Tembelea Butiama

Tembelea Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Karibu Butiama / Welcome to Butiama

Kurasa Muhimu

Sunday, September 26, 2010

Kikwete ahutubia Musoma Mjini kwenye kampeni za uchaguzi

Jana, mgombea urais wa Chama cha Mapinduzi (CCM) na Rais wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete, alihutubia umati wa wananchi wa Musoma Mjini katika ratiba yake ya kampeni ya kuwania kiti cha urais katika uchaguzi mkuu wa mwezi Oktoba mwaka huu.


Mgombea urais wa CCM akihutubia mkutano wa kampeni za uchaguzi kwenye kiwanja cha Shule ya Msingi Mukendo jana mjini Musoma 
Katika hotuba ambayo ilitanguliwa na hotuba fupi za mbunge aliyemaliza muda wake wa CCM kwa jimbo la Bunda, Stephen Wassira, na ya mbunge mwingine wa CCM aliyemaliza muda wake katika jimbo la Musoma Mjini, Vedasto Mathayo, na ya Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Mara, Makongoro Nyerere, Rais Kikwete alitoa ahadi mbalimbali za chama chake kwa wapiga kura iwapo atachaguliwa kuongoza tena kuanzia Oktoba.

Aidha, aliorodhesha yale aliyoyataja kama mafanikio ya serikali yake katika kipindi cha miaka mitano iliyopita kwenye sekta za afya, maji, umeme, barabara, kilimo na ufugaji.

Ahadi nazo zilikuwa nyingi tu katika sekta zote muhimu, zikiwa ni pamoja na kumalizia ujenzi wa hospitali ya Kwangwa iliyopo Musoma; mpango wa kuongeza matumizi ya serikali kupambana na ugonjwa wa Malaria kwa matumizi ya chandarua, pamoja na kunyunyuzia dawa za kuua mbu. Alitaja pia mpango wa ushirikiano na nchi ya Cuba, nchi ambayo ilifanikiwa kufuta malaria kwa dawa zinazoshambulia mbu katika maeneo ya kuzalia.


Mgombea urais wa CCM alisema:
Nimekuja tena kuwaomba CCM iendelee kuongoza nchi yetu. Sababu ziko nyingi, nitataja mambo matatu. La Kwanza, hakuna chama kama CCM. Vyama vya siasa viko vingi, lakini kwa muundo, kwa mtandao, kwa sera, kwa mipango, mipangilio na uendelezaji hakuna hata kimoja kitaikaribia CCM.
Pili, tunaingoza vizuri nchi hii. Nchi imetulia, mafanikio yanaonekana dhahiri. Tanzania ilivyokuwa mwaka 1961 sivyo ilivyo leo, ilivyokuwa mwaka 2005 sivyo ilivyo leo. Na katika miaka mitano hii tumefanya mambo mengi ambayo huko nyuma yalionekana hayawezekani, tumeyaweza.
Tatu, sisi waaminifu.

Katika hotuba yake hawakusahau kina mama:
Wakipewa nafasi kina mama wanaweza. Kina mama niliahidi tutawapeni nafasi, mawaziri wengi katika baraza langu kuliko wakati mwingine wowote katika historia, majaji wengi. Kila mahali, tuliahidi [asilimia] hamsini kwa hamsini. Bunge lijalo wanawake watakuwa [asilimia] hamsini, na kina baba watakuwa [aslimia] hamsini.
Aliendelea:
Tuliahidi kuborehsa upatikanaji wa huduma mbalimbali: elimu, afya, maji, barabara, umeme, mitandao ya simu, na kadhalika.

Mwaka 2005, sekondari za Musoma zilikuwa na vijana 3,000. Leo sekondari zina vijana 10,777. Ameeleza mheshimiwa mbunge kuwa ziko changamoto za walimu, vitabu, maabara, na nyumba za walimu. Ni kweli. Lakini ni changamoto za maendeleo. Lakini sisi tumejiandaa kuikabili changamoto hiyo na tumepata mafanikio makubwa.

Tuliamua kupanua mafunzo ya ualimu katika vyuo vikuu, na vyuo vya ualimu kwa ngazi ya diploma. Mwaka 2005 tulikuwa tunapata kutoka vyuo vikuu walimu wasiozidi 600. Mwaka huu tutatoa walimu 12,124. Si mafanikio madogo. Ni mambo yanayofanywa na watu makini kama sisi, na yanatekelezwa na serikali makini kama serikali ya CCM.

Mwakani kila shule ya sekondari itapata walimu wasiopungua watano. Chuo Kikuu tulichojenga Dodoma kitatoa wanafunzi 40,000. Kati ya hao 15,000 ni wanafunzi waliyosomea ualimu. Tatizo la ualimu lipo?
Waliyomtangulia walisema yafuatayo:

Alianza Stephen Wassira:

Stephen Wassira, mgombea ubunge wa CCM kwa jimbo la Bunda, akihutubia wakazi wa Musoma jana
Watu wengine nao wamesema wanataka tuwachague. Lakini kilichonishangaza wakati nafuatilia maneno yao, nikagundua wanawadanganya Watanzania kwa ahadi za uongo. Mmoja anasema, 'mkinichagua mabati yatakuwa shilingi elfu tano.' Sasa mimi namuuliza: pale Ikulu kuna kiwanda cha mabati? Maana mabati ni bidhaa, inatengenezwa katika mazingira fulani ya uchumi. Kuna masuala ya gharama ya kuzalisha mabati hayo. Kuna gharama ya kusafirisha. Kuna mambo ambayo yako nje kabisa hata ya uwezo wa rais wa Watanzania. Bei ya mafuta ikipanda, huyo rais wa mabati ya shilingi elfu tano atayafanyaje? Anaongopa....Huyu anadanganya, tena anadanganya mchana.
Akafuatia Makongoro Nyerere:
Leo amekuja mgombea wetu wa urais, na kila harusi huwa haikosi wasindikizaji.Ukifika kwenye stendi ya mabasi kuna watu kadha wa kadha ambao wanashughulikia shughuli ya usafiri. Wapiga debe wapo, makonda wapo, na madereva wa magari wapo. Wewe ukifika pale stendi, hela yako unampa mpiga debe? Utafika? Usimpe hela yako mpiga debe, maana yeye ni mpiga debe tu. Mpe hela yako konda.
Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mara, Makongoro Nyerere, akiwa jukwaani muda mfupi kabla ya kumkaribisha mgombea urais wa CCM, Jakaya Kikwete, kwenye mkutano wa jana.
Leo mtu anataka kuwa raisi wetu aende akauweke mwenge [wa Uhuru] stoo. Halafu anakuja hapa anadanganya wana Musoma wenzangu eti yeye anamuenzi Nyerere. Wewe unamuenzi Nyerere mwenge wake unataka kwenda kuuweka stoo, ndiyo ujanja wako huo?


Akamalizia Vedasto Mathayo:

Katika kipindi cha miaka mitano...ilani ya uchaguzi tumeweza kuitekeleza barabara, tumeitekeleza kwa asilimia tisini. Mwaka 2005, tulisema kwamba lazima tuendelee kuboresha huduma za kijamii, na tukasema: kipaumbele chetu cha kwanza tutakipeleka kwenye elimu. Ilani yetu ya uchaguzi ilikuwa inatuagiza 2005 - 2010 kila kata iwe na sekondari moja. Kazi hiyo tumeifanya vizuri...tunazo sekondari 15.

Rais Kikwete, kushoto, akiwa na mgombea ubunge wa CCM kwa jimbo la Musoma Mjini, Vedasto Mathayo, kulia, kwenye mkutano wa jana 
Hakuna mtoto wa Musoma Mjini hata mmoja aliyefaulu akashindwa kwenda sekondari. Pale ambapo wazazi hawana uwezo, Serikali ya Chama cha Mapinduzi kila mwaka kwa  Musoma Mjini, inasomesha watoto zaidi ya 250 bure.

Aliendelea kutaja mafanikio kwenye ujenzi wa barabara, sekta ya afya, na maji. Alimuomba mgomea urais wa chama chake aweke nguvu katika ujenzi wa barabara.

No comments: