuikataa noti, ila niliomba tena kwa unyenyekevu mkubwa. Lakini ukifuatilia habari zilizoandikwa juu ya ombi langu utapata picha tofauti.
ITV walifungua dimba la upotoshaji kwa kusema kuwa nilitamka kuwa picha ile inamdhalilisha Mwalimu (au familia yake?). Huu ni uongo wa mchana na siyo kweli kabisa kuwa nilitumia neno “kudhalilisha.” Nikisoma baadhi ya vichwa vya habari vya baadhi ya magazeti yaliyoandika habari hizo navyo vinapotosha.
The Citizen wameandika kuwa nimeitaka serikali kuiondoa hiyo noti. Huo nao ni uongo mwingine. Gazeti lingine limeandika kuwa familia ya Mwalimu Nyerere imeikataa noti ya shilingi elfu moja. Ni uongo juu ya uongo. Naamini orodha ni ndefu zaidi lakini sijapata fursa ya kufuatilia kwa muda mrefu.
Sikusema kuwa familia imeikataa noti. Nilichosema ni hayo niliyoandika mwanzo wa taarifa hii.
Ninayo bahati mbaya ya kutungiwa maneno ambayo sijayasema kwenye taarifa zinazonihusu. Mwanzo nilikuwa napuuzia nikiamini kuwa tatizo hili litaisha lakini kila muda unavyozidi kupita naona hali ni ile ile.
Nimekuwa nawashauri waandishi wa habari waache kutumia mtindo wa kuandika “Madaraka alisema….” na badala yake watumie maneno yangu mwenyewe na kuandika habari kwa njia ya kuninukuu. Naamini njia hii inapunguza kuweka maneno ambayo hayakutamkwa.
Naanza kufikia kuamini kuwa maneno yangu mwenyewe huwa hayauzi magazeti na inalazimika mwandishi kuweka chumvi kidogo ili magazeti mengi zaidi yatoke. Kama hii ni kweli basi hali hii inadhirihisha kuwa sifa ya weledi kwenye sekta ya habari inaanguka, na inahitaji kufanyika jitihada ya kuirekebisha.
Saturday, October 4, 2014
Hiki ni kielelezo cha utu uzima
Leo nimetembelea kituo cha polisi kutoa taarifa ya kupotelewa vitu vyangu. Nimegundua umri umepiga hatua kubwa.
Afisa aliyechukuwa maelezo yangu aliponiuliza umri wangu nilijibu: 54.
Akauliza: miaka? Nikamjibu: ndiyo, miaka. Au naonekana nimezidisha?
Nilitamani kumwambia: Hapana. Maandazi.
Ningejibu hivyo labda saa hizi ningekuwa rumande kwa kosa la kudhalilisha Jeshi la Polisi.
Lakini nilitambua kuwa kwake yule afisa miaka 54 haikuwa kidogo.
Tuesday, September 30, 2014
Mila na tamaduni: Watanzania ni wakarimu (sehemu ya tano)
Jiunge nami kwenye sehemu ya tano na ya mwisho ya msafara huu...
Agosti 5
Ni zaidi ya kilomita 40 toka Bunda kuelekea Butiama na safari inaenda vizuri tu nikiwa nimejaa shauku ya kumaliza hili zoezi.
Hata hivyo adui mkubwa wa masafa marefu kwa baiskeli ni njaa na suala la kupata chakula cha mchana ni muhimu kabisa ili kuweza kuendesha baiskeli kwa saa zaidi ya tano kwa siku ya leo. Naenda kwa wastani wa kilomita kama 11 kwa saa. Kwa hiyo nalazimika kusimama tena Nyamisisi kukamilisha mlo wangu wa mchana kabla ya kuendeela na safari hadi Butiama. Nyamisisi ni sehemu ambayo siyo mashuhuri tu kwa matunda ila ina sifa ya kuwepo wataalamu juu ya taarifa za wanasoka na wasanii maarufu.
Mimi namalizia ziara yangu ya kilomita zaidi ya 170 lakini nahisi nahitaji mapumziko baada ya safari yangu ya kutoka Ukerewe mpaka Butiama.
Saturday, September 27, 2014
Mila na tamaduni: Watanzania ni wakarimu (sehemu ya nne)
Jiunge nami kwenye sehemu ya nne ya msafara huu...
Agosti 4
Sijaendesha baiskeli kwa masafa marefu kwa muda mrefu kwa hiyo leo naanza kusikia mwili unapanga njama za kuanzisha mgomo wa kutoendelea na safari. Hata hivyo hii ni njia ambayo nimeshawahi kupita kwa baiskeli kuelekea Ukerewe na muda si mrefu najikuta nimefika kwenye kiwanda cha kuchambua pamba cha Bulamba.
Inanipa matumaini kuwa safari ya kwenda Bunda imepungua kwa kiasi kikubwa. Nilipokaribia Bunda nilikimbiliwa na mtoto wa miaka sita hivi akaniomba pesa. Huwa nawakanya watoto wasiwe na tabia ya kuomba pesa kwa wapita njia ili kulinda usalama wao. Hata hivyo kwa leo ninakiuka taratibu zangu mwenyewe na kufanya naye majadiliano yafuatayo:
"Unataka pesa za nini?"
"Za kununulia pipi."
Hapo nilifungua mfuko wangu na kutoa kipande cha chokoleti kilichochanganywa na karanga. Alipofungua kifungio naamini ile taswira ya alichokiona ilimfanya asite kidogo akaniuliza:
"Hiki ni nini?"
"Kula tu ni tamu sana."
Alivyoonja alicheka ghafla akiwa na furaha isiyo na kifani halafu akaniambia: "Uwe unapita hapa kila siku!"
![]() |
Alipofungua chokoleti alisita kuila. |
Taarifa inayofuata: Naagiza chipsi mayai
sehemu ya tatu ya makala hii
Wednesday, September 24, 2014
Mila na tamaduni: Watanzania ni wakarimu (sehemu ya tatu)
Jiunge nami kwenye sehemu ya tatu ya msafara huu...
Agosti 3
Mapema asubuhi nilianza safari yangu ya baiskeli ya kurudi Butiama kwa kuelekea kwenye kivuko cha Rugezi na ni leo ndiyo iliyodhihirisha kwangu kuwa Watanzania bado watu wakarimu. Nilipovuka upande wa pili kwenye mji mdogo wa Kisorya, nilisimama kwa muda kwenye mgahawa kuongeza mlo wa asubuhi wa chapati mbili na chai, ingawa ilikuwa inakaribia saa tano asubuhi.
Nikiwa na uhakika kidogo wa kuendelea na safari yangu mpaka njaa itakaponilazimisha kusimama na kula chakula cha mchana, nilianza safari ya kuelekea Kibara. Hata hivyo haikuchukuwa muda nikalazimika kusimama kutafuta chakula kwenye kijiji kilicho njiani.
Pembeni yangu niliona jengo linafanana na mgahawa. Alitokeza binti mmoja na mazungumzo yakawa hivi:
"Una chakula?"
"Ndiyo"
"Chakula gani?"
"Chai na chapati"
"Mimi nimeulizia chakula, siyo chai."
"Samahani, nina chai na chapati tu."
Niliendelea kudadisi:
"Kwani wewe mchana huli chakula?"
"Nitakula.
"Unapika nini?"
"Ugali na dagaa."
"Basi ongeza na cha kwangu halafu nitakulipa."
Akakubali. Chakula kilipokuwa tayari akanikaribisha kwenye mgahawa wake, akanipa maji ninawe na yeye akanawa tukakaa pamoja kula.
![]() |
Niliegesha usafiri wangu, nikapiga picha, halafu nikaingia kusubiri chakula. |
Nikijiandaa kuondoka nilimuuliza nimlipe kiasi gani kwa kile chakula. Alinishangaa na kuniambia: "Wewe si nilikwambia kuwa hakuna tatizo? Pesa za nini?"
Nikabaki hoi. Lakini nilifungua mfuko wa baiskeli yangu na kutoa pakiti ya biskuti nikampa na kusema ni zawadi kwa watoto wake. Alifurahi sana na kuniuliza bei ya biskuti zile. Nilimwambia shilingi elfu tatu nikapanda basikeli na kuanza safari ya kuelekea Kibara.
Vijijini wema huu bado upo. Sina hakika kama mijini hali imebakia hivi.
Taarifa ijayo: Hiki ni nini?
Sehemu ya pili ya makala hii
Saturday, September 6, 2014
Mila na tamaduni: Watanzania ni wakarimu (sehemu ya pili)
Jiunge nami kwenye sehemu ya pili ya msafara huu...
Agosti 2
Tulitembelea makazi ya kwanza walipofikia Wakristu wa kwanza kutua kwenye kisiwa cha Ukerewe zaidi ya miaka 100 iliyopita. Hakuna maelezo mengi sana kuhusu eneo hili ila simulizi za mauaji yaliyofanyika hapo dhidi ya baadhi ya wageni hao na mtawala wa eneo hilo wa wakati huo. Ni eneo ambalo liko kwenye kilima chenye mwinuko mkubwa unaowezesha kuona umbali mkubwa juu ya Ziwa Viktoria. Mwenyeji wangu aliniambia kuwa nyakati ambapo hakuna ukungu yawezekana kuona ndege zikipaa na kutua kwenye uwanja wa ndege wa Mwanza.
![]() |
Ukerewe ni kisiwa chenye mandhari za kuvutia na visiwa vingi vinavyokizunguka. Upande wa kulia wa picha kinaonekana kisiwa cha Bwiru. |
Taarifa ijayo: Watanzania ni watu wakarimu
sehemu ya kwanza ya makala hii
sehemu ya tatu ya makala hii
Saturday, August 23, 2014
Mila na Tamaduni: Watanzania ni wakarimu (sehemu ya kwanza)
Jiunge nami kwenye msafara huu...
Agosti 1
Safari yangu ilianzia Mwanza kwa kuvuka na meli iitwayo MV Clarias kuelekea Nansio, Ukerewe. Huko nilipokelewa na muongozaji wageni maarufu wa kisiwa cha Ukerewe, Tumaini Yohana Ladislaus ambaye ni mmiliki wa Tumaini Tours.
![]() |
Muda mchache kabla ya kuanza safari ya kuelekea Ukerewe kutokea Mwanza. |
![]() |
Muongozaji wageni akitoa maelezo ya picha mbili za Mtemi Michael Lukumbuzya. |
Inasemekana Ukerewe ndiyo eneo lenye mkusanyiko mkubwa zaidi kwa kilomita za mraba za wasomi wa shahada za uzamivu kuliko sehemu yoyote ile Tanzania, na pengine hata Afrika.
Itaendela na: Mjasiriamali wa Ukerewe
sehemu ya pili ya makala hii
Tuesday, July 29, 2014
Mwisho wa Tanzania siyo Kibaha
Nitatoa mifano. Jana nilitaka kukamilisha usajili wangu wa shahada mojawapo ya chuo kikuu kimojawapo cha Tanzania. Waliopitia zoezi hili wanafahamu kuwa maombi yote yanafanyika kwenye mtandao. Ukikwama wakati wa kujaza maombi zimetolewa namba za simu ambazo unaweza kupiga kupewa maelekezo. Nilikwama mapema kwa sababu nina stashahada ya nje ya nchi ambayo mchakato wa maombi hauitambui. Nilipiga simu hizo kwa muda mrefu lakini au hazipokelewi au haziko hewani.
Bahati nzuri nilipata namba nyingine ya Kamisheni ya Vyuo Vikuu (TCU) ambayo nilipiga na kuunganishwa na mama mmoja. Nilimueleza tatizo langu. Akaniambia kuwa TCU bado haijakamilisha tathmini ya shahada za nje na kwa hiyo nilipaswa kupeleka shahada yangu “ofisini” ili ihakikiwe.
Nilimwambia kuwa mimi niko Musoma. Akanijibu: “Sasa mimi nifanyeje?” Ilikuwa ni kama vile ananieleza: “Nani kakutuma kuishi bara?”
Sifahamu kama watu wanaopanga taratibu mbovu kama hizi wanatambua kuwa safari kutoka baadhi ya sehemu za Tanzania ni zaidi ya kilomita 1,000 hadi Dar es Salaam na inagharimu pesa. Hawa wanatoa majibu kama vile Watanzania wote milioni 45 wanaishi Dar. Naamini kuna makumi ya maelfu ya waombaji wa kusoma kwenye vyuo vikuu ambao hawako Dar. Kwanini inashindikana kuwepo mwakilishi wa Kanda ili mimi niliye Butiama nisilazimike, mathalani, kusafiri hadi Dar kuhakiki cheti changfu? Ingetosha kusafiri hadi Mwanza tu, ingawa wakati mwingine hata Mwanza pia naona ni mbali ambako ingewezekana kupanga muda maalumu wa kuonana na huyu mhakiki na gharama yake kujunuishwa kwenye gharama ya maombi. Ongezeko la gharama hii haitazidi gharama za kusafiri kwenda Dar.
Ukweli ni jukumu la serikali kuhakikisha kuwa raia wake wote wanapata huduma kwa haki na usawa ule ule. Ningekuwa na muda (na pesa) ningefungua kesi mahakamani kudai kukiukwa kwa haki zangu za msingi kama raia ambaye anastahili kupata huduma ile ile ya umma kama raia anayeishi Dar es Salaam.
Mfano mwingine, na hapa nasisitiza kwa nini nimesema kuwa hata Mwanza ni mbali, unahusu kampuni za simu. Kuna aina nyingi za matatizo ambayo yanaweza kumalizwa kwenye simu, lakini baadhi ya watoa huduma za kampuni za simu watakwambia unapaswa kwenda kwenye ofisi zao ili kutatua shida fulani.
Nagombana mara kadhaa na watoa huduma wa kampuni ya simu ya Voda. Watoa huduma wa Voda wanayo sentensi wanayopenda sana kutumia kumaliza tatizo: “Nenda Voda Shop.” Mimi kwenda Voda shop iliyo karibu ni kilomita 80 (kwenda na kurudi). Mimi nilifikiri maana ya kuwa na simu ni kupunguza ulazima wa kufunga safari zisizo za lazima, na kuongeza ufanisi katika kazi. Ukiniambia niende Voda Shop napoteza siku nzima ya kazi bila sababu ya msingi.
Halafu siku ukitoa takwimu kuwa una wateja milioni 10 na mimi pia utanihesbau katika usawa ule ule na mteja wa Dar es Salaam wakati mimi nalazimika kulipia gharama za ziada ili kutumia huduma yako?
Nasema haya siyo kwa kukosoa tu bila sababu ila kwa kutoa hoja kuwa kuna baadhi ya taratibu zinapaswa kupitiwa upya ili kutoa huduma sawa kwa mteja wa Butiama kama ambavyo anafaidika mteja wa Dar. Kuna ukweli kuwa foleni za Dar zinaweza kusababisha hata mkazi wa Dar kuona kuwa safari ya kwenda Voda Shop badi ni kero kwake. Kama hii ni kweli, basi hata yeye ana haki ya kulalamika.
Teknolojia ina manufaa ni na ingerahisisha sana shughuli za utawala na biashara nchini lakini bado ziko hitilafu nyingi za kurekebisha. La msingi ni kuwa Tanzania ni nchi kubwa na inahitaji mtazamo huo mpana kupanga mipango ya kuhudumia raia na wateja.
Saturday, July 26, 2014
Mada yangu ya leo: siyo kila aliye chumbani amelala usingizi
![]() |
Ofisini kwangu. |
Wednesday, July 16, 2014
Tujisahihishe
Kombe la Dunia la FIFA limeisha hivi karibuni na nilisikia (kwenye redio na runinga) na kuona kwenye maandishi, haswa kwenye mitandao ya jamii, matumizi yasiyo sahihi ya majina ya baadhi ya timu zilizoshiriki kwenye mashindano hayo.
"Ujerumani" iliandikwa "Ujeruman." Na kwa Kiingereza badala ya kuandika "Germany", baadhi ya watu waliandika "German." Tatizo hili la matumizi ya lugha lisichukuliwe kuwa ni kwa lugha au majina ya kigeni pekee. Jana nikiwa kwenye ndege nilisikia mfanyakazi wa ndani ya ndege akitutangazia abiria kuwa "tumetua kwenye uwanja wa ndege wa kimataifa wa Julius Nyerele." Huyo ni Mtanzania anashindwa kutamka "Nyerere." Na haikuwa mara yangu ya kwanza kusikia "Nyerere" kuitwa Nyerele." Kama ungeondoa muktadha ungefikiri alikuwa anazungumzia nyenyere.
Lakini jambo la kushangaza zaidi ni kuwa baada ya kutamka hivyo alianza kuongea kwa Kiingereza kutoa taarifa hiyo hiyo kwa abiria tuliokuwa ndani ya ndege, lakini alipoongea kwa Kiingereza alitamka "Nyerere" kwa usahihi.
![]() |
Nilipanda ndege ya shiriki hili. Safari ilikuwa nzuri, lakini lugha ilikuwa na walakini. |
Nawasilisha hoja.
Sunday, July 13, 2014
Wakati mwingine picha zinadanganya
Kushoto mwa picha hii (hapaonekani) kuna jengo kubwa lenye ofisi na maduka kwenye ghorofa za chini na nyumba za kuishi kwenye ghorofa za juu. Ni sehemu ambayo zamani waliishi Watanzania wa jamii ya Kiasia . Jengo lililojengwa hapo lilibadilisha kabisa taswira ya eneo hilo na liliongeza idadi ya majengo mapya ambayo yanachipuka Dar es Salaam kila kukicha. Majengo mengi ya zamani na ya kihistoria yanaendelea kubomolewa.
Lakini pamoja na mabadiliko makubwa yanayoendelea kutokea kwenye baadhi ya maeneo ya Dar es Salaam ninahisi kuwa picha hii haiakisi ukweli wa hali ilivyo katika eneo hilo. Ukweli ni kuwa picha hii inapamba zaidi hali halisi.
Nimeshapita kwenye eneo hili mara mia kadhaa lakini sijaona hali hiyo nzuri ambayo naiona kwenye picha hii. Kwa hakika teknolojia ya kamera imefanikiwa kupamba ukweli kwa sifa bandia.
Saturday, July 12, 2014
Wageni wa Butiama: Urmila Jhaveri
![]() |
Mama Urmila Jhaveri akiwa Butiama kwenye Makumbusho ya Mwalimu J.K. Nyerere. |
Wakati wa kudai uhuru wakati mume wake akiwa mmoja wa viongozi wa chama cha Waasia, Indian Association, kilichoshirikiana na kuunga mkono sera za Tanganyika African National Union (TANU), Urmila alishiriki kwenye harakati hizo akiwa mwanachama wa kitengo cha wanawake cha TANU ambacho kilijulikana kama TANU Women's Section.
Hivi karibuni amechapisha kitabu juu ya maisha yake kiitwacho Dancing with Destiny ambacho atakizindua tarehe 19 Julai 2014 jijini Dar es Salaam.
Itakuwa fursa nzuri kwa wote kukumbuka mchango muhimu wa makundi mbali mbali ya Watanzania kwenye harakati za kudai uhuru.
Sunday, May 18, 2014
Mwanza, juzi
Juzi nikiwa jijini Mwanza, mtu mmoja nisiyemfamu aliniomba pesa. Nilimjibu kuwa sikuwa na pesa za kumpa. Aliendelea kuniomba. Nilisisitiza sikuwa na pesa.
Akasema: "Du! Sasa mheshimiwa unaniacha na hali mbaya sana."
Mimi: "Vumilia. Leo huna, kesho utapata."
Yeye: "Tutafika kweli? Eti wanasema tusubiri mpaka mwaka 2025 ndiyo mambo yatakuwa mazuri kwetu sisi maskini? Tutakuwa bado tunaishi kweli?
Mimi: "Vumilia. Tutafika."
Niliondoka nikiwaza kuhusu matarajio ya raia mwenzangu kuhusiana na Visheni ya Maendeleo ya 2025 inayolenga kuifanya Tanzania kuwa nchi ya uchumi wa kati.
Ikifika tarehe 1 Januari 2026 na hali yake iko vile vile patachimbika.
Tuesday, May 13, 2014
Uandishi ni kazi kweli kweli!
Tatizo mojawapo linalonizuwia kuandika mara kwa mara ni kusafiri huku na kule kwa shughuli mbali mbali. Nimejenga mazowea ya kuandika nikiwa sehemu moja tu: nyumbani. Ninaposafiri sipati utulivu wa kutosha kuniwezesha kuandika vyema.
Hata hivyo naweka kando hivyo visingizio na natarajia kuanza tena kuhuisha blogu hii kwa kuweka habari hapa na maoni yangu ya masuala kadha wa kadha.