Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Tuesday, September 28, 2010

Kisa cha kuacha kuvuta sigara: safari yangu ya kupanda Mlima Kilimanjaro (makala ya sita kati ya kumi)

Alhamisi 21 Agosti 2008
Tulianza na mpando wa taratibu kutoka Kambi ya Shira (iliyopo mita 3,400 kutoka usawa wa bahari) na tutafika na kupita Lava Tower (iliyopo mita 4,600 juu ya usawa wa bahari). Wenye nishati ya ziada wanaweza kukwea Lava Tower ambayo nilikadiria ina urefu wa mita 500 juu ya njia ya kuelekea Kambi ya Barranco, kikomo cha safari yetu kwa siku ya leo. Tulikutana na kundi la vijana wa Kijerumani wakiteremka toka Lava Tower.
Taswira ya Mlima Kilimanjaro kutoka upande wake wa mashariki

Ilikuwa ni mteremko mmoja mrefu na wa kuchosha kutoka Lava Tower kuelekea Barranco (iliyopo mita 3,950 kutoka usawa wa bahari) ambako nilikutana na wahifadhi wawili, wote wakiwa wanamazingira, na ambao walionyesha shauku kubwa kujua kusudio la msafara wangu. Kwanini nilikuwa napanda Mlima Kilimanjaro? Nikifanikiwa kufika kileleni nitapanda milima mingine, kama Meru, au Oldoinyo Lengai? Mmojawapo aliniambia kuwa yeye ni Mmasai na aliniambia kuwa ana jina refu kama langu. Aliniambia kuwa mwenzie ni kutoka wa kabila la Wairaqi.

Jioni wakati wa tathmini ya siku nilihisi kama Yahoo alihisi kuwa ninapata shida kupanda mlima baada ya yeye kushauri kuwa mimi nitumie njia tofauti ya kuteremka badala ya ile njia ambayo Jose' alipendekeza na ambayo Le alikuwa na shauku ya kuitumia. Yahoo alisema pengine itabidi nichukue njia ya moja kwa moja kuelekea lango la Mweka badala ya kutumia njia ya Machame iliyopendekezwa na Jose'.

Nilikubali. Kiongozi wa msafara ndiyo hufanya maamuzi yote ya mwisho kwa kuzingatia tathmini yake kwa kila moja na ingawa sikujihisi kuwa nimefikia kikomo cha uwezo wangu, sikuwa na nguvu ya kutosha kuanza kubishana nae baada ya kutembea kwa siku nzima. Labda nitakuwa na maoni tofauti kesho asubuhi.

Ijumaa 22 Agisti 2008
Nimeamka nikijisikia na hali nzuri zaidi leo. Tulianza kutembea tukiwa mbele ya jabali ambalo nakisia lilikuwa na urefu wa mita 750. Hii, Pius alituambia, ndiyo inaitwa "Mpando wa Kifungua Kinywa" Kutokana na ugumu wa mpando huu alisema mara tutakapofika kule juu tutajihisi kuwa tunahitaji kupata tena kifungua kinywa. Alituambia kuwa wakweaji wengi huwa wakifika hapa hukata tamaa na kuteremka kurudi Moshi. Na cha kustaajabisha ni kuwa hii ni njia ambayo mwasisi mmoja aliamua kuwa, kama ambavyo Le anapenda sana kutamka, inawezekana kupita.

Pius alituambia kuwa alikaribia kuacha kazi yake kama muongozaji wa misafara ya kupanda Mlima Kilimanjaro alipoambiwa kwa mara ya kwanza kuwa Mpando wa Kifungua Kinywa ndiyo njia pekee ya kuelekea kileleni kutokea hapa. Katikati ya kupambana na Mpando wa Kifungua Kinywa tulifika eneo linaloitwa Busu la Mwamba ambapo unakumbatia uso wa jabali ili kujinusuru kuanguka na kuepuka mauti.

Sehemu ya mwisho tulipokaribia Kambi ya Karanga (iliyopo mita 3,963 juu ya usawa wa bahari) ilikuwa ni mpando mwingine mrefu na wa kuchosha. Kutokea Karanga tuliweza kuuona Mlima Kilimanjaro kama ambavyo wengi tumozoea kuuona. Kadiri tunavyozidi kuelekea mashariki, tunapata taswira tofauti ya mlima kila siku. Kabla ya kulala, nilikunywa mojawapo ya kopo moja ya Red Bull na nilisumbuka sana karibu usiku mzima. Asubuhi Pius alituambia kuwa yawezekana kuwa usiku nyuzi joto zilishuka chini ya kiwango cha kugandisha maji.

Makala ijayo: Athari za Red Bull


Makala zinazohusiana na hii:

No comments: