Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Monday, September 27, 2010

Kisa cha kuacha kuvuta sigara: safari yangu ya kupanda Mlima Kilimanjaro (makala ya tano kati ya kumi)

Jumanne 19 Agosti 2008
Tulipanda gari kutoka Moshi tukielekea upande wa Arusha halafu tukakatiza kuelekea Machame kwenda eneo la kuanzia safari yetu. Nilisikitika kuwa mawingu yalituzuwia kuuona vizuri Mlima Kilimanjaro. Wahifadhi 

Le, akiwa nje ya mahema yetu ya kulala
Kilimanjaro walikagua vifaa vya wasindikizaji wetu kwenye lango la Londorossi. Kundi letu lilikuwa na wabeba mizigo 9, Yahoo, na msaidizi wake.

Wabeba mizigo wa Mlima Kilimanjaro wanafanya kazi katika mazingira magumu na wanabeba mizigo mizito  ya mahema, mifuko ya kulalia, chakula, na maji ili kutuwezesha sisi kufika kilele cha Uhuru katika mazingira ya starehe. Hata hivyo, mazingira yao magumu yanasababisha athari siyo tu kwa afya zao ila na hata kwa maisha yao. Tulisimuliwa hadithi ya wabeba mizigo waliokuta mauti kutokana na kutokuwa na mavazi muafaka ya kuhimili baridi.

Mlima Kilimanjaro unaonekana kwa mara ya kwanza baada ya kutoka eneo la msitu.
Tuliteremshwa mwisho wa barabara mbaya, aina ya barabara ambayo inapitika na magari yaliyotengenezwa mahususi kukabili barabara za aina hiyo. Tulianza na mwendo wa kutembea wa kasi ndogo kabisa ambayo sijawahi kuona tangu nianze kujifunza kutembea. Yahoo, akiwa mbele yetu, ndiye aliyepanga hiyo kasi ambayo tuliendelea nayo kwa muda wa saa nne. Katika siku zilizofuata, tulivyoanza kupambana na maeneo magumu ya mpando nilielewa umuhimu wa kasi ile ndogo ambayo inasaidia sana kupiga hatua ya wastani wakati wote. Usiku wa kwanza tulilala kambi ya Big Tree, tukiwa kati ya mbega kadhaa.

Tatizo kuu la usiku wa kwanza ni kulala mapema. Kujaribu kulala saa mbili usiku ilikuwa mateso, lakini kwa usiku wa kwanza tu. Katika siku saba zilizofuata nilikuwa na uchovu mkubwa sana kutokana na kutembea kila siku kiasi ambapo ningeweza kulala hata saa 6 mchana. Mtihani mwingine ulikuwa kulala ndani ya mfuko wa kulalia. Jaribu kufikiria kulala ndani ya zulia lililoviringishwa na uweze kupata usingizi. Wakati tukikaribia kumaliza safari yetu Le alipendekeza kuwa nitafute mfuko wa kulalia toka Australia ambao unatengenezwa na nafasi kubwa zaidi kwa mtumiaji.

Niliona ajabu sana kuwa wakati nahangaika kutafuta usingizi nilisikia jamaa anakoroma kutoka hema la jirani yangu.

Jumatano 20 Agosti 2008
Leo, naamini nilifanikiwa kutembea kwa mwendo mrefu kuliko yote ambayo nimewahi kutembea. Siamini hata Neslon Mandela amewahi kutembea kwa mwendo mrefu zaidi. Kuachilia saa moja ya mlo wa mchana katika kambi ya Shira, tulitembea kuanzia saa 1 asubuhi mpaka karibia saa 2 usiku, tukiwa tumepambanishwa na mpando mmoja mkali baada ya kumaliza eneo la msitu na kuelekea kwenye Uwanda wa Shira.

Sehemu ngumu kuliko yote kwa leo ilikuwa baada ya machweo wakati Yahoo alipotuonyesha mwanga uliyokuwa mbali juu ya safu ya kilima na akasema ndiyo kikomo cha safari yetu kwa leo. Ilikuwa ni mpando mgumu ambao ulikuwa kama hauelekei kwisha. Ilifika wakati nilimpa Yahoo mfuko wangu wa mgongoni na nilimalizia safari bila mzigo. Baada ya hapa nilianza kuwa na hofu kuwa pengine sitaweza kufika kileleni.

Ingawa sikusumbuliwa na baridi nilihisi kupungukiwa pumzi, na Yahoo aliniambia kuwa hizo zilikuwa dalili za ugonjwa wa nyanda za juu unaosababishwa na upungufu wa oksijeni. Alisema baadhi ya dalili za mgonjwa mahututi ni pamoja na rangi ya ulimi kugeuka kijani.

Makala ijayo: Tunaelekea kambi ya Barranco na "mpando wa kifungua kinywa".


Makala zinazohusiana na hii:

No comments: